About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Friday, October 28, 2011

MHANDISI STELLA MANYANYA AKAMILISHA ZIARA WILAYA YA TUNDURU NA SONGEA VIJIJINI KWA CHEREKOCHEREKO

 Mhandisi Stella Manyanya(Mb) na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa akisaini kitabu cha wageni cha chama na Serikali Wilayani Tunduru alipowasili Wilayani humo kwa ziara ya siku moja



 Mhandisi Stella Manyanya(Mb) na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa akisaini kitabu cha wageni cha Chama cha CCM  Wilaya ya Songea Vijijini alipotembelea ofisi ya chama hicho kabla ya kuanza ziara ya siku moja wilayani humo
 Viongozi wa CCM Wilaya ya Songea Vijijini wakiwa kwenye picha ya pamoja na Mhandisi Stella Manyanya(Mb) na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa

 Wananchi wa kata ya Mtyangimbole ndivyo walivyokuwa wanampokea Mhandisi Stella Manyanya(Mb) na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa alipofanya ziara leo Songea Vijijini




Viongozi wa CCM Wilaya ya Songea Vijijini wakiagana na Mhandisi Stella Manyanya(Mb) na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa katika ofisi za BetterLife Tanzania tawi la Ruvuma

SHAMLA SHAMLA YA MAPOKEZI YA WILAYA YA NAMTUMBO ILIVYOKUWA KUWA WAKATI WA ZIARA YA MBUNGE MHANDISI STELLA MANYANYA NA MKUU WA MKOA WA RUKWA

 Mhandisi Stella Manyanya(Mb) Mkuu wa Mkoa wa Rukwa akicheza ngoma baada ya kupokelewa Kata ya Kitanda Wilayani Namtumbo
 Uwt Wilaya ya Namtumbo wakitoa Zawadi kwa Mgeni rasmi Mhandisi Stella Manyanya(Mb)Mkuu wa Mkoa wa Rukwa alipomaliza kuhutubia wananchi wa kata ya Kitanda
 Mhandisi Stella Manyanya (Mb) Mkuu wa Mkoa wa Rukwa akitoa msaada wa shilingi laki mbili na themaanini kwa vikundi vya ujasiliamali kata ya Kitanda
Diwani wa Kata ya Kitanda Vitus Ngoma akipokea jezi kwa ajili ya timu ya Kata kutoka kwa Mhandisi Stella Manyanya(Mb) Mkuu wa Mkoa wa Rukwa

AUAWA BAADA YA KUVAMIWA NA WATU WANAOHISIWA KUWA NI MAJAMBAZI LUPAPILA

Na Gideon Mwakanosya, Songea
NESTORY  Ndomba (20) Mkazi wa Mtaa wa Lupapila katika Manispaa ya Halmashauri ya Songea Mkoa wa Ruvuma amevamiwa na kundi la watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi na kumsababishia kifo papo hapo baada ya kumpiga na kitu kizito kichwani wakati akiwa anaendesha pikipiki akitokea Lizaboni kwenda Lupapila.
Akizungumza na mtandao wa www.stephanomango.blogspot.com jana ofisini kwake Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma Naftari Mantamba amesema kuwa tukio hilo limetokea octoba 27 mwa huu majira ya saa 2.30 usiku huko katika eneo la Mtaa wa Londoni uliopo jirani na Lizaboni.
Mantamba amebainisha zaidi kuwa Ndomba anadaiwa kuwa aliuwawa na kundi la watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi ambao wote walijifunga vitambaa vyeusi usoni huku wakiwa wameshika nondo mikononi.
Amesema kuwa majambazi hao baada ya kumkamata walianza kumpiga na kitu kizito kichwani huku wengine wakiendelea kumpekua mifukoni na baadaye walimfunga mikono yote miwili kwa nyuma kiunoni kwa kutumia kamba ya katani ndipo walipomlaza chini na kumnyang’anya pikipiki aina ya sunlug ambayo alikuwa akiiendesha akitokea Lizaboni kwenda Lupapila.
Ameeleza zaidi kuwa Ndomba baada ya kufungwa kamba hiyo majambazi hao walitokomea kusikojulikana na pikipiki hiyo yenye namba za usajili T 846 AYS ambayo thamani yake ni shilingi milioni 1.8 .
Hata hivyo Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma Mantamba amesema kuwa mpaka sasa majambazi hayo hayajakamatwa na jeshi la Polisi Mkoani humo linaendelea kuyasaka ili yafikishwe mikononi mwa vyombo vya dola.
Wakati huo huo mtu mmoja aliyetambuliwa kwa jina la Thadei Luambano (45) Mkazi wa Mtaa wa Madizini Kata ya Lizaboni katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea amefariki dunia baada ya kukosa hewa wakati akichimba kisima cha maji huko katika eneo la Jeshi Kambi ya Chabruma mjini Songea.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma Naftari Mantamba amethibitisha kutokea kwa tukio hilo ambalo amedai kuwa lilitokea octoba 27 mwaka huu majira ya saa 10 jioni huko katika kambi ya JWTZ Chabruma ambako Afisa mteule namba 1 wa jeshi la wananchi Tanzania (JWTZ) Augustino Rashid ndiye aliyetoa taarifa ya tukio hilo katika kituo kikuu cha Polisi cha Songea na Polisi bado inaendelea na uchunguzi juu ya  tukio hilo

Thursday, October 27, 2011

WANANCHI WAENDELEA KUMPOKEA KWA SHANGWE MBUNGE STELLA MANYANYA NA MKUU WA MKOA WA RUKWA KATIKA ZIARA YAKE YA KIKAZI MKOANI RUVUMA

Mbunge Mhandisi Sella Manyanya wa kwanza kulia akipiga ngoma ya Beta baada ya kufurahia mapokezi mazuri katika ziara yake,wa kwanza kushoto ni Katibu wa Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Frank Maten akishuhudia mapokezi hayo

Mhandisi Stella Manyanya ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Rukwa na Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Ruvuma akimpatia Katibu wa UWT Wilaya ya Songea Mjini shillingi laki mbili kwa ajili ya mahitaji madogo madogo ya ofisi ya UWT Wilaya ya Songea Mjini,baada ya kupokea ripoti ya utekelezaji kwa kipindi cha mwaka 2011, katikati ni Katibu wa UWT Mkoa wa Ruvuma Mariam Yusuph

Viongozi wa Chama na Serikali wakifanya maombi kwenye kabuli la Nduna Songea Mbano

Mjukuu wa Nduna Songea Mbano,Aidan Mbano akizungumza na Wazee Mashujaa 66 waliozikwa kwenye kabuli la pamoja ikiwa ni dua maalum kwa Mbunge na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Ushauri wa Makumbusho ya Taifa ya Majimaji Songea Mhandisi Stella Manyanya alipotembelea Makumbusho hayo ili kupata baraka za Wazee hao ikiwa ni desturi yake kabla ya kuanza ziara zake mkoani Ruvuma

Viongozi mbalimbali wa chama na Serikali wakimkaribisha Mbunge na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhandisi Stella Manyanya kwenye viwanja vya mkutano vya Makumbusho ya Taifa ya Majimaji Songea

Mama wa Kimasai akimpatia zawadi za kabila hilo Mbunge Mhandisi
Stella Manyanya baada ya kuwahutubia wananchi wa Songea Mjini katika viwanja vya Makumbusho ya Taifa ya Majimaji
Viongozi wa chama wa Wilaya ya Namtumbo wakimpokea Mbunge Mhandisi Stella Manyanya

MAKANISA NDUGU KUFANYA TAMASHA LA UIMBAJI MIAKA 50 YA UHURU WA TANZANIA


                    Mhashamu Askofu Mkuu Norbert Mtega
Na Gideon Mwakanosya,Songea
WAUMINI wa Makanisa ndugu katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea Mkoani  Ruvuma wanatarajia kufanya tamasha kubwa la uimbaji  la Jubilei  ya miaka 50 ya uhuru wa Taifa la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Oktoba 29 Mwaka huu ambapo mgeni rasmi kwenye tamasha hilo ni Waziri wa Habari utamaduni na michezo Dr. Emmanuel  Nchimbi.
Akizungumza na mtandao wa www.stephanomango.blogspot.com  jana ofisini kwake Katibu wa umoja wa Makanisa ndugu katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea Mackie Mguhi amesema kuwa tamasha hilo ambalo linatarajiwa kuhuzuliwa na mamia ya waumini wa Makanisa ndugu wakiwemo Askofu Mkuu wa Kanisa katoliki jimbo kuu la Songea Norbert Mtega, Askofu wa dayosisi wa Ruvuma kanisa la Angelikana  Dr. Martenius Kapinga, Mkuu wa kanisa la kiinjili la kiliteli Tanzania (KKKT) Mchungaji Nashoni kikalawa Pamoja na mkuu wa mkoa wa Ruvuma Saidi Mwambungu 
Mguhi ameyataja Makanisa yanayeunda umoja huo ambao umeandaa tamasha kubwa ni kanisa katoliki Parokia za Songea,Mjimwema na Bombambili kanisa la kinjili la kiluteli Tanzania (KKKT) Usharika na Songea mjini na Msamala kanisa la Anglikana Songea Mjini pamoja na kanisa la Moraviani Tanzania ushirika wa Songea.
Ameeleza zaidi kuwa Tamasha hilo litafanyika siku ya jumamosi oktoba 29 mwaka huu katika uwanja wa michezo wa mpira wa miguu wa Majimaji ambalo litatanguliwa na maandamano makubwa  ya waumini wa Makanisa ndugu yatakayoanzia katika kanisa la Luthelani Songea Mjini hadi uwanja wa Majimaji.
Amesema kuwa lengo la tamasha hilo ni kuonyesha furaha kubwa kwa waumini wa Makanisa ndugu katika manispaa ya Songea kwa jubilee ya nchi ya Tanzania Kwa vitendo pili kuendelea kumshukuru mungu na kumuomba kwa upendo ,Amani na uvumilivu aliyo ijalia nchi ya Tanzania pamoja na viongozi  na wananchi kwa ujumla .
Amebainisha zaidi kuwa  katika tamasha hilo pia litaudhuliwa na wanafunzi wa chuo cha elimu ya Taifa Songea , Shule ya wasichana na Wavulana Songea na kwaya zaidi ya ishirini zimesibitisha kushiriki kwenye tamasha hili na viongozi wa makanisa hayo wanatarajiwa kuongoza ibada ya maalumu ya kuiombea amani kwa mwenyezi mungu kwani  Tanzania toka ipate uhuru hawajawai kupata misuko suko ya aina yoyote tofauti  na nchi zingine zikiwemo baadhi ya nchi zilizo pakana na Tanzania ambazo wananchi wake wakipata shida kutokana na vita.

Wednesday, October 26, 2011

MHANDISI MANYANYA AANZA ZIARA KWA KUPOKELEWA NA DUA MBALIMBALI KUTOKA KWA WASAIDIZI WA CHIFU WA KINGONI

Wasaidizi wa Chifu wa Kabila la Kingoni (Mjukuu wa Nduna Songea Mbano na Gama) wakitoa dua zao kwa Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Ruvuma na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhandisi Stella Manyanya ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ushauri ya Makumbusho ya Taifa ya Majimaji alipotembelea Makumbusho ya Taifa ya Majimaji Songea kabla ya kuanza ziara yake ya siku tano mkoani Ruvuma

Wazee wa Ngoma ya Beta wakimpa Nasaha mbalimbali  Mhandisi Manyanya kwa heshima na Mila za Desturi za Kingoni walipomtembelea Ofisini kwake kabla ya kuanza ziara yake

Ndivyo mapokezi ya Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhandisi Manyanya alipopokelewa na wakina mama wa BetterLife Tanzania mara alipowasili mjini Songea kabla ya kuanza ziara yake ya siku tano mkoani Ruvuma

MBUNGE STELLA MANYANYA AFANYA ZIARA YA KIKAZI YA SIKU TANO MKOANI RUVUMA

                                                     Mhandisi Stella Manyanya
Na Mwandishi Wetu,Songea
MBUNGE wa Viti Maalumu Mkoa wa Ruvuma Mhandisi Stella Martin Manyanya ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Rukwa anatarajia kuanza ziara ya siku tano mkoani Ruvuma kuwashukuru wapiga kura wanawake na wananchi kwa ujumla wao  kwa kukipa ridhaa chama cha Mapinduzi (CCM)kushika dola
Katika ziara hiyo Octoba 26 Mhandisi Manyanya atafanya mkutano wa hadhara Songea Mjini na Kijiji cha Kitanda Wilayani Namtumbo ambapo atafungua vikundi vya ujasiliamali na kuwahutubia wananchi wa eneo hilo
Octoba 27 atawasili Wilayani Tunduru na kufanya mkutano wa hadhara ambapo Octoba 28 atafanya mkutano Songea Vijijini,Octoba 29 atasalimia Halmashauri kuu ya chama cha Mapinduzi pia atafanya mkutano wa hadhara  kata ya Burma Wilayani Mbinga
Ziara hiyo itakamilika Octoba 30 kwa kufanya mkutano wa hadhara Wilayani Nyasa katika Kata ya Ngumbo na kisha kurejea Mkoani Rukwa kwa shughuli zingine za kiserikali

Tuesday, October 25, 2011

UCHAKACHUAJI WA MAPATO YATOKANAYO NA MAZAO YA MISITU MBINGA WASABABISHA HASARA

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga Shaib Mnunduma
Na Gideon Mwakanosya,Mbinga
HALMASHAURI ya Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma imepata hasara ya shilingi milioni 18 kupitia idara yake ya maliasili na mazingira kutokana na uzembe uliofanywa na watumishi wachache wa idara hiyo, waliopewa dhamana ya ukusanyaji wa ushuru wa mazao ya misitu.
Kwa mujibu wa vyanzo vya uhakika kutoka katika halmashauri hiyo ambavyo vilizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti kwa sharti la kutotaja majina yao, vilisema kuwa hasara hiyo imetokea kufuatia vitabu vyenye risiti ambavyo hutumika kukusanyia ushuru huo vimepotea katika mazingira ya kutatanisha.
Habari zinaeleza kuwa jitihada za kutafuta vitabu hivyo vilivyopotea mpaka sasa zimegonga mwamba jambo ambalo uongozi wa wilaya ya Mbinga, ulilazimika kuchukua hatua za kuripoti kituo kikuu cha polisi kwa msaada zaidi ambapo baadhi ya watumishi wa idara ya maliasili na mazingira wilayani humo waliwekwa mahabusu kwa siku kadhaa.
Aidha pamoja na watumishi hao kuwekwa mahabusu hivi sasa wameachiliwa huru na hakuna hatua zingine walizochukuliwa huku wakiendelea na kazi zao kama kawaida kitendo ambacho kimekuwa kikisababisha kuzua maswali mengi kutoka kwa watumishi wengine wa halmashauri hiyo.
Utaratibu wa halmashauri ya wilaya hiyo katika utoaji wa vitabu hivyo unaeleza kuwa alikabidhiwa mkuu wa kitengo cha kukusanya ushuru wa mazao ya misitu Nambole   Nanyanje ambaye huwagawia watumishi wenzake wanaohusika na suala la kukusanya ushuru huo.
Mwandishi wa habari hizi alipomuuliza kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga Bernard Semwaiko juu ya tuhuma hizo alikiri kuwepo kwa upotevu wa fedha na vitabu hivyo huku akisema halmashauri yake imekwisha kamilisha utatuzi wa jambo hilo.
“Ni kweli kiasi hiki cha fedha kilipotea kutokana na upotevu wa vitabu vilivyokuwa vikitumika kukusanyia ushuru wa mazao ya misitu, najua umewahi kusikia kuna baadhi ya watumishi tuliwaweka mahabusu”, alisema Semwaiko.
 Kadhalika Mwandishi alipotaka kujua undani wa tatizo hilo Semwaiko alifafanua kuwa lilibainika kufuatia wakaguzi waliokuwa wakifanya kazi ya kukagua mahesabu ya halmashauri hiyo, ndipo wakaguzi hao waligundua kuna upotevu wa fedha hizo na vitabu, yenye jumla ya thamani ya shilingi milioni 18 kutoka idara ya maliasili na mazingira wilayani humo ambavyo vilitumika kukusanyia ushuru wa mazao ya misitu.

AJALI YAUA MMOJA NA KUJERUHI WATU SITA BAADA YA GARI KUACHA NJIA NA KUPINDUKA

Na, Gideon Mwakanosya SongeaMTU mmoja mkazi wa Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma amekufa papohapo na wengine sita wamejeruhiwa vibaya baada ya basi walilokuwa wakisafiria kutoka Songea mjini kwenda Namtumbo kuacha njia na kupinduka.
Akizungumza na waandishi wa habari jana ofisini kwake Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma Naftari Mantamba amesema kuwa tukio hilo limetokea oktoba 24 mwaka huu majira ya saa 8.00 mchana katika eneo la Mletele Songea mjini.
Mantamba amemtaja aliyefariki dunia kuwa ni Sabina Similia(80) mkazi wa eneo la Faraha Store Mbinga mjini na kwamba waliojeruhiwa amewataja kuwa ni Failuna Komba(70) na Hassan Ally(40) wote wakazi wa kijiji cha Mgombasi kilichopo katika wilaya ya Namtumbo.
Amewataja majeruhi wengine kuwa ni Flora Mamzi(39) mkazi wa mtaa wa Furaha Store Mbinga mjini,Amina Komba(63) mkazi wa kata ya Lizabon Songea mjini,Mohammed Hassan(50) mkazi wa mtaa wa Ruhila Songea mjini na Omary Mtumbuka(42) mkazi wa kijiji cha Litola kilichopo wilayani Namtumbo.
Kaimu Kamanda Mantamba amefafanua kuwa basi hilo lenye namba za usajili T761 ATN aina ya Isuzu Forward ambalo lilikuwa limebeba abiria kutoka Songea mjini kuelekea Namtumbo na kwamba lilikuwa likiendeshwa na Hamis Chidumule(35) mkazi wa kata ya Ruvuma Songea mjini likiwa kwenye mwendo mkali liliacha njia na kupinduka.
Amesema kuwa majeruhiwa mpaka wamelazwa katikahospitali ya mkoa kwenye wodi za majeruhi ambapo hali zao zinaendelea vizuri  na kwamba chanzo cha ajali hiyo gari hiyo ilikuwa kwenye mwendo mkali hali iliyosababisha dereva ashindwe kumudu ukukani na hivyo kuacha njia na kupinduka.
Hata hivyo polisi mkoani hapa imefanikiwa kumkamata dereva wa gari hilo na kwamba kwa sasa uchunguzi unaendelea kufanyika ukikamilika mtuhumiwa atafikishwa mahakamani.

WANANCHI WA MPAKANI MWA MSUMBIJI NA TANZANIA WATAKA BARABARA KWA KIWANGO CHA LAMI

 Meneja wa Tanroads Mkoa wa Ruvuma Abraham Kissimbo akitoa maelekezo ya ujenzi wa daraja la Mkenda kwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu hayupo pichani alipotembelea mpaka wa Msumbiji na Tanzania
 Daraja la Mkenda linalounganisha nchi ya Msumbiji na Tanzania
 Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu akiwa na Viongozi mbalimbali wakipita juu ya daraja la Mkenda wakielekea nchi jilani ya Msumbiji
 Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu akipata maelekezo ya ujenzi wa daraja linalounganisha nchi ya Msumbiji na Tanzania lililojengwa kivukoni Mkenda kutoka kwa Meneja wa Tanroads mkoa wa Ruvuma Abraham Kissimbo
Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu (katikati) akipokea maelezo ya jengo lililojengwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania(TRA) kutoka kwa Meneja wa TRA mkoa wa Ruvuma Apily Mbaruku kushoto na Mkuu wa Wilaya ya Songea Thomas Oley Sabaya kulia
Na Stephano Mango,Songea
WANANCHI wa kitongoji cha Mkenda kilichopo katika kijiji cha Nakawale kata ya Mhukuru wilaya ya Songea vijijini mkoani Ruvuma wameiomba Serikali kupitia Wizara ya Miundombinu kuona umuhimu wa kuwakumbuka kwa kuwajengea barabara kwa kiwango cha lami ili waweze kusafirisha bidhaa zao yakiwemo mazao ya kilimo kiurahisi.
Ombi hilo wamelitoa jana kwa Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu wakati alipofanya ziara ya kutembelea kitongoji hicho kilichopo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji ambako Serikali imefanikiwa kujenga daraja la kudumu ambalo linaunganisha na nchi hiyo jirani katika mto Ruvuma.
Mmoja wa wakazi wa kitongoji hicho Ramadhani Hussein alisema kuwa kitendo cha Serikali cha kujenga daraja la Mkenda kwenye mto Ruvuma kumepelekea kuwepo kwa maendeleo makubwa kwa wananchi wa eneo hilo kutokana na biashara zinazofanyika kati yao na wananchi wa nchi jirani ya Msumbiji.
Hussein alisema kutokana na hali hiyo ni vyema Serikali ikafikiria kujenga barabara kwa kiwango cha lami kutoka Songea mjini hadi Mkenda yenye urefu wa kilometa  124   hali itakayokuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi wa tarafa ya Mhukuru ambayo ipo mpakani.
Naye Mwenyekiti wa Chama Cha FRELIMO kijiji cha Congress nchini Msumbiji John Bosko ambaye alihudhuria mkutano huo wa hadhara alimwomba Mkuu wa mkoa wa Ruvuma kufanya mawasiliano na Serikali ya Msumbiji ili kuhakikisha kuwa barabara ya kutoka Songea hadi Mkenda inajengwa haraka na kwamba barabara kutoka Mkenda hadi Maputo inajengwa kwa manufaa ya wananchi wa pande zote mbili.
Kwa upande wake Meneja wa wakala wa barabara mkoa wa Ruvuma(TANROADS) Mhandisi Abraham Kissimbo alisema kuwa Serikali imedhamira kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami na kwamba mpaka sasa tayari michoro imekamilika na kinachosubiriwa ni utekelezaji.
Naye Mkuu wa mkoa wa Ruvuma aliwaeleza wananchi hao kuwa Serikali imedhamiria kwa dhati kufanyia matengenezo barabara zote zikiwemo za mipakani ili zipitike kiurahisi na kwamba aliwahimiza wananchi kujikita kwenye kilimo ili barabara hizo zitakapokamilika waweze kusafirisha mazao yao pamoja na bidhaa zingine.
Aidha Mwambungu aliwataka wakazi wa kitongoji hicho kujitokeza kwa wingi kuchangia nguvu zao kwenye ujenzi wa kituo cha polisi hasa ikizingatiwa kitongoji hicho cha Mkenda kipo mpakani mwa nchi ambapo kwa siku za usoni unatarajia kuwa mji mdogo hali itakayopelekea pia kuwepo na vitendo vya uharifu na kwamba alichangia shilingi milioni moja kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho.

Monday, October 24, 2011

SANGOMA MBARONI KWA TUHUMA ZA KUMTOA MIMBA BINTI YA MIAKA 19

Na Cresensia Kapinga,Songea
JESHI la Polisi mkoani Ruvuma linamshikilia Mganga wa jadi Christian Ngonyani (58) mkazi wa kijiji cha Ngahokola Songea Vijijini kwa tuhuma za kumtoa mimba yenye umri wa miezi tisa  ya Mwanamke  Rehema Njerekela (19) mkazi wa kijiji cha  Magagula  wilaya hiyo.
Akizungumza na waandishi wa Habari kwa niaba ya Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma Inspecta  Paul Mashimbi amesema kuwa tukio hilo limetokea  oktoba 18 mwaka huu majira ya saa mbili usiku katika kijiji cha Magagula  ambapo Mganga huyo alipatiwa kiasi cha shilingi elfu arobaini na tano kwa lengo la kumtolea mimba  ya miezi tisa.
Alisema kuwa,awali mwanamke huyo alienda kwa Sangoma huyo wakati akiwa na ujauzito wa miezi minne ambapo walipojaribu kumtoa mimba hiyo iligoma kutoka  lakini ilipofika oktoba 18 mwaka huu akiwa na sangoma huyo walirudia tena kuharibu mimba hiyo lakini safari hii Kilitoka kiumbe chenye jinsia ya kiume kikiwa hai .
Inspekta mashimba ameongeza kuwa,mara  baada ya kufanya jaribio hilo na kufanikiwa kutoa mtoto akiwa hai  siku mbili baadaye Mwanamke huyo alimfukia akiwa hai baada ya kumchimbia shimo upenuni mwa nyumba yao na kumfukia akiwa hai.
Alisema, mara baada ya tukio hilo polisi walipokea taarifa toka kwa wasamaria wema zikiwaeleza kuwepo kwa tukio la mwanamke huyo kumfukia mtoto wake akiwa hai na walipofika  na kufukua  walimkuta mtoto huyo akiwa ameshafariki .
Alisema, Jeshi la polisi linamshikilia mwanamke huyo pamoja na Sangoma kwa kosa  la mauaji na upelelezi zaidi kuhusiana na tukio hilo unaendelea ,na ukikamilika watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma za mauaji.
Aidha,Mganga mkuu mfawidhi wa hospitali ya mkoa  Dkt.Benedicto Ngaiza amethibitisha kumpokea mwanamke huyo ambaye amelazwa hospitalini hapo kwa ajili ya matibabu  baada ya kupata maumivu makali baada ya kuharibu mimba hiyo.
MWISHO.

WAKAZI WA MKENDA WAHAHA KUSAKA MAJI SAFI NA SALAMA MIAKA 50 YA UHURU WA TANZANIA


Wakazi wa Kitongoji cha Mkenda Kijiji cha Nakawale Kata ya Muhukuru wakihaha kuchota maji kwenye bomba maarufu kwa Danida ikiwa ni miaka 50 ya UHURU na wakati mwingine ulazimika kusaka maji hayo zaidi ya kilometa 3,wananchi hao wamekuwa wakikabiliwa na uhaba wa huduma za afya,elimu,miundombinu na maji

MTAJI WA MASKINI NI NGUVU ZAKE MWENYE NDIVYO INAVYOTAFSIRIKA PICHA HII

Vijana ambao hawakuweza kufahamika majina yao mara moja wakiwa wanasukuma mkokoteni jilani na Kanisa Katoliki Jimbo la Songea Mjini ikiwa ni kuelekea miaka 50 ya UHURU wa Nchi yetu kama walivyokutwa na mpiga picha wa mtandao huu wa http://www.stephanomango.blogspot.com/

Sunday, October 23, 2011

MTUHUMIWA WA MAUAJI YA LEVINA ADAKWA,AKUTWA NA VITU VYA MAREHEMU

Na Gideon Mwakanosya, Songea
 
JESHI la Polisi mkoani Ruvuma limemtia mbaroni Thomas Jilala (22) mkazi wa Mwanza kwa tuhuma za kumuua anayedaiwa kuwa mpenzi wake Levina Kihwili (26) mkazi wa Mfaranyaki katika Manispaa ya Songea ambaye alikutwa akiwa amekufa kwa kunyongwa shingo katika nyumba ya kulala wageni ya Mikumi mjini hapa
 
Akizungumza kwa niaba ya Kamanda wa Polisi, Kaimu Kamanda wa polisi mkoa wa Ruvuma, Inspekta Paulo Mashimbi alisema tukio hilo lilitokea Octoba 22 mwaka huu majira ya saa 2 asubuhi huko kwenye nyumba hiyo ya kulala wageni chumba namba Kumi.
 
Insekta Mashimbi alisema kuwa ililetwa taarifa katika kituo kikuu cha polisi mjini Songea kuwa katika nyumba ya kulala wageni ya Mikumi chumba namba Kumi kilichokuwa kikitumika na watu wawili alikutwa mwanamke akiwa amefariki dunia huku mwanaume aliyekuwa naye akiwa amekimbia.
 
Alisema mnamo octoba 23 mwaka huu majira ya saa Sita usiku mtuhumiwa anayedaiwa kufanya mauaji hayo Jilala ambaya anadaiwa alikuwa Mpenzi wa marehemu alikamatwa akiwa anatoroka kuelekea barabara ya Songea-Tunduru maeneo ya Namtumbo.
 
Alieleza kuwa mtuhumiwa Jilala baada ya kukamatwa alikutwa na baadhi ya vitu vya marehemu ikiwemo Saa aliyokuwa ameivaa kabla ya kuuawa pamoja na simu Mbili za mkononi vyote vikiwa ni mali ya marehemu.
 
Alifafanua kuwa mtuhumiwa pia alikutwa na vifaa vingine vilivyoibiwa kwenye ofisi aliyokuwa akifanyia kazi marehemu usiku wa kuamkia siku ya tukio hilo la mauaji.
 
Hata hivyo vyanzo vya habari vimeeleza kuwa Jilala kabla hajafanya kitendo hicho cha kinyama alikuwa akionekana mara kwa mara katika Ofisi ya marehemu ijulikanayo kwa jina la Mpenda Production kwa madai kuwa amekuja kutengeneza kadi za harusi ya kaka yake.
 
Aidha Jeshi la Polisi mkoani Ruvuma limesema linaendelea na uchunguzi dhidi ya tukio hilo na kwamba baada ya uchunguzi huo kukamilika mtuhumiwa atafikishwa mahakamani kujibu shitaka la mauaji linalomkabili.
 
Mganga mkuu mfawidhi wa hospitali ya mkoa mjini Songea, Dkt. Benedict Ngaiza alipohojiwa na waandishi wa habari ofisini kwake amethibitisha kuuawa kwa Levina na kwamba uchunguzi unaonesha kwamba alivunjika shingo baada kupigwa na kitu kizito.
 
Wakati huo huo Jeshi la Polisi linawatafuta watu wasiofahamika kwa tuhuma za kumuua mtu mmoja wa Kiume ambaye jina lake halijapatikana kwa kumchoma moto na mwili wake kuharibika vibaya.
 
Insekta Mashimba alisema tukio hilo lilitokea octoba 23 mwaka huu majira ya saa 12 asubuhi katika eneo la shule ya Msingi ya Bombambili mjini Songea ambako inahisiwa kuwa marehemu huyo alikuwa ni kibaka.
Mwisho.  

KIJANA ASIYEFAHAMIKA JINA LAKE AKUTWA AMEKUFA BAADA YA KUCHOMWA MOTO NA WATU WASIOFAHAMIKA KATIKA UWANJA WA BOMBAMBILI USIKU WA KUAMKIA LEO

 Mwili wa Marehemu ukiwa kwenye gari la Polisi nje ya Chumba cha kuhifadhia Maiti katika Hospital ya Mkoa Songea



 Mwili wa Marehemu ukishushwa kwenye gari la Polisi ukiingizwa kwenye chumba cha kuhifadhi Maiti katika Hospital ya Mkoa wa Songea
 Mwili wa Marehemu ukiingizwa kwenye chumba cha kuhifadhia Maiti kwa ajili ya kukamilisha taratibu kabla ya mazishi
Watu waliojitokeza kwenye chumba cha kuhifadhia maiti katika Hospital ya Mkoa Songea wakiwa na nyuso za huzuni baada ya kuuona mwili wa marehemu
Mtandao huu wa www.stephanomango.blogspot.com una laani vikali vitendo vya kujichukulia sheria mikononi kwa kuondoa haki muhimu ya binadamu ya kuishi kwani tunapaswa kutambua kuwa mwenye mamlaka ya kuondoa uhai wa binadamu ni Mwenyezi Mungu pekee,Binadamu tusinyang'anye mamlaka ya Mwenyezi Mungu

Matukio hayo yameanza kushamiri mkoani Ruvuma ambapo sababu zinazotajwa hazifanani na adhabu zinazotolewa kwa mkosaji kwani anapouawa hawezi kujilekebisha kwani tunaamini kuwa lengo la kuwepo kwa adhabu ni kumrekebisha mkosaji

HOSPITAL YA WILAYA TUNDURU YAKABILIWA NA CHANGAMOTO LUKUKI NA KUSABABISHA KERO KWA WAGONJWA NA WAUGUZI


Na Augustino Chindiye,Tunduru
WAGANGA na wauguzi wa Wilaya ya Tunduru wameonywa kuacha tabia za ubabaishaji wakati wa utekelezaji wa majukumu na shughuli zao za kila siku na kwamba Mganga Mkuu wa Wilaya hiyo hata husika katika utetezi wa mtumishi yeyote pindi sheria itakapotakiwa kufuata mkondo wake.

Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya hiyo Dkt. Alex kazula wakati akijibu swali juu ya kuwepo kwa malalamiko mengi kutoka kwa wananchi juu ya utendaji mbovu dhidi ya wataalamu wa idara hiyo huku kukiwa na taarifa za mgomo baridi kutoka kwa Madaktari,Maafisa Tabibu na Wauguzi wa Wilaya hiyo huku ofisi yake ikidai kuto kuwa na taarifa zozote juu ya kinacholalamikiwa na wataalamu hao.

Katika taarifa hiyo Dkt. Kazula alikiri kuwa hivi sasa Hospitali yake imegubikwa na wimbi kubwa la malalamiko mbalimbali kutoka kwa wagonjwa na watu wanaokwenda kuuguza wagonjwa katika Hospitali, Vituo vya Afya na Zahanati kuwa wataalamu wake hawawajibiki ipasavyo wanapokea fedha kutoka kwa wagonjwa na wamekuwa na majibu mabaya na wakati mwingine wamekuwa wakiwatukana wateja wao.

Dkt. Kazula aliendelea kueleza kuwa malalamiko mengine aliyoyapokea  ni pamoja na kushamiri kwa matukio ya  VIFO visivyo vya lazima ambavyo hutokea  kwa wagonjwa wanaoenda kutibiwa na kulazwa katika Hospitalini hali ambayo imekuwa ikizusha manung`uniko kutoka kwa wananchi kuwa Wataalamu hao wamekuwa hawajitumi katika kutekeleza wajibu wao wa kutoa tiba sahihi na kuokoa maisha ya wateja wao.

Alisema sambamba na malalamiko hayo pia ofisi yake inazo taarifa za malalamiko ya Waganga na Wauguzi hao kutoa huduma kwa upendeleo ambapo wagonjwa wasio na uwezo kifedha hawapatiwi huduma kabisa na kwamba ukiona Daktari au Muuguzi anahangaikia mgonjwa kwa nguvu zote ujue amepokea chochote (RUSHWA) kutoka kwa mgonjwa huyo.  

Kufuatia hali hiyo Dkt. Kazula amesema milango ipo wazi kwa wagonjwa na wauguzaji kwenda kutoa malalamiko na ushahidi dhidi ya watumishi hao ili atayebainika sheria ifuate mkondo wake ikiwa ni pamoja na mhusika kufukuzwa kazi.

Wakati hayo yakiendelea  baadhi ya wagonjwa na wauguzaji wa wagonjwa wanaolazwa katika hospitali ya Wilaya hiyo nao waliibua  malalamiko ya kuwepo kwa hali mbaya na harufu kali katika vyoo vilivyopo Hospitalini hapo.

Walisema kufuati hali hiyo wamekuwa wakilazimika kutoka nje hasa nyakati za usiku ili kupata hifadhi katika mapori yaliyopo eneo la uwanja wa Ndege uliofungwa baada ya kupoteza siza za kutua ndege.
Mwisho

WATUMIKIA KIFUNGO CHA MIAKA MITATU JELA KWA KOSA LA MAUAJI NA MWINGINE AACHIWA HURU

Na Augustino Chindiye, Tunduru

MAHAKAMA kuu Kanda ya Songea imewahukumu kifungo cha miaka mitatu kila mmoja mtu na dada yake baada ya kukiri na kupatikana na hatia ya kufanya kosa dogo la kuua bila kukusudia na kumuachilia huru mtoto wa miaka 14.

Akitoa hukumu hiyo Jaji wa Kanda ya Songea Jaji Hamisa kalombola alisema kuwa adhabu hizo zimetolewa baada ya kuzingatia hoja zilizotolewa na upande wa Jamhuri uliokuwa ukiongozwa na Mwanasheria wa Serikali Hamimu Nkoleye aliyeiomba Mahakama hiyo iwahukumu kifungo cha maisha huku upande wa utetezi ulioongozwa na Wakili wa kujitegemea Sebastian Waryuba akiiomba Mahakama hiyo iwapatie adhabu ndogo wateja wake akidai kuwa kukubali kwao kumeipunguzia usumbufu Mahakama hiyo.

Kaka na dada waliohukumiwa kutumikia kifungo hicho cha miaka mitatu Jela ni Hashim Msusa Ibrahim na Mwanahawa Msusa Ibrahim waliokuwa wanakabiliwa na Shauli la mauaji namba 8/2011 la kumuua marehemu Halifa abdalah February 2/2010 wakiwa wanagombea mfuko tupu wa kubebea mahindi wa kiroba cha mbolea ambapo tukio hilo lililotokea katika kijiji cha Lijombo Wilayani Tunduru.

Shauli jingine lililotolewa maamuzi na kufikia maamuzi ya kumuachilia huru yaani (Anconditional Discharge) baada ya Mahakama hiyo kumtia hatiani kwa kosa dogo la kuua bila kukusudia ni Shauli Namba 2/2011 lililo kuwa likimkabili Mwamini Mwandope (14) aliye muua marehemu Salome Sanga baada ya kutokea ugomvi kati yao katika tukio lilitokea katika Kijiji cha Hanga Wilayani Namtumbo Mkoani Ruvuma.

Jaji Hamisa kalombola aliendelea kueleza kuwa mahakama yake   imeamua kutoa adhabu hizo kwa kuzingatia kifungu cha Sheria Namba 119 kifungu kidogo (2a) na kifungu kidogo cha (4) vya sheria ya kanuni ya adhabu vinavyoipatia mamlaka Mahakama hiyo.
  
Awali kabla ya kutolewa kwa adhabu hizo watuhumiwa hao walitiwa hatiani na mahakama hiyo baada ya kukiri kufanya kosa dogo la kuua bila kukusudia  baadaya kusomewa kosa la kumuua bila kukusudia ambapo Mtoto aliye achiliwa huru alidaiwa kumuua marehemu Salome Sanga kwa kumchoma kisu baada ya kutokea ugomvi kati yao huku wanandugu Hashimu na Mwanahawa wakidaiwa kumuua kwa kumpiga na mangongo kichwani marehemu Halifa Abdala katika ugomvi wa kugombea mfuko tupu.

Jaji Kalombola alisema kuwa pamoja na mambo mengine Mahakama yake imeridhishwa na hoja zilizotolewa na Wakili wa Upande wa utetezi Sebastian Waryuba kwamba pamoja na mambo mengine kikiwemo kigezo cha kukubali kosa hilo mbele ya Jaji na kuiondolea Mahakama usumbufu mteja wake anastahili kupatiwa adhabu yenye unafuu chini ya kifungu cha 119 cha Sheria ya watoto namba 21ya mwaka 2009.

Awali katika ujenzi wa hoja za Utetezi kwa mteja huyo wakili msomi wa kujitegemea Sebastian  Waryuba alidai kuwa chini ya makosa hayo wateja wake wanapaswa kunufaika chini ya kifungu cha 119 cha sheria za kanuni ya adhabu sura ya 16 kama ilivyofanyia mapitio mwaka 2002 ambapo wakati mtuhumiwa akitenda kosa hilo Agosti 28/2010 na huku akimwelezea Mtoto Mwamini Mwandope kuwa wakifanya kosa hilo alikuwa na umri wa miaka 13, na sasa  ana Mtoto mchanga mwenye umri wa miezi 6 ambaye alijifungua wakati akiwa mahabusu.

Alisema kipitia kifungu hicho mteja wake anastahili kupewa adhabu ya kifungo cha nje ama kutumikia adhabu ya kutumikia jamii huku Mwanasheria wa Serikali Hamimu Nkoleye akiiomba mahakama hiyo impatie adhabu ya kifungo cha maisha.
Mwisho

Friday, October 21, 2011

SERIKALI YATAKIWA KUFUFUA VYOMBO VYA JAMII VINAVYOSHUGHULIKIA WATOTO WAISHIO KATIKA MAZINGIRA HATARISHI

Mwenyekiti wa Mtandao wa Mashirika yasiyo kuwa ya Serikali yanayojishughulisha na masuala ya Ukimwi Mkoani Ruvuma (RUNOWA) Mathew Ngarimanayo akiwasalimia wananchi waliohudhuria Mahafari ya Darasa la Saba katika Shule ya Msingi Sabasaba yaliyofanyika hivi karibuni

Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Sabasaba Simon Lupanga akisalimia ndugu,jamaa,walezi na wazazi waliofika katika Mahafari hayo kuwapongeza wahitimu wa shule hiyo

Mwenyekiti wa Shule hiyo Joseph Kalande akitoa nasaha zake kwa wahitimu wa shule ya Msingi Sabasaba,kulia ni Mratibu wa Elimu Kata ya Matarawe Theofrida Mango,wa kwanza kushoto Mwalimu Mkuu wa Sabasaba Simon Lupanga,wa pili Mwenyekiti wa RUNOWA)Mathew Ngarimanayo

Mgeni Rasmi katika Mahafari ya Shule ya Msingi Sabasaba Mwenyekiti wa RUNOWA Mathew Ngarimanayo akiwahutubia wananchi waliohudhulia Mahafari hayo

Wazazi na Walezi wakisikiliza kwa umakini hotuba ya Mgeni Rasmi Mathew Ngarimanayo aliyoitoa katika Mahafari hayo
Na Stephano Mango,Songea
SERIKALI  imetakiwa kusimamia kikamilifu mpango wa mifuko ya jamii ya kusimamia watoto wanaoishi katika mazingira magumu ili waweze kusaidiwa na jamii wanamoishi kwa kutumia kamati maalumu ya kuratibu watoto hao kuanzia ngazi ya mitaa hadi Wilaya ili kuweza kuleta ustawi na maendeleo ya watoto hao
Wito huo umetolewa jana na Mwenyekiti wa Mtandao wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali yanayojishughulisha na masuala ya Ukimwi Mkoani Ruvuma(Runowa) Mathew Ngarimanayo wakati akihutubia kwenye mahafari ya darasa la saba Shule ya Msingi Sabasaba
Ngarimanayo ambaye alikuwa mgeni rasmi katika mahafari hayo alisema kuwa suala la watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi ni bomu kubwa ambalo linazinyemelea familia zetu na taifa kwa ujumla hivyo kila mwananchi anatakiwa aamke na kutambua kuwa watoto hao wanaongezeka siku hadi siku katika jamii zetu
Alisema kuwa kila mdau popote alipo aliangalie suala hilo na achukue hatua stahiki ya kupunguza wimbi hilo kwanikwasasa takwimu za watoto hao mkoani Ruvuma imefika jumla ya watoto 32,532 ambapo sababu zinazosababisha hali hiyo ni pamoja na mimba za utotoni,kuzaa nje ya ndoa,umasikini wa kipato katika familia,mifarakano ya wanandoa,magonjwa mbalimbali,ajali za barabarani na maafa mengine
Alisema kuwa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii mwaka 2006 na 2008 ilifanya zoezi la utambuzi wa watoto hao katika Wilaya za Mkoa wa Ruvuma na wakaweka utaratibu ambao wananchi walipaswa kuchukua na kuhakikisha watoto hao wanasaidiwa katika jamii wanamoishi
Alieleza zaidi kuwa katika ngazi za mitaa,Kata,Wilaya viliwekwa vyombo ambavyo vinaweza kukaa na kujadili kwa kina masuala ya watoto hao na kuweka mikakati ya kumaliza tatizo hilo kwa kutumia Kamati za Ukimwi kuanzia ngazi ya mitaa hadi Wilaya kwani Kamati hizo zingekuwa zinafanya kazi yake kikamilifu tatizo la watoto hao lingekwisha
“Wahitimu tambueni elimu mliyoipata ni ya msingi tu na kwamba safari mliyonayo ni ndefu maishani ili mfikie mafanikio ya kweli,msibweteke naomba Mungu awajalie wote mfaulu kwenda Sekondari,vyuo na kuendelea pia mkawe mfano wa tabia njema huko nyumbani kwa kuwa nyie ndio mnaotegemewa kushika nafasi mbalimbali katika jamii,epukeni vitendo viovu ambavyo vinaweza kufuta ndoto zenu katika maisha”alisema Ngarimanayo
Awali akisoma risala ya wahitimu hao Sauna Juma alisema shule hiyo ina watoto waishio katika mazingira hatarishi 17 ambapo kati yao wa 4 wanahitimu leo na kwamba shule ina kabiliwa na changamoto mbalimbali za ujenzi wa madarasa na ofisi za walimu
Akijibu risala hiyo mgeni rasmi Ngarimanayo alichangia mifuko 10 ya saruji na kuliagiza shirika la Swaat/Sedeco ambalo linafanya kazi katika Kata ya Matarawe ambapo shule ya Sabasaba ipo kuwatambua watoto ngo hao na kuwaingiza katika mpango ili waweze kuhudumiwa haraka iwezekanavyo kadiri ya mahitaji ya vipaumbele vya watoto wenyewe
MWISHO