About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Tuesday, July 10, 2012

MADAKTARI; KUNA KIKOSI CHA KUMUUA ULIMBOKA


• Wasema Ulimboka alimtambua afisa aliyemteka

Na Irene Mark


BAADA ya kutekwa, kupigwa na kutelekezwa kwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari nchini, Dk. Steven Ulimboka, viongozi wa vyama vya madaktari wamedai maisha yao yako hatari hali iliyowalazimu kuomba ulinzi Umoja wa Mataifa na makundi mbalimbali ya kutetea haki za binadamu.
Madaktari hao wamesema hawana imani na maofisa wa serikali ya Rais Jakaya Kikwete, wanaotishia usalama wa maisha yao kwa namna tofauti hasa baada ya tukio la Dk. Ulimboka la Juni 27 mwaka huu.
Barua ya madaktari hao kwenda kwa Mwakilishi Mkazi wa Umoja wa Mataifa hapa nchini ya Julai 7, 2012, madaktari wameeleza namna maofisa wa serikali wanavyotishia usalama wa maisha yao hao na kuwaeleza namna walivyowatuma wenzao Afrika Kusini kuhakikisha Dk. Ulimboka anapoteza maisha.
Pia barua hiyo yenye kumb. Na.MAT/UN/SU/01, imetumwa kwa Mwenyekiti wa Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), Dk. Namala Mkopi, Shirika la Human Rights Watch na Amnesty International.
Taasisi nyingine zilizopelekewa nakala ya barua hiyo ambayo Tanzania Daima ina nakala yake ni Kituo cha Haki za Binaadam (LHRC), SIKIKA Tanzania, Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (TAMWA).
“Hata hivyo, watu kutoka serikalini waliihakikishia MAT kwamba timu ya wasaidizi wao imeenda Afrika Kusini kuhakikisha Dk. Ulimboka anarudi nyumbani akiwa maiti.
“Kwa kuongezea hapo, viongozi wa MAT tunapokea vitisho kwa njia ya ujumbe mfupi wa maandishi kwenye simu na wakati mwingine tunapigiwa simu na namba zisizopatikana tukitishiwa maisha,” ilieleza sehemu ya barua hiyo iliyosainiwa na Dk. Mkopi.
Aidha, barua hiyo imeuomba Umoja wa Mataifa kuwahakikishia madaktari usalama wa Dk. Ulimboka kwenye hospitali anayotibiwa na kuwalinda madaktari wengine hasa viongozi wa vyama na jumuiya ya madaktari.
Kadhalika barua hiyo imeuomba umoja huo kuushauri mfumo wa sheria za Tanzania kutokubali kutumika kwa faida za kisiasa na kulitaka Bunge kubaki na majukumu yake ya Kikatiba ya kuiwajibisha serikali kwa vifo vya watu kama matokeo ya mgomo unaoendelea.
Katika barua hiyo madaktari hao wameeleza namna Dk. Ulimboka alivyoteswa na watekaji hao kwa kung’olewa kucha, meno na kuumizwa sehemu mbalimbali za mwili wake huku akimtambua ACP Msangi kuwa miongoni mwa watekaji hao.
Walieleza namna polisi wa kituo cha Bunju walivyoshindwa kuwapa ushirikiano kwa haraka ili kumuwahisha majeruhi huyo kwenye Hospitali ya Taifa Muhimbili na jinsi walivyokuwa wakizuiwa na magari ya askari kwa lengo la kumchelewesha asipate huduma za kitabibu.
“Akiwa kwenye chumba cha wagonjwa mahututi Kitengo cha Mifupa Muhimbili (MOI), Dk. Ulimboka licha ya maumivu makali aliyokuwa nayo alimtambua ACP Msangi kuwa ni miongoni mwa waliomteka na kumtesa,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo na kubainisha kwamba ACP Msangi ni kiongozi wa tume iliyoundwa kuchunguza suala hilo.
Ikulu yasononesha viongozi wa dini
Baadhi ya viongozi wa dini waliojitolea kusuluhisha mgogoro baina ya madaktari na serikali, wameeleza kusononeshwa na jibu la Ikulu la kukataa kuonana nao huku wakibainisha kwamba jukumu lao kubwa ni kuhakikisha amani inatawala.
Akizungumza kwa niaba ya viongozi hao, Msemaji wa Kamati ya Vijana wa Baraza Kuu la Waislamu (Bakwata), Said Mwaipopo, alisema licha ya jibu hilo wanaendeleza juhudi za kuhakikisha mgogoro huo unamalizika kwa njia za amani.
“Hatukatishwi tamaa na jibu la Ikulu kazi yetu kubwa ni kuhakikisha amani inakuwepo… ndiyo maana jana tulikutana na viongozi wa madaktari tukawaeleza kwamba njia bora ya kufanya ni kuandika barua na kuieleza jamii kupitia vyombo vya habari kwamba wanaomba msamaha kwa Rais, wananchi na serikali.
“Kitu kinachotusikitisha vijana wale walikataa ushauri wetu tukagundua kwamba inawezekana nyuma yao kuna siasa zinaingia,” alisema Mwaipopo.
Akijibu suala hilo Katibu wa Jumuiya ya Madaktari, Dk. Edwin Chitage, alikiri kukutana na viongozi hao jana na kueleza kwamba walichokubaliana ni kusubiri barua rasmi kutoka Ikulu ikiwataka madaktari hao kuandika barua kuomba msamaha kwa Rais, Watanzania na serikali.
“Ni kweli lakini alichokisema Mwaipopo ni kwamba alipigiwa simu na watu waliodai kwamba wako Ikulu, hivyo wakawaambia viongozi hao wa dini watuambie madaktari tuandike barua ya kuomba msamaha.Tunaomba msamaha kwa nini,” alihoji.
Dk. Mkopi aliongeza kuwa madai yao hayajatekelezwa licha ya kuwepo kwa muda mrefu tangu mwaka 2005 na kwamba kama serikali haina dhamira ya kweli ya kumaliza mgogoro huo utaendelea hata baada ya miaka 10.
Kukutana na Dk. Mwinyi
Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari Dk. Godbless Chale alisema walipokea simu kutoka kwa Waziri mpya ya Afya na Ustawi wa Jamii Dk. Hussein Mwinyi ikiwataka kwenda kumweleza sababu za mgomo wao.
“Kweli Dk. Mwinyi alitupigia simu akatuita alisema hajui madai yetu hivyo twende tukamweleze hivi kwa akili ya kawaida kweli ofisi inakosa nyaraka za kumbukumbu?!! Tunaona hayupo ‘serious’.
“Kabla hajatuita wizara yake iliteua wajumbe watatu Naibu Katibu Mkuu, Naibu Mganga Mkuu Dk. Donald Mbando na Mkurugenzi wa Rasilimali tukaketi nao kuwaeleza siku chache baadaye waziri anasema hajui madai yetu hii tumeona ni ‘kamchezo’ wanataka kutufanyia,” alisema Dk. Godbless.