About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Saturday, June 23, 2012

WANAWAKE WATAKIWA KUJIUNGA NA CHADEMA KWA UKOMBOZI


Na Stephano Mango, Songea
WANAWAKE nchini wametakiwa kuzisikiliza sera za Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema na kujiunga na chama hicho chenye malengo ya kuleta ukombozi kutoka mikononi mwa Chama cha Mapinduzi ambacho kimewanyonya watanzania kwa muda mrefu na kuwafanya maskini
Wito huo umetolewa jana na Katibu wa wanawake wa Chadema Jimbo la Songea Asia Ngonyani akiwahutubia mamia ya wananchi baada ya kufungua Tawi la Chadema na Ofisi ya Chama hicho mtaa wa Kuchile kata ya Seedfarm Halmashauri ya Manispaa ya Songea  kwenye ziara  yenye lengo la kuimarisha chama katika kata za pembezoni mwa mji
Ngonyani alisema kuwa Chama cha Mapinduzi kimekuwa kikiwatumia wanawake kwenye chaguzi mbalimbali na kuwavesha vilemba na vitenge ambavyo hata ukivaa vinaangaza na baada ya kumaliza uchaguzi na kuunda Serikali ambayo imekuwa ikikosa mipango na vipaumbele vya kuwakomboa wanawake kiuchumi na kijamii
Alieleza kuwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi imekuwa ikiwanyanyasa na kuwadhalilisha sana wanawake wanapokuwa kwenye biashara zao ndogondogo kwa kuwakamata na kuwanyang’anya vitu vyao kwa kutumia mgambo wa mji hali ambayo inaendelea kuwaondolea utu katika jamii
Alisema kuwa kwa muda mrefu Serikali imekuwa ikiwadanganya wakina mama kuwa huduma za kujifungua ni bure na matibabu ya mtoto wa chini ya miaka mitano ni bure wakati wakina mama wanalipia huduma hizo kwa fedha nyingi
Alifafanua kuwa licha ya wakina mama kulala wanne wanne kwenye kitanda kimoja na wengine kulala chini , basi ukitaka kufa au kupoteza mtoto katika vituo vya afya au Hospital za Serikali usiwe na fedha au umwambie muuguzi kuwa natakiwa kupata huduma za matibabu bure
Naye Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Ruvuma na Diwani wa Kata ya Mjini Joseph Fuime  akiwahutubia wananchi hao alisema kuwa Serikali imeshindwa kuwaheshimu watanzania kutokana na matendo yao katili dhidi ya wananchi kutokana na kuwapandishia gharama za maisha kila kukicha,kushindwa kutekeleza ahadi ya maisha bora kwa kila mtanzania,kuwatoza kodi nyingi huku wakishindwa kutoa huduma stahiki kulingana na kodi zinazotozwa kwa wananchi
“Ili kufanya mabadiliko katika nchi hii ni lazima wananchi waamue kuchukua hatua za kuzisikiliza sera za Chadema na kujiunga nacho ili kuweza kuleta ukombozi stahiki mara uchaguzi wa Serikali za Vijiji,Mitaa na katika uchaguzi mkuu wa Madiwani,Wabunge na Urais”alisema Fuime
Alisema kuwa leo tumefungua Ofisi ambayo imegharamiwa na baadhi ya wanachama wa Chadema katika kata yenu hivyo tumewaletea chama chenye uhai na matumaini kwa watanzania na ambacho kina dhamira ya kweli ya kuwakomboa watanzania
Alieleza kuwa hakuna anayelazimishwa kukipokea na kujiunga nacho hivyo kama mnataka kuendelea kukandamizwa na Serikali ya Ccm miaka 50 ijayo ya uhuru,mnahiyali ya kukipokea au kukikataa kwa faida yenu na vizazi vijavyo
MWISHO

WASAFIRISHAJI RUVUMA WAIDAI SERIKALI ZAIDI YA MILIONI 375

Na Stephano Mango, Songea
WASAFIRISHAJI wa Mizigo mkoani Ruvuma wameitaka Serikali kupitia  Wizara ya Kilimo,Chakula na Ushirika kuona umuhimu wa kuwalipa deni la fedha zaidi ya milioni 375 wanazozidai kwenye kitengo cha Taifa cha kuhifadhi mahindi kilichopo mkoani Ruvuma (SGR) baada ya kufanya kazi ya kubebelea mahindi kutoka vijijini na kuyaleta kwenye hifadhi hiyo mwaka 2011
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wasafirishaji hao ambao wameomba majina yao yahifadhiwe walisema kuwa walikopwa kuyabebelea mahindi hayo kwa ahadi kuwa fedha zao wangelipwa mara baada ya kumaliza kubebelea na kuyaleta kwenye hifadhi lakini cha ajabu toka wamemaliza kuyaleta mahindi hayo ambayo tayari yameuzwa na Serikali hawajalipwa hali ambayo inaendelea kuwakatisha tamaa
Walisema kuwa wafanyabiashara wengine waliikodisha Serikali Magodauni ili wahifadhi mahindi hayo kwa sababu Magodauni ya kituo cha Hifadhi kilichopo mjini hapa hayakuwa na uwezo wa kuhifadhi mahindi yaliyokuwa yanabebelewa na wasafirishaji kutokana na uwingi wake, pia wapo wafanyabiashara ambao walikopwa mafuta lakini wote hawajalipwa
Walisema kuwa Wasafirishaji hao walijitahidi kwa uaminifu mkubwa kuyabebelea mahindi hayo kutoka kwenye maeneo ambayo miondombinu yake ni mibovu sana huku mafuta na vipuri vya magari vikipanda kila mara hivyo tumepata tabu sana na sasa biashara zetu zinayumba tunaiomba Serikali itulipe fedha zetu
Walieleza kuwa wafanyabiashara hao wana mikopo ya biashara Benki na wanalipa kodi mbalimbali zikiwemo za Mamlaka ya Mapato (TRA) na wanachangia michango mbalimbali ya maendeleo mkoani hapa lakini wanashangazwa na kitendo cha Serikali cha kutowathamini wasafirishaji hao kwa kuwacheleweshea fedha zao hali ambayo inasababisha kupungua kwa mzunguko wa fedha mkoani Ruvuma na kupungua kwa kasi ya ulipaji wa kodi kutokana na madeni wanayodaiwa
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana Mwenyekiti wa Chemba ya Wafanyabiashara, wenye Viwanda na Kilimo (TCCIA) mkoani Ruvuma Mays Mkwembe alisema kuwa wafanyabiashara wengi ambao waliikopesha Serikali ili kuweza kufanikisha uletaji wa mahindi mjini wamekuwa wakihangaika sana katika shughuli zao kutokana na fedha nyingi kuidai Serikali
Mkwembe alisema kuwa ni vema Serikali ikawalipa wafanyabiashara haraka ili waweze kulipa kodi ambazo wanadaiwa katika msimu wa fedha wa 2011/2012 kwani bila kufanya hivyo hali ya mapato ya mkoa yatakuwa ni madogo sana kuliko ilivyopanga, ingawa pia wafanyabiashara wengi wanadaiwa riba kwenye taasisi za fedha kutokana na mikopo waliyoikopa
Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma Hassan Bendeyeko alikiri kuwa wafanyabiashara wanaidai Serikali kutokana na huduma waliyoitoa hivyo wasubiri kidogo kwani Serikali inaandaa utaratibu wa kuwalipa haki zao kama ambavyo makubaliano yalivyo kwani Serikali inatambua mchango wao katika harakati za kimaendeleo mkoani hapa na taifa kwa ujumla.
MWISHO