About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Monday, February 10, 2014

WAFANYABIASHARA SONGEA WAIGOMEA SERIKALI MASHINE ZA TRA

Na Stephano Mango, Songea.
 
WAFANYABIASHARA   wa maduka mbalimbali katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma wamegomea kufungua maduka  yao  kwa kile kinachodaiwa  kuwa    serikali imeshindwa kuwasikiliza kilio chao cha mashine za kielektroniki   (EFD) ambazo zinatakiwa kwa muda mrefu waliomba zishushwe bei .

Uchunguzi uliofanywa na waandishi wa habari  wa mjini Songea  umebaini kuwa  katika mitaa yote  ya Manispaa ya Songea  maduka yote yamefungwa  na kwamba katika eneo la soko kuu  kwenye vibanda  vinavyolizunguka soko hilo  navyo vimefungwa isipokuwa  wafanya biashara ndogondogo wanaouza mchele, unga , nyanya na mbogamboga ndio wanaoendelea kufanya biashara .

Badhi ya wafanya biashara  waliohojiwa  kuhusiana na mgomo huo walisema kuwa  kwa muda mrefu     waliiomba mamlaka ya mapato Tanzania (TRA)  Mkoa wa Ruvuma  iangalie uwezekano  wa kushusha   bei ya mashine  za kielektroniki  amabazo zimekuwa zikiuzwa kati ya shilling laki sita  na laki nane  jambo ambalo walidai kuwa bei hiyo wafanyabiashara wengi wanashindwa kuimudu .

Walisema kuwa hivi karibuni alifika mijini Songea Naibu Waziri  wa fedha Mwigulu Nchemba na kufanya mkutano mkubwa kati yake na  wafanya biashara  lakini alishindwa kutoa maelezo yakinifu kuhusiana na bei   ambayo imeonekana kuawa ni kandamizi kwa wafanyabiashara hao.

Walifafanua kuwa wafanyabiashara hawagomei kuzinunua mashine hizo isipokuwa wamedai kuwa kwa muda mrefu wamekuwa wakivutana kwa kuitaka serikali iangalie namna ya kuzishusha bei ambayo wafanyabiashara wanaweza kuimudu tofauti na hivi sasa.

 Wameelezakuwa  mawakala wa kuuza mashine hizo mkoani Ruvuma wameteuliwa wachache na kuonekana kuwa kuna viwingu namna ya upatikanaji wa mashine hizo hivyo wameiomba serikali itumie mfumo wa soko huria.

 Kwa upande wake meneja wa mamlaka ya mapato [TRA] mkoani Ruvuma Apili Mbaruku alithibitisha kuwa maduka katika manispaa ya Songea kuwa yamefungwa lakini alieleza kuwa ofisi yake inafanya utaratibu wa kuangalia tatizo jinsi lilivyo.

 Naye katibu mtendaji wa chama cha wafanyabiashara [TCCIA]mkoani Ruvuma ,Moyo akiongea kwa njia ya simu alisema kuwa kuanjia majira ya saa za asubuhi wafanyabiashara kwa pamoja waliamua kufunga maduka yao wakidai kuwa bei za mashine za kielektroniki ni kubwa tofauti na biashara wanazo zifanya lakini kufuatia tukio hilo la mgomo tayari mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu ameitisha kikao kwa mazungumzo zaidi.
 
Hata hivyo mkuu wa mkoa wa Ruvuma Mwambungu akiongea kwa njia ya simu alithibitisha kuwepo kwa mgomo huo na kwamba anatarajia kukutana na wafanyabiashara pamoja na maafisa kutoka mamlaka ya mapato ili kuangalia tatizo hilo.
    MWISHO.
 

Wednesday, January 29, 2014

LOWASSA HATARINI KWA TAMKO LA VIJANA



 Paul Christian Makonda,Katibu wa Hamasa na Chipukizi.
“..Chama Cha Siasa chochote duniani hubomoka kutokana na migongano iliyokithiri ya muda mrefu. Uzoefu wa vyama vikubwa vilivyoporomoka umeonyesha hivyo! Chama lazima kidhibiti uchu wa madaraka wa baadhi ya viongozi wake na ndani ya serikali yake...” – Dr Eginald P. Mihanjo
“..Chama cha siasa ni itikadi. Chama cha siasa ni siasa kwa maana halisi ya neno lenyewe siasa –“siasa”. Ni mahali ambapo watu wenye madhumuni mamoja yaliyoainishwa waziwazi hukutana na kuwa kitu kimoja. Chama cha siasa sio mkusanyiko wa “majini dume yenye tamaa”, - majini ambayo yametanguliza mbele tamaa kufa na kupona-tamaa ya kutengeneza pesa au kupata vyeo kwa gharama yoyote! – Dr Bashir Ally

UTANGULIZI:
Hili ni tamko la vijana makini wa jumuiya ya umoja wa vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) kuunga mkono juhudi na utendaji wa sekretarieti ya halmashauri kuu ya Chama Cha Mapinduzi ikiongozwa na Katibu Mkuu Komredi Abdulrahaman Kinana.

Maneno ya utangulizi yamebeba dhima ya tamko hili, kufuatia taarifa zilizoripotiwa kwenye baadhi ya vyombo vya habari vikiwanukuu baadhi ya wanachama wa Chama Cha Mapinduzi, wakiwatuhumu Viongozi wa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM, Katibu Mkuu Ndugu Abdulrahaman Kinana na Katibu wa Itikadi na Uenezi Ndugu Nape Moses Nnauye.

Sisi Vijana tunatambua kuwa tuhuma hizo na maneno hayo ya hovyo yametolewa kwa nia ovu yenye kulenga kuwakatisha tamaa Viongozi hao wa Chama. Tunafahamu kuwa upo mkakati wa kiuhaini ulioandaliwa na kuratibiwa na “mtandao” ndani ya Chama ambao umejipanga kuendesha uhaini huo.

Sisi vijana wa UVCCM tunatambua na kuthamini juhudi za Katibu Mkuu na Sekretarieti yake katika kukijenga na kukiimarisha Chama kwa kuisimamia barabara misingi na shabaha ya kuundwa kwake, katika umri wetu hatukuwahi kuona Chama kikiwa karibu na wananchi kwa kufuatilia, kusikiliza na kushiriki katika utatuzi wa kero, shida na changamoto zao kama ilivyo katika kipindi hiki chini ya Comrade Kinana na timu yake. Juhudi hizi ni za kuungwa mkono na kamwe si za kubezwa na mwanaCCM muadilifu, muaminifu na mwenye mapenzi ya kweli kwa Chama.

Juhudi za kukiimarisha Chama kutoka ngazi za chini, kwa mabalozi ni mkakati bora kuwahi kutekelezwa na Chama, kukirudisha Chama kwa wanachama ni kutimiza lengo la kuundwa kwa Chama hiki, Chama hiki ni cha wanyonge, masikini wa Taifa hili, HAIWEZEKANI matajiri watake kukihodhi na waratibu mikakati ya kukihujumu kwa pesa zao hali sisi vijana tukitazama, tunasema tutakilinda Chama chetu na tutawalinda viongozi wetu waadilifu.

Ni hawa ambao wanabezwa leo ndio wameweza kurudisha Imani ya wananchi kwa Chama, Imani na matumaini ambayo tayari yalishaanza kupotea na Chama kuonekana si tena cha wanyonge, wakulima na wafanyakazi wan chi hii.

Ni Comrade Kinana na timu yake ndio waliozunguka kwenda kukutana na wakulima wa Pamba kule mikoa ya Kanda ya ziwa na kumpeleka balozi wa China na kumshawishi kujenga viwanda ili kuboresha manufaa kwa wakulima.

Ni Comrade Kinana na timu yake ndio waliokwenda Kusini kukutana na wakulima wa Korosho na kushirikiana nao pamoja na bodi kutatua tatizo la Korosho.

Ni Comrade Kinana na timu yake ndio walioibua hoja na kero za wafugaji, walimu na wananchi kwa ujumla, na kuwataka viongozi wa Serikali kuhakikisha wanawajibika kwa wananchi walipa kodi wa Taifa hili.

Kupinga mafanikio ya Ziara hizo ni kupinga utetezi wa wanyonge.

Mtu anayebeza ziara hizo na kuwaita Viongozi waliozifanya waropokaji na wahuni wahuni ni mtu mjinga, mtu wa hovyo,hana maadili, asiyekipenda Chama, mhaini na mzandiki anayepaswa kuchukuliwa hatua kali za kinidhamu ili iwe fundisho kwa wengine.

TAMKO hili limezingatia wosia wa Baba wa Taifa, muasisi wa Chama Cha Mapinduzi Mwl Julius Kambarage Nyerere katika kitabu Chake TUJISAHIHISHE.

“Inapofikia wasimamizi wa Kanuni za Chama wanapigwa vita ya wazi kwa uamuzi wao wa kukisimamia Chama, tafsir yake ni moja tu watu wanaowapiga vita hawakitakii mema chama chetu.”

Imetolewa na Paul Christian Makonda.

Katibu wa Hamasa na Chipukizi.

Monday, January 27, 2014

WAFANYABIASHARA MANZESE WAUCHARUKIA UONGOZI WAO



Na, Stephano Mango, Songea
WAFANYABIASHARA  wa Soko la Manzese B lililopo katika halmashauri ya Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma wameutaka Uongozi wao ujiudhuru mara moja kutokana na utawala mbovu wanaoufanya na kuendeleza vitendo vya hujuma katika soko hilo

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na waandishi wa Habari jana katika viwanja vya soko hilo walisema viongozi hao wamekuwa wakishirikiana na Viongozi wa Halmashauri ya Manispaa kukiuka maadili ya uongozi na kusababisha migogoro ya mara kwa mara inayopelekea uvunjifu wa amani

Walisema kuwa toka kuwepo kwa mpango wa ujenzi wa vibanda 68 vya Soko hilo, viongozi wamekuwa wakifanya vikao vya siri vya kuwahujumu wafanyabiashara waliopo sokoni hapo kwa kupanga mipango ya kuwanyang’anya ili vibanda hivyo wapewe wafanyabiashara  vigogo ambao hawafanyi biashara katika soko hilo

Walisema kuwa mipango hiyo ya siri imezua malalamiko makubwa sana miongoni mwa wafanyabiashara kwani makubaliano ya awali yalikuwa ni lazima wafanyabiashara waliopo wapewe kipaumbele katika ujazaji wa mikataba katika ujenzi huo

“ Tunashangaa kuona viongozi wa Soko na Viongozi wa Halmashauri wanatoa mikataba kwa siri kwa wafanyabiashara vigogo kutoka maeneo mengine kinyume na utaratibu kitendo ambacho kimetusikitisha sana kwani hakijawa na uhalali wa kidemokrasia zaidi ya ubabe”

Walisema hali hiyo inaonyesha wazi kabisa kuwa kuna vitendo vya rushwa, ukiukwaji wa haki za binadamu kwani mara kwa mara wafanyabiasha wakihoji uhal wa mambo ambayo yanafanywa na viongozi hao wanatishiwa kwa maneno ya kuudhi

Akizungumza na Waandishi wa Habari Mwenyekiti wa Soko hilo Omary Masai alisema kuwa yeye sio msemaji wa jambo hilo kwani linafanywa Mstahiki Meya wa Halmashauri Charles Mhagama hivyo kwa maelezo zaidi atafutwe yeye

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Misufini ambako soko hilo lipo Salumu Mfamaji alisema kuwa ujenzi huo unafanywa kihuni kwani kuanzia viongozi wa Serikali ya Mtaa na Serikali ya Kata haijashirikishwa na kuwa jambo hilo linaonekana limegubikwa na rushwa

Mfamaji alisema kuwa amewasiliana na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea Nachoa Zakaria na wataalamu wake kusitisha mara moja ujenzi huo mpaka pale mkutano wa wafanyabiashara utakapoitishwa ili waweze kutendewa haki ikiwemo ya kuonyeshwa ramani ya Soko hilo na mikataba

Naye Meya wa Manispaa hiyo Charles Mhagama alipohojiwa kuhusiana na malalamiko ya Wafanyabiashara alisema kuwa tatizo hilo lipo lakini alidai kuwa msababishaji mkubwa ni Diwani wa kata hiyo na ndio maana Halmashauri imeamua kusimamia yenyewe ujenzi huo

Hata hivyo juhudi za kumtafuta Mkurugenzi wa Halmashauri kupitia simu yake ya kiganzani Nachoa Zakaria ziligonga mwamba kwani simu yake ilikuwa inaita tu bila kupokelewa

MWISHO

Sunday, November 10, 2013

UBAYA ALETA UBAYA CHUO CHA UALIMU SONGEA





Ni jengo la Utawala ambalo ni Ofisi ya Ubaya Suleiman Salum ambaye ndiye Mkuu wa Chuo Cha Ualimu Songea

HALI TETE CHUO CHA UALIMU SONGEA, WIZARA YA ELIMU YAMBEBA MKUU WA CHUO.

Na, Stephano Mango, Songea

Ni takribani miezi nane sasa tangu nianze kufuatilia  uendeshaji wa chuo cha Ualimu Songea kama kinaweza kuendana na kauli mbiu ya sasa ya Serikali ya Big Result Now (Matokeo Makubwa Sasa)

Nimelazimika kukifuatilia Chuo hicho kutokana na mgogoro mkubwa uliopo kati ya wafanyakazi (wakufunzi) na mkuu wao wa chuo Ubaya Suleiman.

Mgogoro huo umetokana na uongozi mbovu usiozingatia misingi ya uongozi na Demokrasia katika vyuo vya ualimu Tanzania kwani Mkuu huyo wa chuo amekuwa na lugha za matusi,vitisho kwa wafanyakazi na wanachuo, kutopokea ushauri kwa washauri wake, mbinafsi, kutowaamini watendaji wake kwa nafasi alizowateua, kufanya kazi kwa kutumia vyanzo visivyo rasmi, Matumizi mabaya ya fedha za Serikali na vyombo vya usafiri

Pamoja na hayo mkuu huyo wa chuo amediriki kuwapeleka baadhi ya wafanyakazi wake kwenye vyombo vya dola (polisi) (kuwatishia) akiwatuhumu kuwa wanataka kumuua. Baada ya mgogoro huo kutopata suluhu kupitia vikao vya ndani, Jitihada zifuatazo zilifanyika na wafanyakazi wa chuo hicho ili kuleta hali ya amani na utulivu wa chuo;

Tarehe 27/04/2013 walifanya kikao na mkuu wa wilaya ya Songea Joseph Mkirikiti, tarehe 15/05/2013 na tarehe 01/06/2013 walifanya kikao na Bodi ya ushauri ya Chuo, hata hivyo suluhu ya mgogoro huo haikupatikana. 

Kutokana na hali hiyo Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Profesa Sifuni Mchome aliunda tume ya watu watano ikiongozwa na Mkaguzi Mkuu wa shule na vyuo wa nyanda za juu kusini ambaye alifahamika kwa jina moja la Lyapambile, kuja kufanya utafiti wa chanzo cha mgogoro, lakini mpaka sasa tume hiyo haijatoa majibu ya uchunguzi wa jambo hilo 

Tume hiyo haikuishia hapo tarehe 13/08/2013 wafanyakazi walifanya kikao na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu, ambaye baada ya kusikiliza mgogoro huo aliahidi kuleta suluhisho la kudumu mapema iwezekanavyo ili kuleta amani na utulivu(peace and Tranquility) chuoni hapo. 

Lakini cha kushangaza hadi sasa yapata miezi mitatu hakuna kilichofanyika hali ambayo imeendelea kuwavunja moyo wafanyakazi wa chuo hicho.

Licha ya jitihada zilizofanywa, Mkuu huyo wa Chuo Ubaya Suleiman anaendelea kuwanyanyasa wafanyakazi wake na kusema pigeni kelele lakini wakuning’oa mimi hapa hayupo na lugha zingine ambazo sio za ustaarabu anazitoa, na kuwafanya wafanyakazi wenzake wahoji nguvu aliyonayo katika utendaji, mfano wa lugha zake mbovu ni “kwani mizizi yangu ni mirefu”. Kitendo hicho kinawafanya wafanyakazi wa chuo na wadau wengine watilie mashaka juu ya sifa za uteuzi wake kushika nafasi kubwa kama hiyo.

Tunamuomba Waziri wa Elimu na mafunzo ya ufundi Shukuru Kawambwa na Naibu wake Philipo Mulugo kumuondoa mkuu huyo wa chuo madarakani na kumtafutia shughuli nyingine ya kufanya kwa ustawi wa chuo cha ualimu songea, taaluma ya ualimu Tanzania na ili kuleta ufanisi wa kauli mbiu ya serikali ya Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (Big Results Now)  

Sababu zinazopelekea hilo ni nyingi ila kwa sasa nitazitaja chache ili kuweka kumbukumbu sawa, ya kwanza Novemba 1, 2013 Mkuu huyo wa chuo bila kuwasiliana na Mtaaluma wake wa Chuo Maiko Luoga, alidiriki kuwaandikia Barua Wakufunzi kuwataka watunge Mtihani wa Moko wa Ualimu viwango vya Baraza la Taifa la Mitihani(NECTA) kwa lugha ya kejeri hali ambayo imesababisha maudhi na utulivu wa akili miongoni mwa wafanyakazi katika kufanikisha utungaji wa mitihani hiyo

Kitendo hicho licha ya kuwa ni kinyume na utawala bora , lakini pia kimekiuka maagizo ya Bodi ya Chuo ambayo yalitolewa tarehe 28/8/2013 (……. mambo yote yanayohusu fedha yaendeshwe kwa uwazi na ushirikishwaji mkubwa miongoni mwa wanaidara / taasisi kwani inaonekana mambo yanaenda kwa usiri mno).

Sababu ya pili amekuwa na vitisho vingi katika utendaji wake na maneno ya kuudhi dhidi ya viongozi wenzake , mfano wa maneno yake ambayo anayatamka huku akigonga meza kuashiria ubabe na kiburi cha madaraka ni kama vile,(…. Ukiingia ndani ya kumi na nane zangu nakumaliza, Angalieni msije mkaumia wengine tunambavu za chuma, Nipo tayari kuua inzi kwenye kioo cha TV hata kama itavunjika potelea mbalimbali raha yangu ni kuhakikisha inzi amekufa, Mkitoboa mtumbwi nitahakikisha kabla sijazama mimi nawazamisha ninyi kwanza, Angalia wengine watakaanga mbuyu na kuwaachia wenye meno watafune, Amekuwa akitishia kung’oa mtu kwa kumwendea (kumpandia)wizarani ndani ya siku mbili na kumchukulia barua ya uhamisho kwenda vyuo vya pembezoni mwa Tanzania, Mimi nafanya haya hata niking’olewa kwa muda mfupi potelea pote nitakuwa nimejenga historia)

Sababu ya tatu ni kutokuwa na uwazi, ukweli na ushirikishwaji kwa njia ya kidemokrasia miongoni mwa idara zake katika chuo hicho na hasa katika fedha ambazo zinakuja kwa ajiri ya manunuzi ya vitu mbalimbali, fedha ya kuendeshea mafunzo ya ualimu kwa vitendo(BTP)

Fedha hiyo licha ya kuchelewesha kuitoa kutokana na ufisadi wake lakini pia hakuitoa yote na wala hakueleza kwa uwazi na ukweli, hali ambayo haikuwezesha wakufunzi  kwenda kufanya kazi stahiki kwenye maeneo kusudiwa ya kuwatahini wanachuo ambao walikwenda kwenye shule mbalimbali kwa ajili ya mazoezi ya kufundisha kwa vitendo.

Sababu ya nne ni uwezo wake wa kiuongozi kwani kumekuwepo na mashaka mengi katika Wasifu wake wa kielimu na kiutendaji, hali inayopelekea kuendesha Chuo katika misingi binafsi bila kuzingatia Kanuni, Sheria na Taratibu za Wizara.

Kutokana na hayo yote Chuo hicho kimejikuta kikiingia kwenye mgogoro wa muda mrefu na mkubwa na kupelekea shughuli zote za kiutendaji chuoni hapo kutofanyika katika viwango vyenye ubora na kwa wakati na hasa pale anaposafiri mambo huwa yanasimama, kwani mara nyingi utendaji wote anaufanya yeye mwenyewe na wakati mwingine huwa anajiita Chief Accountant na kumuona Makamu wake kuwa hana uwezo wala mamlaka ya kutoa maamuzi kwa mustakabali wa chuo

Ni mengi ambayo nimeyabaini na ushaidi upo wazi kuwa Mkuu huyo wa Chuo hafai kuendelea kuongoza Chuo hicho kwani Wakufunzi, Wafanyakazi na Wanachuo hawana imani nae, na wanafanya mambo mengi bila morari ya utendaji kutokana na mazingira mabovu ya utendaji kazi katika chuo hicho

Nimefanya jitihada za kukutana na baadhi ya Wakuu wa Idara Chuoni hapo na kupata majibu ambayo yanaonyesha ukataji wa tamaa kutokana na mazingira mabovu ya kiutawala ambayo yanaonyeshwa na Mkuu wa Chuo hicho katika kufanikisha mpango mkakati wa matokeo makubwa sasa,

Pia nimebahatika kuwauliza viongozi wa Bodi akiwemu Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo ambaye amejitambulisha kwa jina la H,Lugome naye pia ameonyesha masikitiko makubwa sana juu ya utendaji wa Mkuu wa Chuo hicho

Lakini pia Mkuu wa Wilaya ya Songea Joseph Mkirikiti ambaye pia ameshiriki kusuluhisha mgogoro huo katika kikao chake cha April 27, 2013 lakini ameshindwa na kukata rufaa kwa kulipeleka swala hilo kwa Mkuu wa Mkoa ili aweze kuliingilia kati

Naye Naibu Waziri wa Wizara ya Elimu Philipo Mulugo alipo tafutwa kupitia simu yake ye kiganjani yenye namba  hii 0754315922 alijibu kuwa swala hilo bado halijafika mezani kwake na endapo likifika basi atachukua hatua stahiki za kinidhamu na kisheria dhidi ya Mkuu yoyote wa Chuo ambaye atakwamisha malengo na ufanisi wa kazi nchini

Kutokana na hayo na mengine mengi ni dhahiri kuwa utendaji wa kazi katika chuo cha  Ualimu Songea kilichopo eneo la Matogoro Mkoani Ruvuma wilayani Songea ni mgumu miongoni mwa Wafanyakazi na kusababisha hali ya sintofahamu katika Saikolojia zao na mustakabali wa Elimu ya wanachuo

Ni vema sasa mamlaka zinazohusika zikachukua hatua stahiki za kumaliza mgogoro huo ikiwemo na kumuondoa Mkuu huyo wa Chuo ili kurudisha Amani na Utulivu chuoni hapo miongoni mwa wanajumuia wanaokizunguka chuo hicho ili kuweza kufanikisha mikakati mbalimbali iliyopo nchini ya kuhakikisha kuwa elimu bora inafikiwa nchini hapa

Mwandishi wa Makala hii
Anapatika kwa 0755-335051 AU 0715-335051
Barua pepe,stephano12mango@yahoo.com
www.stephanomango.blogspot.com

Saturday, October 26, 2013

DKT NCHIMBI APIGWA MAWE SONGEA NA MSAFARA WAKE


Waziri wa mambo ya Ndani ya Nchi Dkt Emmanuel Nchimbi ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Songea Mjini

Na Stephano Mango,Songea

MSAFARA wa Waziri wa mambo ya Ndani ya Nchi Dkt Emmanuel Nchimbi ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Songea Mjini Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma wapigwa mawe na wananchi waliojitokeza kuzungumzia kero ya daraja la Matarawe ambalo linadaiwa kusababisha vifo vya watu zaidi ya watatu katika mwezi huu wa octoba mwaka huu

Wananchi hao wa kata ya Matarawe  Manispaa ya Songea,wakiwemo waendesha  Pikikipiki maarufu kwa jina la Yebo Yebo  walifunga barabara kwa  zaidi ya masaa mawili na kufanya fujo za kung’oa kingo za daraja  pamoja na kuweka  magogo na mawe  katikati ya daraja na kuchoma matairi moto  ili Mbunge huyo asipite mpaka atoe majibu ya kina kuhusu daraja

Hali hiyo ililazimisha Jeshi la polisi kuwatawanya  wananchi hao kwa kuwafyatulia mabomu ya machozi kwa lengo la kuzuia uharibifu zaidi na kuufanya msafara upite wakati ukirudi kutoka kwenye Mkutano wa hadhara wa Matarawe baada ya kuzuiriwa wakati wa kwenda na wakati wa kurudi ambapo hadi sasa watu nane wanashikiliwa na Jeshi hilo kutokana na vurugu hizo.

Tukio hilo limetokea jana kati ya saa kumi  hadi saa kumi na mbili jioni  ambapo wananchi hao wakiwa na hasira walifanya fujo hizo  wakiwa na lengo la kumshinikiza Mbunge wa Jimbo la Songea  mjini ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Dkt.Emmanuel Nchimbi  awasaidie kupanua daraja  la mto Matarawe ambalo ni dogo kwani kwa  muda mrefu limekuwa likisababisha ajalli mara kwa mara katika eneo hilo kutokana na ufinyu wa daraja hilo.

Awali  Mbunge huyo akiwa katika ziara yake ya siku ya pili akitokea  mtaa wa Liumbu kata ya Mletele  kukagua shughuli mbali mbali za maendeleo pamoja na kuzungumza na wananchi akiwa anaelekea kata ya matarawe  kwenye mkutano wa hadhara ndipo alikutana na umati mkubwa wa wananchi wakiwemo  waendesha piki piki  walikuwa wamezuia njia na kusimama njiani ili asikilize kero zao kutokana na watu kufa mara kwa mara ambapo siku moja kabla ya mbunge huyo kufanya ziara kuna kijana aliyetambulika kwa jina la Mashaka Nuhu mkazi wa Matarawe akiwa anaendesha piki piki alitumbukia mtoni na kufariki dunia papo hapo.

Hata hivyo Dkt.Nchimbi alilazimika kusimama na kushuka kwenye gari yake  akiwa ameongozana na viongozi mbali mbali wa  chama na Serikali akiwemo Mkuu wa Wilaya ya Songea Joseph Joseph Mkirikiti  ambapo Mbunge huyo aliwapa pole kwa ajali zinazotokea na kwa watu ambao wamepoteza ndugu zao alizungumza nao na kuwataka wawe na subira  wakati ombi lao linashugulikiwa, majibu ambayo wanachi hao hawakulizika nayo

“Natoa pole sana kwa msiba na ajali ambazo zimetokea nimewasikia, na ninaahidi  nitawajengea daraja  hili ,kama nimeweza kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami bila maandamano wala kufungiwa barabara nitashindwa daraja? hivi ni vitu vinavyozungumzika  hili ni jambo dogo hivyo naomba  twende kwenye mkutano wa hadhara na tutaongea vizuri zaidi , kwani ni kweli daraja ni finyu na linahitaji kufanyiwa maboresho zaidi, ‘alisema Dkt. N chimbi.

Dkt.Nchimbi akiwahutubia Wananchi  kwenye mkutano wa hadhara  uliofanyika kwenye viwanja vya  Shule ya sekondari ya kutwa ya matarawe  amesema,amesikitishwa na tukio hilo kwani tabia hiyo haipendezi ,haikubaliki na haina maadili na aina
tija kama wangekuwa na busara wangefika kwenye mkutano na kutoa kero zao badala ya kufanya fujo ambapo ameliagiza jeshi  la polisi kuwasaka wahusika wa fujo hizo.

Amesema, ni kweli daraja hilo ni dogo ila siyo ustarabu kufunga barabara kwa masaa mawili kwani wamesababisha shughuli mbali mbali za maendeleo kusimama kutokana na barabara hiyo kufungwa  na kwamba tayari ameshamuagiza Mhandisi wa halmashauri ya Manispaa hiyo kufanya tathmini ili kujua gharama zinazohitajika ili liweze kupanuliwa.

Mapema Diwani wa kata ya Matarawe James Makene aliungana na kundi kubwa la wananchi hao na alimweleza Nchimbi kuwa  hiyo ni changamoto ambayo wakazi wa matarawe  wamekuwa wakilia kila mara hivyo wanahitaji msaada wa kupanua daraja hilo ambalo limeonekana kuwa ni kero ya muda mrefu.

Kwa upande wake kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma Deusdedit Msimeki ameeleza kuwa kufatia vurugu hizo tayari watu nane wanashikiliwa na wanaendelea kuhojiwa zaidi ili kuwabaini vinara wengine wa fujo waliowashawishi wananchi kufanya fujo hizo .
MWISHO.

Thursday, October 3, 2013

MASHINE ZA TRA ZAZUA BALAA, WENGINE WASHUSHIANA MKON'GOTO



Na Kenneth Ngelesi

WAFANYABIASHARA mkoani Mbeya wamezua kizaazaa wakigoma kufungua maduka wakipinga agizo la Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) linalowataka kununua mashine za kielektroniki kwa ajili ya kukatia risiti za wateja pindi wanapowauzia bidhaa.

Katika sokomoko hilo lililotokea jana na kusababisha taharuki kwa muda kadhaa, wafanyabiashara hao wanadai kuwa gharama za mashine zitolewe na serikali.

Eneo la Soko la Sido ambalo lina wafanyabiashara wengi na tegemeo katika uchumi wa Jiji la Mbeya, walifunga biashara zao kwa muda usiojulikana.

Kadhia hiyo inakuja siku moja tangu Mkuu wa Mkoa huu, Abbas Kandoro, akutane na viongozi wa wafanyabiashara kutoka Soko la Sido na kuwataka viongozi kuwataarifu wenzao wasitishe mkutano ambao walitaka kuufanya jana katika uwanja wa Shule ya Msingi Ruanda Nzovwe.

Kandoro alifikia uamuzi wa kukutana na viongozi hao baada ya kupata taarifa kupitia gari la matangazo ambalo lilikuwa likipita na kuzunguka katikati ya jiji na kuwataka wafanyabiashara hao kufunga maduka na kufika mkutanoni ili kujadili suala zima la mashine hizo.

Taarifa zinadai kuwa baada ya Kandoro kusikia matanagzo hayo, aliliagiza Jeshi la Polisi kumkamata dereva wa gari hilo pamoja na Mwenyekiti wa Soko la Sido na kuwaweka rumande kwa muda usiojulikana.

Baada ya wawili hao kuwekwa ndani, lilitolewa agizo la kuzunguka tena mitaani kwa kutumia gari hilo ili kuwatangazia wafanyabiashara hao kuwa mkutano huo umesitishwa.

Uamuzi wa kusitisha mkutano huo ulipuuzwa na wafanyabiashara hao ambao jana waliendelea na maandilizi ikiwa ni kukodi gari jingine la matangazo kupita mitaani kuwahimiza wenzao kujitokeza kwa wingi. 

Hatua hiyo iliufanya uongozi wa mkoa kuwasambaza polisi mitaani kuzuia mkutano huo. Mabomu ya machozi na maji ya kuwasha vilitembezwa kwa wafanyabiashara hao ambao walikuwa wamekusanyika huku maduka yao yakiwa yamefungwa.

Mabomu hayo ya polisi yaliwaathiri wanafunzi wa Shule ya Msingi Kagera na kuwafanya wataharuki na kuanza kukimbia hovyo huku wengine wakizirai.

Kufuatia hali hiyo, Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Ayoub Kiwanga, Ofisa Mtendaji wa Kata ya Ilomba, Erasto Mwakaponda na Diwani wa kata hiyo, Dickson Mwakilasa, walikubaliana kuwakabidhi wanafunzi hao kwa wazazi wao waliofika shuleni hapo kuwajulia hali baada ya kupokea taarifa za kupigwa mabomu.

Wakizungumza na Tanzania Daima, wafanyabiashara hao walisema kuwa wanashindwa kuelewa nguvu kubwa ambayo inatumiwa na polisi wakati hakuna vurugu zozote katika eneo hilo.

Alex Oswald, kwa niaba ya wenzake alisema kuwa wao waliamua kufunga maduka kwa hiari yao na kwamba lengo la mkutano lilikuwa kutoa msimamo wa kuiomba serikali itoe mashine hizo bure.

Naye Peter Tweve, alisema kuwa kimsingi wao hawajagoma kutumia mashine hizo bali wanataka wawekewe bure, kwani si kila mfanyabiashara anaweza kuinunua mashine hiyo ambayo kwa sasa inauzwa kwa sh 800,000.

Alipotafutwa Kandoro kuelezea tukio hilo, aligoma akisema kuwa yupo katika kikao, pia Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Diwani Athumani, simu yake iliita bila kupokewa.

Wiki moja iliyopita, Mkurugenzi wa Elimu ya Kodi wa TRA, Richard Kayombo, alitoa taarifa kuwa wafanyabiashara wenye mapato ya zaidi ya sh 45,000 kwa siku wanapewa hadi Oktoba 14, mwaka huu wawe wamenunua mashine hizo.

Friday, September 20, 2013

WAZIRI AMTISHA JK

Na, Betty Kangonga

WAZIRI wa Sheria na Katiba, Mathias Chikawe amemtisha Rais Jakaya Kikwete akisema kuwa endapo hatasaini muswada wa sheria ya marekebisho ya sheria ya mabadiliko ya katiba wa mwaka 2013, atakuwa ameingia kwenye mgogoro na Bunge.

Muswada huo uliopitishwa hivi karibuni na wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) pamoja na Augustine Mrema wa TLP (Vunjo), unapingwa vikali na vyama vya upinzani pamoja na makundi mbalimbali ambayo sasa yanamshinikiza rais asiusaini kuwa sheria.

Makundi hayo ambayo yamepata msukumo wa vyama vitatu vya CHADEMA, CUF na NCCR-Mageuzi ambavyo wabunge wake walikataa kuujadili muswada huo wakipinga uchakachuaji uliofanyika wa kuongeza vifungu na kutoishirikisha Zanzibar, tayari yametishia kwenda kortini ikiwa watapuuzwa.

Akizungumza jana na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Chikawe alisema kuwa ni vyema makundi mbalimbali yakaacha kumlaghai Rais Kikwete ili asiusaini muswada huo.

Kwa mujibu wa Chikawe, iwapo Rais Kikwete ataliafiki suala hilo la wapinzani na makundi mengine, na kuacha kutia saini muswada huo, atakuwa ametengeneza mgogoro na mhimili wa Bunge kutokana na chombo hicho kukamilisha kazi yake.

Alisema kuwa taratibu zote zilifuatwa kuhusiana na kupitishwa kwa muswada huo, na kudai kushangazwa na baadhi ya makundi yanayopiga kelele.

“Hao wanaolalamikia juu ya jambo hilo hawatendi haki kwani sheria zote zilifuatwa na hayo mapendekezo wanayotoa ya kutaka Rais Kikwete asitie saini sio sahihi hata kidogo, huko ni kutaka ‘kumblack mail’ na kumsababishia mgogoro na Bunge,” alisema.

Waziri Chikawe alisema kuwa ameshangazwa na baadhi ya matamshi yanayotolewa juu ya kuwepo kwa fujo au kumwagika damu na kusema jambo hilo haliwezi kufanikiwa kama halijapangwa.

“Fujo zinapangwa, hivyo wale wanaotaka kumwaga damu ni vyema wakajitaja na kusema kuwa ‘sisi tutamwaga damu’ kwa kuwa naamini damu haiwezi kumwagika yenyewe,” alisema.

Waziri huyo alisema kuwa ni vyema wale wanaotaka kuzunguka kwa wananchi na kufanya udanganyifu juu ya suala hilo, wangekubali kuwasilisha hoja hizo ndani ya Bunge na si mahali kwingine.
Kuhusu Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria kutopeleka muswada huo kwa wananchi wa Zanzibar, 

Chikawe alisema kuwa utaratibu uliotumika ni hisani tu, kwani hakuna sheria inayotaka muswada wa aina yoyote kupelekwa kwa Watanzania.

“Utaratibu wa kupitisha muswada huo sio huo tu, bali zipo njia nyingi ambapo anaweza kuandika anayohitaji na kuwasilisha kwa kamati ya Bunge na wapo waliofanya hivyo,” alisema.
Chikawe aliongeza kuwa inawezekana Kamati ya Katiba na Sheria ikawa na  sababu za kushindwa kuwafikia wananchi wote, lakini kwa upande wao walipokea maoni ya Serikali ya Zanzibar yaliyotolewa Mei 27, mwaka huu.

Alisema kuwa moja ya pendekezo lililotolewa na Serikali ya Zanzibar ni juu ya kuongezwa kwa siku 20 kati ya 70 zinazotakiwa kutumiwa na Bunge Maalumu la Katiba.
Chikawe alisema kuwa ni vyema yale yanayoenda kutolewa kwenye mkutano wa wapinzani kesho katika viwanja vya Jangwani, yangepelekwa bungeni kwa kuwa hata wakitoa katika viwanja hivyo haitasaidia.


ju





Thursday, September 19, 2013

WAANDISHI WAKWIDWA , WANYANYASWA NA KUPOKEA KIPIGO




Na Dixon Busagaga, Moshi

WAKATI watuhumiwa wanne zaidi wakiongezwa katika kesi ya mauaji ya mfanyabiashara wa madini ya tanzanite mkoani Arusha, Erasto Msuya, waandishi wanaoiripoti jana walionja joto ya jiwe kwa kukwidwa na kutaka kunyang’anywa vitendea kazi vyao.

Tafrani hiyo ilitokea katika Mahakama ya Hakimu Mkazi mjini Moshi saa 5:30 wakati kesi hiyo inayowakabili washtakiwa saba wanaodaiwa kushiriki kupanga na kutekeleza mauaji ya Msuya ilipofikishwa mbele ya mahakama kwa ajili ya kutajwa.

Akizungumzia tukio hilo, mmoja wa waandishi hao, Fadhili Athuman alisema kuwa walipata wakati mgumu walipojaribu kuchukua picha za ndugu wa Msuya.

Athuman alisema kuwa baada ya kupiga picha kadhaa, alikwidwa na wanafamilia hao, wakitaka kumpora kamera huku mwandishi mwenzake akishikwa na kupigwa kibao.

“Baada ya kesi kuahirishwa iliibuka tafrani, walitaka kuninyang’anya kamera ili wafute picha nilizokuwa nimepiga. Mwenzangu yeye alikamatwa na kupigwa vibao kabla askari wa kikosi cha FFU kumuokoa,” alisema.

Kwa mujibu wa mmoja wa watu wa karibu na familia ya Msuya ambaye aliomba kuhifadhiwa jina, wamechukizwa na hatua ya baadhi ya waandishi kutochapisha picha za watuhumiwa, na badala yake zinatolewa za wanafamilia hiyo.

Hali ya taharuki ilianza mapema baada ya chumba kilichozoeleka kuendeshea kesi hiyo kubadilishwa kwenda kwenye chemba kutokana umati wa watu uliohudhuria kuwa mkubwa.

Wakati huo huo, vilio viliendelea kutawala mahakamani hapo baada ya kesi hiyo kuahirishwa. Mama mzazi wa Msuya, Marry Msuya alipoteza fahamu na kukimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC.

Awali mbele ya Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Ruthi Mkisi, mawakili wa serikali, Stella Majaliwa akisaidiwa na Janeth Sipule waliieleza mahakama kuwa washitakiwa wanne wameunganishwa katika kesi hiyo na kufikia saba.

Majaliwa aliwataja waliounganishwa kuwa ni mshitakiwa wa nne hadi saba ambao ni Jalila Zuberi, Karimu Kihundrwa, Sadiki Jabiri (Chusa) na Joseph Mwakipasile ambao wote walifika mahakamani hapo.

Hakimu Mkisi alisema kesi hiyo imeahirishwa kutokana na upelelezi kutokamilika na hivyo kutaka washitakiwa hao kurudi rumande hadi Oktoba 2, mwaka huu.

Agosti 21, mwaka huu, washitakiwa watatu; Sharifu Mohammed, mkazi wa Kimandolu Arusha, Shaibu Mpungi, mkazi wa Kijiji cha Songambele wilayani Mererani na Musa Mangu mkazi wa Shangarai kwa Mrefu Arusha, walifikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza.

Washitakiwa wote saba waliondolewa mahakamani hapo chini ya ulinzi mkali wa askari wenye silaha za moto wakiwa ndani ya gari lenye namba za usajili T 743 ADC lenye vioo vyeusi.

Msuya aliuawa Agosti 7 mwaka huu saa 6:30 mchana kwa kupigwa risasi 13 kifuani, kando ya barabara kuu ya Arusha – Moshi katika eneo la Mjohoroni wilayani Hai.