About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Monday, October 10, 2011

MADIWANI WAMFYATUKIA DKT NCHIMBI SAKATA LA UMEYA SONGEA

Na Mwandishi Wetu,Songea
MADIWANI 14 wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma waliopiga kura za hapana dhidi ya 12 za ndiyo za kumkataa Charles Mhagama kuwa Mstahiki Meya wa Manispaa hiyo wametoa tamko la kusisitiza kutomtambua Meya huyo na kueleza masikitiko makubwa ya hujuma iliyofanya katika uchaguzi uliofanyika hivi karibuni
Wakitoa tamko lao jana mbele ya waandishi wa habari kwenye Viwanja vya Makumbusho ya Taifa ya Majimaji mjini hapa walisema kuwa wamesikitishwa sana na kulaani vikali hujuma iliyofanywa na Mbunge wa Jimbo la Songea Mjini Dkt Emmanuel Nchimbi kwenye uchaguzi huo ambao ulifanyika kwenye ukumbi wa Saccos ya Manispaa hiyo Septemba 23 mwaka huu
Katika tamko hilo lililosomwa kwa niaba ya Madiwani hao Diwani wa Kata ya Mjini Joseph Fuime lilisema kuwa miongoni mwa hujuma hizo ambazo alizifanya Dkt Nchimbi ni pamoja na kuchukua sanduku la kura ,kukimbia nalo kabla hajadhibitiwa na kumpa nafasi Naibu Meya wa Manispaa hiyo Mariam Dizumba kuziiba na kukimbia nazo nje ya ukumbi na kutokomea nazo  kusikojulikana
Tamko hilo lilisema hujuma nyingine kuwa ni kumwamuru Naibu Meya ambaye si msimamizi wa uchaguzi amtangaze Charles Mhagama ambaye alipata kura za hapana 14 na za ndiyo 12,kumtumia msaidizi wake kuwatisha baadhi ya Madiwani na kutaka kuwatoa nje ya ukumbi huku akijua kuwa msaidizi huyo sio Askari wa Baraza la Madiwani na kutoa lugha ya ufedhuri kwa baadhi ya madiwani wa Manispaa hiyo
Katika tamko hilo pia lilieleza kuwa mnamo Septemba 25 mwaka huu Dkt Nchimbi alitoa taarifa ya uongo kwa vyombo vya habari na kudai aombwe radhi huku akijua anatumia madaraka yake vibaya kuvitisha vyombo vya habari abapo alivituhumu baadhi ya vyombo vya habari kuwa Septemba 23 mwaka huu vilitoa habari inayofanana wakati tarehe hiyo ilikuwa ni mkutano wa Baraza la Madiwani na hakuna chombo kilichoripoti habari hiyo
Tamko hilo lilifafanua kuwa tarehe hiyo kulikuwa na kikao cha Baraza la Madiwani ambacho kilianza saa nne na nusu asubuhi kikiwa na ajenda nne za kufungua mkutano,Uchaguzi wa Mstahiki Meya,Taarifa ya kupitisha kwa mpango na michoro ya Kampuni ya  Ardhi Plan kwa mitaa ya Mitendewawa,Namanyigu na Mshangano katika Kata ya Mshangano na ya mwisho ilikuwa ni kufunga mkutano
Lilieleza zaidi tamko hilo Sasa Mh.huyu anashangaza kwani tulipofika ajenda ya pili tu kabla haijaisha kwa msimamizi wa uchaguzi ambaye ni Mkurugenzi kutangaza matokeo yeye aliingilia kati na kumuamuru Naibu Meya Mariam Dizumba atangaze matokeo na kwa kufanya hivyo vurugu kubwa ilitokea na kikao kusambaratika,sasa yeye anaudanganya umma kuwa kikao kilifungwa majira ya saa 6 mchana
“Sisi Madiwani hatuoni kuwa kuna sehemu huyu Mh.Nchimbi kaonewa,tunavipongeza vyombo vya habari vyote vilivyoripoti kuwa amekimbia na sanduku la kura kwani vilizingatia ukweli wa tukio hilo na tunaamini kuwa vilimtendea haki na kwamba hadi sasa hakuna Meya wa Manispaa ya Songea kwani hakuchaguliwa”lilisema tamko hilo
Akizungumza katika mkutano huo na waandishi wa habari Diwani wa Kata ya Bombambili Kenneth Mbangala alisema kuwa katika uchaguzi wa kumpata Meya taratibu zilivunjwa kwa makusudi ili kumpa nafasi Charles Mhagama kuwa Meya kwani msimamizi wa uchaguzi Jimbo la Songea Mjini ni Mkurugenzi wa Manispaa  Nachoa Zakaria ambaye siku alikuwepo na ndiye aliyepaswa kutangaza matokeo hayo kwani Naibu Meya alikuwa ni mpigakura kama walivyokuwa kuwa madiwani wengine hivyo hakupaswa kutangaza matokeo hayo
Mbangala alisema kuwa licha ya madiwani kumkataa Charles Mhagama ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Matogoro kwa kumpigia kura za hapana 14 na za ndiyo 12 tangazo hilo halikuwa sahihi kwani aliyetangaza ni mtu batili na kufanya uchaguzi huo kuvurugika
Kwa upande wake Mbunge wa Songea Mjini Dkt Emmanuel Nchimbi ambaye pia ni Waziri wa Habari,Utamaduni na Michezo alipoulizwa kwa njia ya simu yake ya kiganjani  kuhusiana na madai ya kuhujumu uchaguzi huo alisema kuwa hahusiki na hujuma hizo ikiwemo ya kukimbia na sanduku la kura
Dkt Nchimbi alisema kuwa sio vyema kwa kiongozi kama yeye kumsingizia mambo kwani kunaweza kumsababisha kushuka kwa morali ya utendaji kazi wake katika utumishi wa umma na kuwataka madiwani hao kuwatumikia wananchi wao badala ya kuzungumzia sakata la uchaguzi wa Meya
MWISHO