About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Saturday, August 27, 2011

Diwani wa Kata ya Mshangano Faustine Mhagama akizungumza na ndugu na jamaa zake akiwa katika Kituo kikuu cha Polisi Songea baada ya kulipoti kituoni hapo akiwa nje kwa dhamana,katikati Joseph Haule ambaye alikuwa ni mtangazaji wa uwepo wa maandamano,kushoto ni dereva wa gari la matangazo ya maandamano Suzo Luoga



POLISI WAMKAMATA DIWANI NA WAZUIA MAANDAMANO SONGEA
Na,Stephano Mango,Songea

JESHI la Polisi mkoani Ruvuma liliwakamata na kuwahoji zaidi ya masaa matatu wakazi wawili wa Kata ya Mshangano na Diwani wa kata hiyo kupitia Chama cha Mapinduzi(CCM)kwa tuhuma za kutangaza maandamano ya amani ya wananchi wa kata hiyo wakidai kupimiwa ardhi yao na Kampuni ya Ardhi Plan na kumtaka Waziri mkuu Mizengo Pinda kuwatimua kazi Mkurugenzi wa Manispaa ya Songea na Afisa Mipango Miji wa Manispaa hiyo ambao wameonyesha dhahili kutaka kuwadhulumu maeneo yao

Wakazi hao waliokamatwa na polisi ni Suzo Luoga ambaye alikuwa ni dereva wa gari ya matangazo lenye namba za usajili T 295 AJS aina ya Chesar mark II,Joseph Haule ambaye alikuwa mtangazaji na Faustine Mhagama ambaye ni Diwani wa kata hiyo ambao wote walikamatwa wakiwa kwenye gari hilo ambalo lilikuwa linapita kwenye mitaa ya kata hiyo kuwatangazia uwepo wa maandamano makubwa

Mmoja wa watuhumiwa hao Haule ambaye alikuwa mtangazaji alisema kuwa kazi hiyo alipewa na viongozi ambao wenyeviti wa serikali ya mitaa ya Namanyigu,Mshangano na Mitendewawa na kwamba shughuli hiyo ya utangazaji ilisimamiwa kikamilifu na Diwani wa kata lengo kuhakikisha ujumbe unawafikia wakazi wote wa kata hiyo

Naye wa Kata hiyo Mhagama akizungumza na mtandao wa http://www.stephanomango.blogspot.com/ jana alikili kukamatwa na alidai kuwa yeye pamoja na wenzake walikamatwa na Polisi majira ya saa tatu usiku huko katika eneo la Mshangano na waliamriwa kuingia kwenye gari la Polisi wakiwa chini ya ulinzi mkali na kupelekwa kwenye kituo kikubwa cha Polisi

Alisema kuwa mara baada ya kufikishwa kituoni hapo waliamliwa kuvuliwa viatu,mkanda na kuanza kupekuliwa na kasha kuwekwa mahabusu ambapo baadae alifika Kaimu Mkuu wa Polisi wa Wilaya  akiwa ameongozana na Askari Kanzu wawili ambao walianza kuwahoji hadi saa tano na nusu usiku ndipo walipoambiwa wawatafute watu wa kuwadhamini ambapo Mwenyekiti wa Kamati ya Mipango Miji wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea James Makene pamoja na Diwani wa Viti maalum Rehema Milinga walifika kituoni hapo na kuwadhamini

Kwa upande wake Makene ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Matarawe aliuambia mtandao huu kuwa kitendo cha kuwakamata Diwani na wenzake ni uonevu mkubwa na kinyume na utawala bora kwa kuwa Serikali ya Kata ya Mshangano ilipeleka barua ya kuomba kibali cha maandamano toka tarehe 19.8.2011 ambapo mpaka wanakamatwa walikuwa hawajapewa barua wala maelezo ya aina yoyote jambo ambalo liliashiria kukubaliwa ingawa baada ya kuwaweka mahabusu ndipo wakapewa barua ya maelekezo jambo ambalo limeleta utata mkubwa wa uadilifu wa jeshi hilo

Naye Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma Michael Kamuhanda alisema kuwa wananchi wa kata ya Mshangano waliomba kibali cha kutaka kufanya maandamano makubwa ya amani lakini katika barua yao ilionyesha mapungufu mengi ikiwa ni pamoja na kutoeleza tarehe,muda na njia ambayo maandamano yatapita

Kamuhada alisema kuwa tayari Serikali ya Kata ilipewa barua ya maelekezo na Jeshi la Polisi yenye kumbukumbu namba.SOA.3.6/65 ya tarehe 25.8.2011 ambayo ilipokelewa na Diwani wa kata hiyo majira ya saa tatu usiku
MWISHO

Katibu Mpya wa Jimbo la Songea Mjini Chadema Masumbuko Paulo

CHADEMA SONGEA WAPATA KATIBU MPYA WA JIMBO
Na,Stephano Mango,Songea
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Wilaya ya Songea mkoani Ruvuma kimempata Katibu mpya wa Jimbo la Songea Masumbuko Paulo katika uchaguzi wa wanachama wa chama hicho uliofanyika jana katika Ofisi ya Kata ya Mfaranyaki
 
Akitangaza matokeo hayo Mwenyekiti wa Jimbo hilo ambaye pia ni Diwani wa kata ya Majengo mjini hapa Idd Abdalah alisema kuwa wanachama waliopiga kura ni 80 ambapo Masumbuko Paulo amepata kura 54,Ajaba Nditi alipata kura 18, Zuber Tindwa alipata kura 8 ambapo Christopha Nyoni alipata kura 0
 
Abdalah alimtangaza Masumbuko Paulo kuwa ndiye ameibuka mshindi wa kwanza na hivyo kuanzia hapo anakuwa Katibu mpya wa Jimbo hilo na kwamba anatakiwa kuanza kazi mara moja ili kuweza kuendana na kasi ya chama hicho
 
Awali Mwenyekiti huyo aliwaambia wajumbe kuwa nafasi hiyo ya Ukatibu ilikuwa wazi kutokana na aliyekuwepo katika nafasi hiyo kuiacha na kwenda kufanya kazi kwenye Mashirika yasiyoya kiserikali
 
Alifafanua zaidi kuwa katika uchaguzi huo Wagombea walikuwa watano ambapo mgombea Said Ligema aliamua kujitoa dakika za mwisho za uchaguzi jambo ambalo viongozi wa Wilaya walikubaliana na uamuzi wake huo
 
Akiwashukuru wajumbe kwa kumchagua Masumbuko Paulo alisema kuwa imani na dhamana waliyompa ni kubwa sana hivyo atakitumikia chama kwa uadilifu mkubwa ili kiweze kupata ushindi stahiki katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa na chaguzi zingine zijazo
 
Masumbuko alisema kuwa Chama kipo katika harakati kubwa za kujiimalisha maeneo ya pembezoni mwa miji na vijijini hivyo kazi hiyo ya kujikita maeneo hayo kwa lengo la kukisambaza chama ni jukumu la wananchama wote wenye mapenzi ya dhati na chama hicho
 
Akifunga mkutano huo wa uchaguzi Mwenyekiti wa Chama hicho Wilaya ya Songea Peter Mboya alisema kuwa wanachama ndio nguzo stahiki ya chama chochote duniani hivyo ni vema popote pale alipo mwanachama anatakiwa afanye jambo kwa maslahi ya chama
 
Mboya alisema kuwa muda wa mabadiliko ya kitaifa umefika ambapo chama hicho kinatakiwa kuchukua dhamana ya kuwaongoza watanzania hivyo ni vema tukaonyesha kwa dhata mbele ya wananchi kuwa tunaweza kuwaondoha hapa walipo katika kipindi hiki cha miaka 50 ya uhuru na kuwapeleka katika hali nyingine ya ustawi wa maisha yao
MWISHO