About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Thursday, June 30, 2011

KILICAFE YATIMIZA MIAKA 10 YA UZALISHAJI WA KAHAWA SPESHELI
Na,Stephano Mango,Songea
KAHAWA ni moja ya mazao muhimu katika kuliingizia taifa pato la kigeni ambapo Tanzania ni moja ya nchi zinazozalisha zao hilo na jitihada mbalimbali zimekuwa zikifanya ili kuboresha zao hilo muhimu kwa uchumi wa taifa letu

Ili kutimiza adhima hiyo Serikali mara nyingi imekuwa ikihamasisha wakulima kujiunga na kuanzisha vikundi au ushirika ili kuongeza uzalishaji na ufanisi zaidi katika kurahisisha wataalam wa kilimo kuwatembelea na kutoa elimu ya kilimo bora

Katika uzalishaji wa kahawa bora wakulima wa kahawa aina ya Spesheri waliamua kuanzisha umoja wao ambao unafahamika kwa jina la Association of Kilimanjaro Specialty Coffe Growers wenye makao makuu mjini Moshi mkoani Kilimanjaro

Umoja huo kwa jina la kibiashara na maarufu unaitwa Kilicafe ikiwa ni alama muhimu ya mlima Kilimanjaro ambao ni fahari ya Tanzania na Afrika kwa ujumla ambapo wakulima hao wa kahawa aina ya Spesheli wakiwa kwenye umoja wao wanatarajia  mwaka huu wa 2011 kutimiza miaka 10 ya uzalishaji wa kahawa hiyo katika kanda ya kanda ya Kaskazini,Mbeya na Mbinga na sherehe ya kutimiza miaka hiyo inatarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi juni mwaka huu

Akizungumza kwenye mkutano wa mwaka wa wanachama wa umoja huo uliofanyika wilayani Mbinga na kuhudhuliwa na viongozi wa Serikali na taasisi mbalimbali mei 17 mwaka huu Mkurugenzi Mtendaji wa umoja huo wa Kilicafe Geoffrey Mwangulumbi alisema kuwa umoja huo ulisajiliwa mwaka 2001

Mwangulumbi alisema kuwa umoja huo ulianza katika mikoa ya Kilimanjaro,Arusha na Manyara kwa ushirikiano wa vikundi kutokana na ushauri wa Shirika la Marekani la TechnoServe ambako umoja huo ulikuwa na vikundi wanachama 10

Alisema kuwa Kilicafe haikukomea mikoa ya Kaskazini bali ilijitanua hadi katika mikoa ya Mbeya na Ruvuma mwaka 2002 ambapo katika kurahisisha utendaji kazi wa umoja huo ulibuni mfumo wa uongozi wa kikanda na kugawanyika katika kanda ya kaskazini yenye mikoa ya Manyara,Kilimanjaro na Arusha,kanda ya Mbinga na kanda yaa Mbeya

Alisema kuwa umoja huu katika kanda ya Mbinga una vikundi vya kibiashara vya wakulima 120 na upo katika tarafa za Mbuji,Mbinga mjini,Mpepo na Namswea kukiwa na jumla ya wakulima zaidi ya 7000

Alisema kuwa malengo makuu ya umoja huo ni kuzalisha kahawa aina ya Spesheri iliyo bora ambayo itapata soko la uhakika katika masoko ya kimataifa,kuboresha maisha ya mkulima kwa kuhamasisha wakulima wanachama kuzalisha kwa wingi na kuandaa kahawa inayokidhi viwango vya soko na kutoa uwiano mzuri kiuchumi

Malengo mengine ni kutafuta masoko mazuri na endelevu kwa ajili ya kahawa inayozalishwa na wanachama ,kutoa mafunzo ya kilimo hususan agronomia na uandaaji bora wa kahawa kwa wananchama na kuwaunganisha kwenye taasisi za fedha ili waweze kupata mikopo ya mitaji ya kununua mashine za kumenyea kahawa na wagavi wa pembejeo

Mkurugenzi huyo wa Kilicafe alisema kuwa umoja huo umepata mafanikio na changamoto kadhaa ambazo zinawakabili kutimiza malengo yao ya kujikomboa kiuchumi ambapo alitaja mafanikio waliyoyapata kuwa ni pamoja na Umoja huo katika kanda hii kudumu kwa miaka tisa sasa, tangu mwaka 2002 ambapo kulikuwa na vikundi 22 tu, sasa vipo vikundi 120 na vikundi 17 vipya vimeomba kujiunga mwaka huu

Alisema kuwa mafanikio mengine ni chama kudumu kwenye shirika la fair-trade ambapo hupata faida ya bei ya wastani wa juu kwa kuwekewa kima cha bei ambapo ikishuka zaidi ya hapo kama ni hasara watafidia ambapo pia kwa kilo ya kahawa inayouzwa hulazimika kimfumo kupata fedha za kuendeleza miradi ya chama na kwamba miradi iliyonufaika na mpango huo ni ujenzi wa ofisi za vikundi na jengo la ofisi ya kanda pamoja na ghala la kuhifadhia kahawa za chama.

Alitaja mafanikio mengine ni makusanyo ya kahawa kuongezeka kutoka tani 420 msimu 2002/03 hadi tani 2,460 kwa msimu uliopita ingawa mwaka uliopita makusanyo yalishuka sana kutokana na hali mbaya ya hewa, ugonjwa wa vidung’ata na ushindani kuwa mkubwa ingawa hatimaye wastani wa mapato ya mkulima wetu ni ya juu kuliko wakulima walio wengi kwani tulikusanya tani 1700 na malipo ni wastani wa Sh 3975 kwa kilo ya kahawa ambapo jumla ya fedha Bilion 6.8 zimeingia wilaya ya Mbinga kwa wakulima wanachama wa Kilicafe

Pia alisema mafanikio mengine kusimika mitambo ya kukobolea kahawa 77 yenye ukubwa kuanzia nusu tani (0.5), tani moja na nusu (1.5) hadi tani mbili na nusu (2.5) kwa saa ambapo mitambo hiyo ya kumenyea kahawa ni za teknolojia ya hali ya juu ukiwa ni uwekezaji vijijini kwa wakulima wenyewe na kwamba mitambo hiyo inanunuliwa na wakulima wenyewe kwa mkopo ambapo umoja unakatwa fedha zake baada ya mauzo ya kahawa.

Alisema kuwa umoja unajivunia mafanikio ya kupata masoko mazuri ya kahawa ambayo hutuwezesha kupata bei nzuri kwa wastani kwani kwa kawaida ni sera ya Kilicafe kurejea nyuma kusawazisha malipo ya awali hii maana yake ni kwamba iwapo bei imeanza kwa TSh 2,000 kwa kilo na kisha kupanda hadi TSh 2,500. Soko huria hawarejei nyuma kuwalipa wakulima waliouza kahawa kwa bei ya TSh 2000 kwa kilo, jambo ambalo ni kinyume na sera yetu ya umoja wa kibiashara ambao hutoa malipo ya awali (bei ya ushindani).

“Sisi ama tunarejea nyuma na kufidia wote ili wawe na malipo sawa ya awali au malipo ya mwisho baada ya kuuza kahawa, hesabu za uwazi huwekwa mezani na kutoa gharama kisha kiasi chote kinachobakia huenda kwa mkulima hivyo, bei ya mwisho hupatikana baada ya mauzo ndipo tunaweza kutofautiana kutegemea ubora wa kahawa na soko ilikouzwa”alisema Mwangulumbi

Alisema kuwa kanda ya Mbinga imejenga ofisi yake hivyo imeondokana na gharama za kupanga kwani ukumbi wa ofisi hutoa huduma kwa wadau wengine kufanyia vikao vyao bila bughudha ni moja ya mafanikio ya miaka 10 ya Kilicafe

Alieleza zaidi mafanikio mengine ni vikundi vingi vya wanachama vimeweza kujenga ofisi zao, kununua mitambo, kujenga visima vya kuoshea kahawa, kujenga meza za kuanikia kahawa, kujenga maghala madogo ya kuhifadhia kahawa ambapo chama kimefanikiwa kujenga ghala la kuhifadhia kahawa katika mji wa Makambako na kupunguza gharama ya uhifadhi wa kahawa kwenye maghala mengine ambapo kwa mujibu wa taratibu za bodi ya kahawa ya Mbinga huuzwa kutokea Makambako.


“Kanda ya Mbinga imeendeleza mfuko wa Pembejeo wa kanda ambao pamoja na mfuko wa akiba wa chama, tumeweza kuwakopesha wakulima mbolea na madawa kila mwaka kiasi cha mifuko ya mbolea zaidi ya 6,000 mbalimbali na kulipa kodi na michango ya wilaya kwani imeweza kulipa kodi ya wilaya zaidi ya milioni 182 na mchango wa vidung’ata sh 19 milioni kama ilivyoamriwa na wilaya ili kupambana na janga la ugonjwa wa vidung’ata unaoteketeza kahawa”alisema Mwangulumbi

Alisema kuwa chama kiliasisi mpango wa umeme jua ili kuwanufaisha wakulima wa vijijini kupata nishati hivyo tumeweza kusimika paneli za umemejua 21 na paneli 103 zitasimikwa Juni 2011 ambapo paneli hizi ni za bei nafuu na kwa mkopo kwa wakulima kwa muda wa miaka mitatu.

Alifafanua kuwa mafanikio mengine ni viongozi na wakulima wa vikundi vichache wamepewa mafunzo ya matumizi ya kompyuta ambazo zinatumika kutunza kumbukumbu za mkulima na kutoa stakabadhi hapo hapo kwa kila mkulima atakayeuza kahawa kwenye vikundi hivyo ambapo vikundi hivyo ni vya Mahenge, Ilela na Kihuka ambazo zitaunganishwa na mtandao wa Mkurugenzi Mtendaji wa chama.

Alisema kuwa ushirikiano kwa wakulima ni kitu muhimu sana hivyo wakulima wa kanda ya Mbinga wameanza kujenga urafiki na wakulima wa ushirika wa wakulima wa kahawa Mzuzu nchini Malawi ambao waliitembelea kanda kubadilishana ujuzi na uzoefu katika kahawa ili kumkomboa mkulima pia kitendo cha Serikali kutambua Kilicafe kuwa ni umoja wa wakulima wenye malengo thabiti ya kuimarisha ushirika kwa uwazi na ukweli ni mafanikio mengine

Mwangulumbi akizungumzia changamoto zinazoukabili umoja huo alisema kuwa ni pamoja na  uwezeshaji katika uwekezaji wa wakulima wadogo kwani ununuzi na usimikaji wa mitambo ni wa gharama kubwa ambapo hali hiyo imefanya vikundi kadhaa kushindwa kununua mitambo haraka kwani mahitaji ya mitambo ni makubwa na yanaongezeka kila mwaka ambapo tulianza na mitambo 4 mpaka msimu huu tuna mitambo 77 hivyo vikundi vipya  43 bado havina mitambo ya kisasa kwani hutumia mitambo midogo ya zamani hata vikundi vyenye mitambo,ujenzi wa miundombinu kama maji, matenki na meza za kuanikia kahawa hutugharimu sana na kwamba ombi letu kwa Serikali vikundi vikiomba visikilizwe na kusaidiwa maombi yao yakiwasilisha kwenye mfuko wa DADPS.

Alisema pia changamoto nyingine ni kuwa ushuru wa Halmashauri licha ya kuwa ni wajibu wetu kuchangia maendeleo lakini wakulima wanaomba angalau kiasi kipunguzwe kiwe asilimia 3 ya bei ya kuuza kahawa na kwamba Serikali iliamua kuwasaidia wakulima kwa kutoa ruzuku kwenye pembejeo bado wakulima wa kahawa hawajanufaika na pembejeo hizo, hivyo tunaomba sera ya pembejeo irekebishwe ili zao la kahawa ambalo ni kinywaji kizuri kwa biashara na chakula lipate kuimarika zaidi.

Baadhi ya wakulima wa zao hilo ambao ni wanachama wa Kilicafe wakizungumza kwenye mkutano huo waliipongeza Serikali ya wilaya ya Mbinga kwa kuamua kusikiliza kilio cha wakulima wa zao hilo kwa kuamua kutoa sehemu ya ushuru wa kahawa kwa ajili ya kununulia miche ya kahawa ambayo mkulima wa zao hilo wilayani humo amekuwa akipewa bure

Menas Msuha mkulima wa kijiji cha Marindindo alisema kuwa kutokana na serikali kutoa miche ya kahawa bure kumemfanya aweze kuzalisha kahawa kwa wingi na kwamba kwa sasa ameshachimba mashimo mengi akisubiri kupanda kahawa nyingine

Naye Edwin Mpolola mkulima wa zao hilo katika kijiji cha Ngima alieleza kuwa Kilicafe imeweza kumsaidia kwa kiasi kikubwa kuboresha maisha yake pamoja na familia kwani hivi karibuni imeweza kumpatia umeme wa jua(Solar Power)ambao umeweza kumsaidi kupunguza gharama za kununua mafuta ya taa ambayo kwa sasa hivi lita moja imekuwa ikiuzwa kwa bei kubwa wilayani Mbinga na kwamba anaweza akapata taarifa mbalimbali kupitia luninga ambayo amefunga nyumbani kwake tofauti na kipindi cha nyuma

Mwandishi wa makala
Anapatikana kwa 0755335051
Baruapepe;stephano12mango@yahoo.com




SERIKALI YATAKIWA KUSHIRIKIANA NA ASASI ZA KIRAIA NCHINI

Wednesday, June 29, 2011

WATENDAJI WAZAWADIWA KWA UTUMISHI ULIOTUKUKA Na Stephano Mango,Songea HALMASHAURI ya Wilaya ya Songea imewatunuku zawadi ya Pikipiki mbili ya utumishi uliotukuka Watendaji wawili wa Kata ya Kilagano na Kata ya Litisha kwa kusimamia vizuri shughuli za maendeleo katika msimu wa bajeti ya mwaka wa 2010/2011 Akizungumza na waandishi wa habari nje ya ukumbi wa mikutano wa Halmashauri hiyo mara baada ya kikao cha Baraza la Madiwani kilichofanyika katika ukumbi wa Maendeleo jana Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Rajabu Mtiula alisema kuwa watendaji hao wamejitahidi kufanya kazi zao kwa kujituma na kwa uaminifu mkubwa Mtiula aliwataja Watendaji hao kuwa ni Notka Tewele wa kata ya Litisha na Skolastika Mkanula wa kata ya Kilagano ambao wameisaidia Halmashauri hiyo katika ukusanyaji wa mapato na usimamizi mzuri wa ujenzi wa miradi ya maendeleo katika maeneo yao Alisema kuwa pikipiki hizo mbili aina ya Sunlg zimegharimu jumla ya milioni 4.6 na kwamba wazitunza na kuboresha utendaji wao wa kazi ili waendelee kuwa na rekodi ya utendaji unaostahili kwa mtumishi wa umma Alisema kuwa Halmashauri inaendelea kuwapa motisha watumishi wake wanaofanya vizuri katika kusukuma guruduma la maendeleo la Wilaya ya Songea na Taifa kiujumla ambapo watumishi hao wamekuwa wakipata zawadi mbalimbali kulingana na eneo lake la kazi Awali Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Anna Mbogo alisema kuwa kwa mwaka wa fedha wa 2010/2011 Halimashauri ilikasimia kukusanya mapato ya jumla ya Shs 10,145,866,000 kutoka kwenye vyanzo vyake vya mapato Mbogo alisema kuwa hadi mei 31,2011 Halmashauri ilikuwa imefanikiwa kukusanya jumla ya Shs 7,776,727,211.84 sawa na asilimia 76.65% ya mapato yote na kwamba ili kuongeza mapato kwa mwaka ujao wa 2011/2012 Halmashauri imejipanga kutekeleza mikakati mbalimbali MWISHO

Thursday, June 16, 2011

TUWAJIBIKE KUZUIA UHARIBIFU WA MAZINGIRA NCHINI-MGOWOLE



TUWAJIBIKE KUZUIA UHARIBIFU WA MAZINGIRA NCHINI-MGOWOLE
 Na;Stephano Mango,Songea

NI wazi kuwa upatikanaji wa nishati ya umeme hapa nchini limekuwa ni tatizo sugu hali inayosababisha Watanzania wachache kutumia nishati hiyo na wengi kutumia mazao ya misitu kwa ajili ya matumizi yao ya kila siku

Kwani kutokana na kukosa nishati ya umeme,wananchi wengi Mijini na Vijijini wanatumia nishati inayotokana na misitu kama vile kuni na mkaa kwa ajili ya matumizi mbalimbali ikiwamo kupikia.

Matumizi ya mazao ya misitu yamesababisha kuwapo na uharibifu wa mazingira kutokana na wananchi wengi kukata miti ovyo bila kupanda mingine.

Akizungumza na gazeti hili Ofisini kwake hivi karibuni Afisa Misitu wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea Robart Mgowole anasema kuwa mazingira ni jumla ya vitu vyote vinavyomzunguka mwanadamu vikiwamo mimea,maji,hewa, miundombinu, ardhi na vingine vingi. Kwa hiyo unapozunguzia mazingira unamgusa binadamu moja kwa moja.

Mgowole alisema kuwa  mazingira ni msingi wa maisha ya binadam na ukuaji wa uchumi wa nchi kwenye maeneo ya rasilimali kama vile misitu,uvuvi,kilimo,wanyamapori,makazi,maji na nishati

Alisema kuwa maisha ya binadamu na viumbe hai wengine hutegemea mazingira na uoto wa asili katika kujiletea maendeleo kwa kutambua hilo, uboreshaji wa mazingira ni jambo la lazima kwa kila mdau wa mazingira

Alieleza kuwa ukataji  wa miti, uchafuzi wa maji na matumizi mabaya ya ardhi ni miongoni mwa uharibifu mkubwa wa mazingira unaofanywa na binadamu katika maisha yake ya kila siku na hivyo huathiri pia viumbe hai na visivyo hai.


“Kutoweka kwa uoto wa asili kama vile miti,nyasi na hata viumbe vinavyoishi majini na ardhini,kutokea kwa ukame na milipuko ya magonjwa  mbalimbali kama vile kipindupindu na uti wa mgongo ni miongoni mwa matokeo ya uharibifu na uchafuzi wa mazingira unaofanywa na binadamu katika shughuli zake.”alisema Mgowole


Alisema kuwa binadamu anapofyeka msitu ajue moja kwa moja kuwa anaharibu vyanzo mbalimbali vya maji na mvua hali ambayo itamfanya binadam mwingine asafiri  masafa marefu kutafuta maji ambapo zao tokeo ni kupata maumivu makali kutokana na umbali mrefu


Alieleza kuwa misitu ikifyekwa  na mahali pakaathirika kutakuwa na madhara makubwa katika eneo husika yakiwemo kukwama kwa shughuli za uzalishaji mali kama vile kilimo na ufugaji ambapo hapa nchi ndiyo uti wa mgongo wa Taifa letu kwa kuwa zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania hutegemea kilimo na ufugaji katika kuendeshea maisha yao .

Afisa huyo alisema uharibifu mwingine wa mazingira unatokana na kilimo cha kuhama hama,ujenzi wa viwanda,matumizi ovyo ya mitambo,utupaji wa taka ovyo na kufanya biashara ya mazao ya misitu bila kufuata sheria,kanuni na taratibu zilizopo.

Kutokana na hali hiyo inakadiriwa tangu kipindi cha mwaka juzi hapa nchini eneo la misitu linapungua kwa kasi ya hekta 91,000 kutokana na shughuli mbalimbali za binadamu sizizo zingatia utunzaji wa mazingira
 Alisema hali hiyo inachangiwa kwa kiasi kikubwa katika uharibifu wa mazingira kwani athari za tabia ya nchi imedhihirika ndiyo maana Serikali inachukua hatua mbalimbali za kuhifadhi mazingira lakini bado wadau hawajapokea wito huo wa kuhifadhi mazingira kikamilifu.


Mgowole alisema kuwa moja ya hatua muhimu ambazo Serikali na wadau wa mazingira wanazichukua kupitia Wizara ya Nishati na madini ni uhamasishaji wa matumizi ya umeme nuru hasa kwa wananchi wa vijijini ambao hawajapata umeme wa gridi ya Taifa ambapo kinachoendelea hivi sasa kuhusiana na nishati hiyo ni ukuzaji na uendelezaji wa soko la umeme nuru katika maeneo mbalimbali kwa kuhamasisha wananchi.
  
“Hivi sasa wananchi wengi hasa katika maeneo ya vijijini hawana huduma ya umeme kutokana na sababu mbalimbali ikiwamo hali ya kijiografia ya vijiji vingi kutofikika kwa urahisi hali inayosababisha Wizara kushindwa kufikisha huduma ya nishati ya umeme ambayo ni muhimu kwa maendeleo ya  wananchi “ anasema.
  
Alisema kuwa kutokana na miundombinu hafifu katika vijiji hivyo Wizara ya Nishati na madini kwa kushirikiana na shirika la Maendeleo la Sweden (SIDA) wameanzisha mpango wa kuhamasisha matumizi ya umeme nuru ambao utasaidia wananchi katika matumizi mbalimbali.
  
Ameyataja matumizi hayo kuwa ni pamoja na ya nyumbani, shuleni, katika vituo vya kutolea huduma za afya ,kwenye taasisi mbalimbali pamoja na matumizi mengine ambapo hadi sasa mradi wa umeme jua umeanza kutekelezwa katika mikoa ya Tanga,Mbeya,Iringa Mtwara, Rukwa, Dodoma,Pwani na Morogoro na kwamba mradi huo wa umeme nuru katika Mkoa wa Ruvuma uliingia Desemba mwaka juzi
  
Alieleza zaidi kuwa takwimu za Kitaifa zinaonyesha kuwa ni asilimia mbili tu ya watu kati ya asilimia 89 ya Watanzania wanaoishi vijijini ndio wanaotumia nishati ya umeme na  asilimia 87 wanaendelea kutumia nishati inayotokana na misitu hivyo kuchangia kwa kiasi kikubwa uharibifu wa mazingira kila mwaka.
  
Jambo la msingi hivi sasa ni kutoa elimu ya utunzaji wa mazingira pamoja na matumizi ya umeme nuru pamoja na gharama nafuu za vifaa vya nishati hiyo ili kuwawezesha wananchi wengi kupata huduma hiyo ili hatimaye wananchi wajikomboe kutokana na matumizi makubwa ya nishati inayotokana na mazao ya misitu.
  
Ni wazi kuwa makamu wa Rais Dk.Mohamed Ghalib Bilal mara kwa mara amekuwa akisisitiza wakulima wa tumbaku,chai na watumiaji wengine wakubwa wa miti,kuni na makaa ya mawe waanzishe mashamba  yao ya miti na ameagiza kila Kijiji kiwe na shamba au mashamba mahsusi ya miti kwa matumizi ya nishati ya kuni,mkaa na biashara ya mbao.
  
Mgowole alisema pia inashauriwa kila kijiji kiandae vitalu vya miche ya miti ifaayo na kupanda miti kila ifikapo Januari mosi na April ya kila mwaka na kuendelea kuitunza ambapo kila mji utenge maeneo ya mashamba ya miti kwa ajili ya nishati, biashara na kuendeleza mandhari ya Mji husika.
  
“Kutokana na madhara yanayoendelea kutokea ya mabadiliko ya tabia ya nchi sisi kama Taifa hatuna budi sasa kuyalinda na kuyahifadhi mazingira yetu kwa nguvu zetu zote ikiwa ni pamoja  na kuacha kabisa tabia sugu ya uchomaji moto na ufyekaji wa misitu ambao huchangia uharibifu wa vyanzo vya maji na mazingira”alisema Mgowole.
  
Anasisitiza kuwa matukio ya uchomaji moto wa misitu na nyika ni marufuku,wahalifu wachukuliwe hatua kali za kisheria na uongozi wa eneo husika uwajibike kikamilifu katika kusimamia hilo na wananchi wahamasishwe kushiriki katika kampeni ya kudumu ya kupanda na kuitunza miti wanayoipanda kila mwaka na kwamba Manispaa ya Songea imetekeleza agizo la Serikali la kupanda miti milioni  1.5 kila mwaka.

Alisema kuwa Halmasshauri ya Manispaa ya Songea imevuka lengo hilo na kufanikiwa kupanda miti milioni 1.7 kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa mazingira na kwamba kuna maeneo ambayo yanapandwa miti na wadau mbalimbali wakati wa mvua na kwamba kuna vikundi vya utunzaji wa mazingira navyo vina maeneo yao wanayopanda miti na kuitunza

Alieleza zaidi kuwa Halmashauri hiyo imekuwa ikizalisha miche ya miti kwenye vitalu vya watu binafsi na kuwagawia wananchi kwa bei nafuu kwenda kuipanda na wakati mwingine hupewa bure kwa ajili ya kuipanda kwenye maeneo yao
  
Alisema kuwa ni vema kampeni ya mazingira ya umma ianzishwe kwa vitendo kwa kushirikisha Serikali za Mitaa na taasisi mbalimbali na kwamba ifanyike jitihada za kudhibiti uvunaji holela wa mazao ya misitu katika maeneo yote nchini,mazao hayo ya misitu ni pamoja na magogo,nguzo,mbao,kuni na mkaa.
  
Alifafanua kuwa mahitaji ya mazao hayo ni makubwa na uvunaji wa mazao hayo nao ni mkubwa. kutokana na hali hiyo ndio maana Wizara ya Maliasili na utalii imependekeza katika kuboresha usimamizi wa uvunaji wa mazao ya misitu.
  
Ambapo katika utaratibu huo mpya kwa mujibu wa Wizara ya maliasili na Utalii aina za miti zipatazo 24 hazitaruhusiwa kuvunwa ikiwamo miti ya matunda kama vile mibuni,mizambarau na mingineyo ambapo maofisa wa misitu katika kila Wilaya wanatakiwa wawe makini katika kuhakikisha utaratibu huu wa kuvunwa misitu unafuatwa.
  
Wasafirishaji wa mazao ya misitu nao wanatakiwa kuhakikisha wanafuata taratibu zilizowekwa na Wizara ya Maliasili na Utalii zikiwamo za hati za usajili wabiashara ya mazao ya misitu, kibali cha usafirishaji, leseni ya biashara na hati za malipo ya mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) ili Taifa liwe na uhakika wa upatikanaji wa mapato wa mazao ya misitu.
  
Katika utaratibu huo wa usimamizi wa uvunaji wa mazao ya misitu kila Wilaya inahusika zaidi na vibali vya kuvuna ambavyo vinatolewa na kamati maalumu ya Wilaya ya usimamizi wa uvunaji wa misitu ambayo inaongozwa na mkuu wa Wilaya husika na kwamba katika vijiji ambako mazao ya misitu yatavunwa vinahusika na udhibiti wa uvunaji na ofisa misitu wa Wilaya husika anatoa leseni baada ya kibali cha kamati.
  
“Kila Wilaya hapa Nchini kulingana na utaratibu huo mpya inatakiwa itenge maeneo ya misitu ya kutengenezea mkaa na kila mwaka na wananchi wayatambue maeneo hayo na shughuli za uchomaji mkaa zisifanywe katika maeneo tofauti na hayo yaliotengwa na kutangazwa na vijiji husika.”alisema Mgowole
  
Alisema kuwa katika utaratibu huo wa usimamizi wa mazao ya misitu kila atakayechoma mkaa anapaswa kuwa na leseni maalumu ya kuchoma mkaa itakayotolewa na Ofisa misitu kwa niaba ya Wizara na kwamba leseni hiyo itatumika katika eneo lililoruhusiwa kwa shughuli hizo.
  
“Watengenezaji hao wa mkaa wataonyeshwa katika kijiji eneo la wazi lenye ukubwa mara mbili ya eneo walilopatiwa kuvuna na kutengeneza mkaa na watatakiwa kupanda miti na kuitunza katika eneo hilo wakati wa msimu wa mvua utakaofuatia na kwamba maeneo hayo yatabakia kuwa mali ya Kijiji chini ya usimamizi wa serikali ya kijiji.’alisema Mgowole
  
Alisema ukataji miti katika misitu ya hifadhi kwa ajili ya kutengenezea mkaa umepigwa marufuku  kwa kuwa miti inayohifadhiwa kisheria hairuhusiwi kutengenezea mkaa na kwamba miti hiyo ni pamoja na msandali,mpingo,mvule, mninga, mpodo, mkora, mkora, muhuhu,mfimbo, mkangazi, mwangati, msekeseke na pangapanga na miti yote ya matunda ya porini ikiwamo mikwaju, mmitonga, mikusu, mitalali, mizambarau, mibula., mingwera, mipingipingi na mifuno.
  
Jamii itambue kuwa Tanzania ina eneo la misitu lipatalo hekta milioni 33.3 za misitu   ambayo inapaswa kulindwa na kutunzwa kwa ajili ya ustawi wa Taifa.
   
  Mwandishi anapatika kwa
  Simu 0755-335051 au 0715 335051
  Barua pepe;stephano12mango@yahoo.com