About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Thursday, December 1, 2011

KIJANA TAIFA LA KESHO NI FALSAFA ILIYOPOTOSHWA KWA MAKUSUDI

Vijana wa kundi la sanaa la Wazalendo wakiwa kwenye picha ya pamoja baada ya kumaliza kikao chao cha maandalizi ya uzinduzi wa filamu ya The Challenge(Majaribu) inayotarajiwa kuzinduliwa Disemba 22 mwaka huu

Na Stephano Mango.Songea
 
TAIFA lolote Duniani haliwezi kukua na kuwa imara kiuchumi na kijamii bila makundi yote ya jamii kushirikishwa kikamilifu katika mapambano dhidi ya umasikini,maradhi na ujinga.

Ni wazi kuwa katika ulimwengu huu wa sasa,asilimia kubwa ni vijana ambao kimsingi ndio wanaopaswa kuwa viongozi wa leo na kesho na nguvu yao inahitajika sana katika jamii zetu kutokana na maarifa na mchango wao katika kusukuma gurudumu la maendeleo ulivyo mkubwa.

Hivyo basi, vijana ni kundi kubwa na rasilimali muhimu katika kuleta maendeleo ya taifa lolote lile duniani kutokana na nguvu na fikra za kimapinduzi walizo nazo.

Ukweli wa jambo hilo huwa ni rahisi kudhihirika waziwazi endapo vijana wataandaliwa vyema katika jamii zao kushiriki na kushirikishwa katika kubuni, kupanga na kutekeleza mikakati mbalimbali ya mandeleo.

Viongozi wengi wamekuwa wakisema mara kwa mara hasa wanapowapa nasaha utasikia wakisikika wakisema “Vijana ni Taifa la kesho fanyeni kazi kwa bidii na sio kuzurula ovyo, hampaswi kuishi lelemama na kuzubaa katika vijiwe huku mkipiga soga ambazo hazina umuhimu katika maisha yenu kwa kuwa kuwepo kwa vijiwe husababisha vishawishi vikubwa katika anasa na tamaa za kumiliki mali pasipo kufanya kazi.
 
Kitendo cha kuwafungua vijana masikio na kuyeyusha fikra mgando ambazo zinatawaliwa na uvivu,uchu wa mali na maisha ya anasa kilikuwa ni kizuri na chenye busara katika fikra yakinifu katika kukabiliana na changamoto zao

Ufanyaji wa shughuli za kimaendeleo ambazo zinaleta ukombozi katika jamii zetu ni jambo la kheri na huleta faraja katika maisha na mustakabali wa harakati za vijana wenyewe na jamii zao.
 
Nimekusudia kuandika makala haya kutokana na kushindwa kuivumilia falsafa inayotumika mara nyingi hasa na viongozi wengi ambao wanadhamana mbalimbali katika nchi hii,ujumbe unaotolewa huenda ulikuwa mzuri katika maisha ya vijana lakini kauli ya kusema vijana ni taifa la kesho ndiyo inayoleta ugomvi katika harakati za vijana na hapa ndio hoja yangu.

Ni dhahiri kuwa falsafa ya “vijana Taifa la kesho” imekuwa ikisemwa mara nyingi ambayo ni upotoshwaji mkubwa katika uhalisia wa mambo licha ya kuwa kauli yenyewe sio ngeni katika masikio ya jamii, kwani imekuwa ikijirudia mara kwa mara katika majukwaa mbalimbali.

 Kuna juhudi kadha wa kadha zimefanyika na wanaharakati mbalimbali wa masuala ya vijana katika kuipinga falsafa hiyo na kuonyesha falsafa mbadala katika kuweka mambo sawa na kupunguza malumbano yasiyo ya msingi

Ila kutokana na ugumu wa wanasiasa wengi kukubali mabadiliko chanya na yenye kueleweka katika maisha ya vijana kwa sababu zao binafsi ikiwemo hofu ya kizazi kipya kuchukua nafasi katika nyanja mbalimbali za uongozi,wanaendelea kuleta mikaganyiko katika jamii kwa faida zao za ulafi wa madaraka

Viongozi hao wamebaki kutoa mahubiri hasi ambayo hayana mantiki bali ni nguvu ya kuwavesha vijana kilemba cha ukoka na fikra mgando za kusubiri muda wa kuitumikia nchi yao kwa kutumia hoja hafifu ya kjana Taifa la kesho pasipo kesho kutimia

 Lugha wanayoitumia ni laghai na kimantiki neno kesho huwa halikamiliki katika mfululizo wa siku ingawa kimsingi kesho ni neno ambalo lina uhalisia wake kinadharia zaidi kuliko kivitendo.

 Jambo ambalo linathibitishwa na kamusi ya Kiswahili sanifu iliyotungwa na Taasisi ya uchunguzi wa Kiswahili chuo kikuu cha Dar-es-salaam ambapo inafafanua kuwa kesho ni “siku inayofuata baada ya leo, ni wakati ujao”.

Hiyo ina maana kuwa hakuna siku itimiayo katika mawazo ya kawaida ya binadamu iitwayo kesho kwa kuwa kesho huwa haifiki, ni siku ambayo inapaswa kusubiriwa tu kila kunapokucha.
 
Napata tabu sana katika kufikiri ili nielewe katika tafsiri ya kijana taifa la kesho,sielewi mwanzilishi wa falsafa hiyo alikuwa anamaanisha nini na kwa maslahi ya nani? Endapo yupo basi nahitaji mjadala naye ili kuweka sawa hoja husika

Wengi katika jamii waliisikia falsafa hii kwa mara ya kwanza katika utoto wao na hasa walipokuwa katika madarasa ya watoto kwenye shule za awali au za msingi.

 Ni wazi kuwa walimu walisikika mashuleni wakiitumia falsafa hii ili kutufanya tujifunze kwa maarifa na ujuzi na tuzoee kutenda mema na kujijengea sifa nzuri kwa ahadi kuwa sisi ni viongozi wa baadaye yaani tafsiri nzuri ni “Taifa la kesho”.
 
Je inawezekana kauli hiyo ilikuwa sahihi kipindi cha utoto wetu,sisi ambao kwa sasa ni vijana? naamini kila mmoja kwa kutumia vigezo vyake anaweza kujibu swali hilo hapo juu,

Katika mikataba na sheria mbalimbali za kimataifa zinafafanua kuwa binadamu mwenye umri kuanzia miaka 0-17 ni mtoto na haruhusiwi kufanya maamuzi yeyote mazito kuhusu maisha yake, ingawa kamusi tajwa hapo mwanzo inaleta utata katika vipande viwili vya umri hasa katika maana ya kijana,kamusi inasema kijana ni mwana mdogo,mtoto mwenye umri wa miaka 7 hadi12.

 Lakini katika mtazamo wa kawaida tunaamini kuwa kijana ni binadamu mwenye umri wa
kuanzia miaka 18-40 na wakati mwingine mpaka miaka 45.

 Ukirejea kamusi tajwa hapo juu tafsiri ya Taifa ni jamii ya watu wanaoishi katika Nchi moja na wanaounganika kutokana na matukio ya kihistoria,mfumo wa uchumi na utamaduni chini ya serikali moja.
  
Kauli ya kijana ni taifa la kesho kwa namna yoyote ile imepotoshwa kwa mujibu wa tafsiri ya kamusi kuhusu taifa.Nasema hivyo kwa sababu tunapozungumzia kesho kimantiki ni wakati ambao unasubiriwa,hata ukizungumza juu ya taifa huwezi kukwepa kutaja ardhi,mipaka,watu na serikali yao kama vielelezo vya taifa husika,sasa itakuwaje kijana ambaye yupo useme ni taifa la kesho,rejea tafsiri ya taifa na kesho

Tafsiri ya mtu kama kijenzi kimojawapo katika taifa haitugawi katika makundi ya umri wala kabila,awe mtoto,kijana,mzee,kilema ama vyovyote vile bado mtu atabaki kuwa ni sehemu ya Taifa tena la leo sio kesho

 Pasipo kujali dhana ya wakati uwe uliopita,uliopo au ujao bali kwa kuzingatia kipindi chote ambacho binadamu yupo hai.
  
Naamini huhitaji nguvu nyingi ili uweze kubaini upotoshwaji uliopo katika falsafa ya kijana ni taifa la kesho kwa kuwa inapoteza maana ya kijana na juhudi zake katika kufikiri,kubuni na kuthubutu kutenda.
  
Kimsingi falsafa hii ina walakini katika kuichanganua na kuelewa kusudio la mwanzilishi wa falsafa hii kwa kuwa watu wengi katika mtazamo wao mara wasikiopo neno kijana,humaanisha ni mtu mwenye umri wa miaka 18 hadi 40 sasa mtu huyo atakuwaje taifa la kesho wakati yupo leo

Binadamu siku zote tunapaswa kuwa makini katika fikra zetu na kauli tuzitoazo kwani uzoefu unaonyesha kuwa ndizo zinazozaa matendo yetu.

Lakini ni muhimu zaidi kusoma matendo yetu na kuyaelewa kwani matendo tuyatendayo ndiyo hasa tabia zetu.

Natambua pasipo shaka utofauti uliopo kutoka binadamu mmoja na mwingine katika jamii zetu,juu ya uwezo wa kufikiri na kuchambua mambo kutokana na sababu za kibailojia.
 
Hivyo naamini kuwa wapo watu wenye mtazamo wa kuwaona vijana ni taifa la kesho,binafsi naona mtazamo huo ni potofu,asiye amini kauli na mtazamo wangu basi mlango upo wazi hivyo karibu katika mjadala ili kuweka mambo sawa.

 Kwa kutumia akili ya kawaida haitamuwia vigumu binadamu yeyote yule kuona,kushawishika na kukubali mchango wa vijana katika maendeleo na ustawi wa jamii katika taifa lolote lile.

 Kwa kuwa vijana ndio wajenzi wazuri wa taifa hata hoja kulingana na mazingira stahiki,na wao ndio wanaopaswa kufanya shughuli zote za kimaendeleo ambapoa wazee wanapaswa kuwa washauri na kuwaachia vijana nafasi ili waweze kulitumikia taifa lao
  
Ni wazi kuwa endapo vijana wakipewa nafasi ya kushiriki katika kuunda taifa na kushughulikia mambo ya kimaendeleo kama vile ulinzi na usalama,biashara ndogo ndogo na kubwa,udaktari,ukulima,masuala ya michezo,sheria na mengineyo taifa litapiga hatua zaidi kimaendeleo.

 Kwa misingi hiyo,falsafa ya kumwona kijana ni taifa la kesho itanapaswa kufa iwe yenyewe au kwa kuiua kwani bila shaka falsafa hiyo inapaswa kuwa ni taifa la wakati wa sasa wafanyapo kazi za kujenga taifa lao (Taifa la leo),hivyo itakuwa ni vigumu kuwahadaa vijana kusubiri taifa la kesho wakati wao wanaishi leo

Falsafa ya vijana ni taifa la kesho ina ukakasi sana kwa sababu inawejengea vijana tabia ya kusubiri katika kuchukua hatua juu ya maisha yao.Hivyo inawapa na kuwajengea matumaini ya kuwa wajinga na wanyonge sambamba na kuhimizwa kuwa na subira kwa vitu visivyokuwepo.
 
Ni wazi kuwa muda umefika wa kumwona kijana ni taifa la leo,sasa hii ndio inapaswa kuwa kauli au falsafa mbadala kuliko kuiendekeza falsafa ambayo haieleweki katika akili za watu

Katika karne hii ambapo maendeleo ya sayansi na teknolojia yamesambaa duniani kote vijana wanapaswa kushika madaraka mbalimbali katika taifa lao,ni jambo la aibu kumkuta mzee ambaye kimsingi anapaswa kuwa amestaafu bado yupo kazini,huu ni ubinafsi,uchoyo na ulafi.Inashangaza kuona wazee wakipunguza umri wa kuzaliwa na kuongeza umri wa kustaafu ili waendelee kung’ang’ania madaraka
  
Vijana tuamke tuseme ukweli dhidi ya wazee wetu,wang’atuke na watupishe ili nasi tutimize wajibu wetu,hakuna ulazima wowote wa wao kuendelea kuzeekea katika madaraka ili hali wana watoto ambao kimsingi wana elimu ,hali kufikiri,kubuni na kuumba vitu anuai,wazee pumzikeni kwani wajibu wenu tayari mmeutimiza ulio baki ni wetu vijana
  
     
        0755 33 50 51 au 0715 33 50 51 au 0784 33 50 51
 

KAPTENI LOWASSA UNAKUMBUKA SWALI LA KIJANA ARON SHERA

 
                                                        Edward Lowassa(Mb)
Na,Stephano Mango,songea
NIMEAMUA leo kuandika makala haya ili kuweka kumbukumbu sawa dhidi ya kauli tata zinazotolewa na Mbunge wa Monduli Kapteni Edward Lowassa mara kadhaa anapopata fursa ya kuzungumza jambo
 
Nimemsikia mara nyingi kiongozi huyu akitamka na kuwataadharisha viongozi wenzake hatari inayokaribia kutokea endapo vijana wataendelea kuachwa nguvu yao ikipotea bure bila kupewa ajila itakayoweza kuleta mabadiliko chanya kwa taifa letu
 
Hakuna ubishi kuwa taifa lolote duniani  haliweza kukua  na kuwa imara kiuchumi na kijamii bila makundi yote ya jamii kushirikishwa kikamilifu katika mapambano dhidi ya umasikini, ujinga na maradhi na hasa kundi kubwa la vijana.
   
Kwani katika ulimwengu huu wa sasa asilimia kubwa ni vijana, na ndio viongozi wa leo na kesho, na nguvu kazi yao inategemewa sana katika kuendeleza jamii zetu licha ya ukweli huo kufahamika, jambo hili linapuuzwa na kuwafanya vijana kukosa thamani kutokana na mambo  mengi yanayo wazunguka ambayo hupelekea kupoteza heshima, utu na nafasi yao katika jamii na Taifa kiujumla
 
Leo anapotokea kiongozi ambaye kimsindi ndio sehemu ya kuasisijambo hilo kwa vijana kupoteza heshima yao na kutoa kauli tata kuhusu ajira kwa vijana,natafakari kwa umakini ili kuweza kuona agenda iliyopo nyuma ya panzia na anayezungumzia hoja hiyo na kubaini usafi wake
 
Na kwasasa nimeamua kuanza na tendo  lililotokea mwishoni mwa mwezi septemba 2007 wakati aliyekuwa Waziri Mkuu Edward Ngoyai Lowassa alipoenda mkoani Mwanza  kwa ziara ya kikazi
 
Ziara hiyo ilikuwa ni muendelezo wa kile kilicho tafsiriwa na watu wengi kuwa ni kwenda kuifafanua na kutangaza uzuri wa bajeti ya serikali kwa mwaka wa fedha wa 2007 na 2008 kwa wananchi.
 
Katika ziara hiyo,Lowassa kamwe hatasahau alipo kumbwa na vituko ikiwemo kushuhudia  majibu ya uongo kutoka kwa aliyekuwa Waziri wa Miundo Mbinu Andrwe Chenge kuhusu kivuko kibovu kilichopo kisiwa cha Ukelewe.
 
Bila aibu wala uwoga Chenge alilazimika kuanzisha malumbano na wananchi waliokuwa wakipinga kauli yake mbele ya  Mbunge wa jimbo hilo wakati huo Getrude Mongela,huku Chenge akiendelea kutetea jibu lake la uongo kwa madai kuwa kivuko kina fanya kazi vizuri
 
Jambo ambalo dhahiri lilikuwa ni utovu wa nidhamu mbele ya Waziri Mkuu,ndipo mbunge wa jimbo husika Getrude Mongella alipo lazimika kuweka mambo sawa kwa kupinga kauli ya Chenge waziwazi na kuacha siasa za kulindana huku akiwaunga mkono wapiga kura wake kwa kusema ukweli.
Hali hiyo ilimfanya Kapteni Lowassa aende eneo husika akajionee hali halisi,akiwa kivukoni almanusula azame pale mashine(Ingine) ya kivuko ilipozima ghafla mbele yake ndipo alipo amuru kivuko hicho kifanyiwe matengenezo ya haraka.
 
Akiwa katika kisiwa hicho cha Ukelewe Kapteni Lowassa aliulizwa swali na kijana Aron Wambura Shera,mwanafunzi wa kidato cha kwanza katika shule ya sekondari ya Pius Msekwa ambapo kijana Aron alimuuliza Lowassa  akiwa Waziri Mkuu wakati huo,ninanukuu”Mheshimiwa Waziri Mkuu tumekuwa tukikusikia kupitia vyombo vya habari,wewe pamoja na wasaidizi wako mkituhimizi tusome kwa bidii na maarifa ili kusudi tuje kuwa viongozi wa taifa la kesho, lakini mbona hatuoni hayo katika matendo yenu?
 
Alihoji uhalali wa viongozi wengi kupewa nyadhifa zaidi ya moja wakati kuna wasomi wengi vijana ambao wangeweza kushika nyadhifa hizo huku vijana wengi wakiwa wameachwa wakizubaa mitaani.
 
Aron akijithibitishia kauli yake alitoa mfano wa aliyekuwa Mkuu wa mkoa wa Mwanza Alex Mselekela ambaye pia ni mbunge wa Tabora kaskazini na kuhoji mtu huyo anawezaje kufanya kazi zote mbili kikamilifu?
 
Kapteni Lowassa  hakujibu swali hilo bila sababu za msingi ila alisema atarudi kujibu swali hilo siku nyingine bila kuitaja  siku husika ambapo staili aliyoitumia Kapteni Lowassa kukwepa swali lenye mantiki liliwashangaza wanafunzi wengi waliokuwepo katika eneo hilo,
 
Toka siku hiyo vijana walikatishwa tamaa na Kapteni Lowassa kwa kuwa walitegemea watapewa majibu mazuri,hii ni kutokana na uwezo wa Kapteni Lowassa kujibu maswali kwa umahiri mkubwa wakati huo akiwa Waziri Mkuu
 
Hadi leo tumetimiza miaka minne Kapteni Lowassa ameshindwa kujibu swali la kijana Aron ambalo liliulizwa kwa niaba ya vijana wa Tanzania kwani swali hilo linaeleza hisia halisi za vijana wa Tanzania na uwepo wa mashaka yao lukuki dhidi ya watawala wao
 
Swali lilikuwa wazi kabisa, kwanza linatoa ujumbe kwa watawala wetu kuwa hawatendi sawa na wanachokisema ni uthibitisho kuwa watawala wanaamini wasichokijua na kudharau wanachokijua .
 
Pili inaonyesha kuwa viongozi hawafanani na kile wanachodai kuwa wanatutumikia ingawa ukweli utabaki palepale kuwa viongozi wengi hutumikia matumbo yao huku wakitulaghai kwa maneno ya kinafiki kama vile uchumi unapaa huku umasikini ukionekana dhahiri kukithiri kwa watanzania wengi.
 
Tatu huo ni uthibitisho wa kukua  kwa kasi kwa fikra za kimapinduzi miongoni mwa vijana ambao Lowassa aliwakatisha tama toka mwaka 2007 ambapo leo tunashangaa anawazungumzia hadharani bila kukumbuka swali aliloulizwa na kijana Aron
 
Ni wazi sasa vijana wanathubutu kuhoji,kueleza mawazo yao na kuwabana viongozi kuhusu matendo yao machafu wayafanyayo wakiwa madarakani,ambayo kimsingi yana haribu mustakabali wa kizazi kilichopo na kijacho.
 
Vijana wamechoshwa na mtazamo wa kuwaona wao kuwa ni viongozi wa taifa la kesho huku leo wakikosa malezi stahiki na maandalizi mazuri katika kuchukua majukumu yao leo na hiyo kesho.
 
Kutokana na viongozi wengi kuwa na  fikra za ulafi wa mali za umma huku watanzania wengi wakiteseka na kushuhudiwa na vijana ambao ndio kundi muhimu na ni nguvu kazi ya taifa lolote lile duniani vijana wameamua kuchukua hatua wao wenyewe
 
Vijana wameamua kupaza sauti zao hasa pale nafasi inapojitokeza kwani wamekandamizwa kwa muda mrefu ambapo kumewafanya waweza kuthubutu  kutoa maoni yao waziwazi bila hofu kutokana na uhalisia na ugumu wa maisha wanaouona kwa wazazi wao na hivyo kujiandaa katika kuonyesha njia stahiki itakayo wasaidia kupata maisha yenye neema huko mbele
 
 Hivyo wanajua fika kuwa hali ngumu ya maisha inasababishwa na viongozi walafi ambao wanakula bila kunawa kwa kuingia mikataba mibovu ,kufanya ufisadi na ubadhilifu wa mali za umma bila huruma na kutuacha tukiwa masikini huku  wakifirisi nchi na kwenda kuwekeza nje ya nchi sambamba na kujirundikia vyeo lukuki ili kulinda maslahi yao
 
Vijana wakiwa katika fikra za mapambazuko na kutafuta mwanga stahiki katika maisha yao wanathubutu kuhoji uhalali wa viongozi kujirundikia vyeo kwa mara moja na wanapiga hatua kwa kutaka mafisadi na wabadhilifu wachukuliwe hatua na sio kuchukua nafasi ya kuwatetea
 
Hebu rejea maandamano ya wanafunzi yaliofanyika Agosti mosi mwaka 2007 yenye lengo la kupinga ongezeko jipya la nauli ya sh 50  na kuwa sh 100  kwa usafiri wa mabasi maarufu kama daladala kwa wanafunzi jijini Dar Es Salaam
 
Katika hali ya kimapinduzi na ukakamavu vijana walithubutu kubeba mabango yenye ujumbe mbalimbali wenye maana pana sana,bango moja lilisomeka “Mh JK utawala umekushinda?tulipe sh 100 kwa kipi mlichoboresha? Kiama chenu 2010, bango hilo halikuishia hapo liliendelea kusomeka”wafilisiwe chege ,lowaza , mkaapa kalamaagi na yona”na tuletewe  mabasi ya shule.
 
Kauli ya vijana ni ishara ya uwepo wa kiu kali miongoni mwa vijana wenyewe dhidi ya kusambaratisha mtandao wa viongozi mafisadi nchini ambao kimsingi ndio chanzo ulafi wa madaraka na kurundikiana vyeo ili kulindana katika maslahi ya kifisadi, ambapo watu wengi huishi katika maisha magumu na yanayozidi kuwavujisha jasho watanzania wengi.
  
Ni wazi kuwa hiki ni kizazi ambacho kimeanza kutambua wajibu wake kwa jamii,ni kizazi kinachoandaliwa katika mazingira ya hasira dhidi ya serikali hii kutokana na kudharauliwa pale wanapodai haki zao.
 
Kamwe vijana wasipuuzwe kupewa haki zao, hakika sio busara kuomba haki,hivyo haki inapaswa kudaiwa waziwazi na yoyote anayefinyanga haki za watu ni adui mkubwa,ni wazi kuwa maneno yaliyo andikwa kwenye mabango yaliyobebwa  na wanafunzi hao yasipuuzwe kwani ujumbe wao umefika ingawa leo vijana tunamshangaa Kapteni Lowassa baada ya kuachia ngazi ya Uwaziri Mkuu anajitokeza kuwatetea vijana
 
Vijana wanajifunza kufikiri kisayansi na kujenga hoja zenye mantiki na zenye ushawishi mkubwa kwa jamii,hivyo majibu sahihi yanahitajika katika kukidhi hamu na matakwa yao kwa manufaa ya nchi yetu.
 
Wanapothubutu kuwahoji watawala wana haki ya kupewa majibu yenye mantiki kwa wakati husika kwani kutokutoa majibu stahiki ni kujiaibisha mbele ya macho ya jamii na kutengeneza mshangao hasa wakati huu ambapo utetezi wa vijana unapotolewa na mtu aliyeshindwa kuandaa mfumo mzuri wa maisha ya vijana nchini alipokuwa kwenye madaraka makubwa kama ya Uwaziri Mkuu
  
 Hivyo Kapteni Lowassa hakuwa na sababu ya kukwepa swali aliloulizwa na kijana Aron Shera kwani swali hilo ni la msingi sana kwa mustakabali wa maisha ya vijana ambao leo kwa unafiki mkubwa anajidai kuwatetea katika suala la ajira
 
Lowassa wakati huo alipaswa kutoa majibu ya kina bila kumung’unya maneno kwani swali hilo halikuhitaji takwimu wala utafiti katika kujibu,sasa ilikuwaje Kapteni Lowassa ashindwe kuwa na jibu hadi aseme angerudi kujibu swali hilo kwa wakati mwingine.
 
Vijana hatutaki kuzubaishwa kwa majibu yenye utata kwa kuwa Kapteni Lowassa alishindwa kutupa jibu hadi alipojiudhuru ambapo bila kificho alijifedhehesha mwenyewe mbele ya vijana kwa kutotimiza wajibu na ahadi yake.
 
Akiwa madarakani Kapteni Lowassa alikumbushwa kulijibu swali la kijana Aron na wanaharakati mbalimbali wa masuala ya vijana nikiwemo mimi lakini aliupuuza ushauri wetu na kutuona tuliokuwa tunamkumbusha tumepungukiwa akili
 
Leo bila kificho tunamtaka ajibu swali aliloulizwa,baada ya hapo atuambie kwanini alishindwa kuweka mikakati stahiki na inayotekelezeka ya kutoa ajira kwa vijana wengi katika sekta binafsi na za umma alipokuwa Waziri kwa mara ya kwanza hadi pale alipokuwa Waziri Mkuu
 
Kwanini leo anajitokeza hadharani kuzungumzia suala la ajira kwa vijana akiwa kwenye madaraka ya Ubunge na katika hali ya uchafu anaodaiwa kuwa nao baada ya kubainishwa kashfa kadhaa ambazo anahusika nazo
 
Vijana tunajitambua kamwe hatuko tayari kuwa muhuri wa watenda dhambi kwani tulipothubutu kueleza mawazo yetu tulipuuzwa na kuendelea kushushwa heshima katika jamii na viongozi wetu leo tunapata tabuu kweli kuamini kuwa wanachokisema ndicho wanachomaanisha ikiwezekana watupishe nasi tushike hatamu katika kuwavusha miaka mingine hamsini baada ya uhuru
 
Mwandishi wa Makala haya
Anapatikana simu 0755-335051