About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Monday, April 30, 2012

WANACHAMA WA SACCOS YA WALIMU TUNDURU WALIDHIA ONGEZEKO LA MAKATO

Na Steven Augustino, Tunduru
WAJUMBE wa Mkutano mkuu wa chama cha Ushirika cha akiba na  Mikopo cha Walimu wa Wilaya ya Tunduru kimeridhia kuongeza makato yao na kufikia Shilingi 30,000 kutoka Shilingi 15,000 walizo kuwa wakikatwa awali zikiwa ni juhudi za kutunisha mfuko  kwa kutumia uwezo wa ndani.
Sambamba na kuthibitishwa kwa maapendekezo hayo wajumbe hao walipitisha bajeti ya mapato na matumizi ya shilingi Milioni 66,819,220 na kutumia jumla ya Shilingi 45,857,840 katika mwaka wa
fedha wa 2012 kukiwa na ongezeko la asilimia 78 % ikilinganishwa na bajeti ya shilingi milioni 52,666,000.  zilizotumika mwaka uliopita wa mwaka 2011.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo iliyotolewa na Kaimu meneja wa  chama hicho Mwl.Hassan Isaya alisema kuwa kati ya Fedha hizo  shilingi 36,675,000 zinatarajiwa kukusanywa kutoka katika vyanzo vya ndani , misaada na Ruzuku kutoka kwa wahisani wamepanga kuingiza jumla ya shilingi 800,000, na Tshs 27,851,220 zitatokana na faida ya mkopo wa CRDB.
Katika taarifa hiyo pia Mwl. Isaya  alieleza kuwa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2011/2012 chama hicho kiliweza  kukopesha jumla ya shilingi Milioni 95,970,325  kwa wanachama wake
 
Mwl. Juma Ado akisoma taarifa zilizotokana na mrejesho wa mikutano mbalimbali alidai kuwa uzoefu unaonesha kuwa pamoja na kuwepo kwa upungufu wa wanchama katika chama hicho pia udogo wa makato ya Tsh 15,000 wanayo katwa wanachama wake ni kikwazo kingine kinacho kwamisha
maendeleo ndani ya chama chao.
Aidha Mwl ,Ado katika taarifa hiyo alitolea mfano hatua za maendeleo zilizopigwa na vyama vya kuweka na kukopa vya UTWANGO SACCOS iliyopo katika Mkoa mpya wa Njombe na NEWALA SACCOS  Mkoani
Mtwara  ambazo zimemudu kujenga vitega uchumi vya kujenga  Nyumba  za kulala wageni kupitia mfumo wa  mbinu za uhamasishaji na kupeana majukumu ili miradi hiyo iwe vyanzo mbadala
vya kutunisha .
Pamoja na kutolewa kwa mapendekezo hayo wito ukatolewa kwa Viongozi wa chama hicho kuongeza juhudi za utoaji wa elimu kwa wanachama wapya pamoja na kumpelekea salamu mwajiri wao kuwa siku atakayo chelewesha makato yao kupeleka katika chama hicho wapo tayari kufanya maandamano
zikiwa ni juhudi za kuongeza mapato ya ndani ili kujiletea maendeleo.
 
Awali akifungua mkutano huo Mkuu wa 12 wa mwaka wa wanachama wa umoja huo uliofanyika kwenye ukumbi wa Klasta, Afisa elimu ya Shule za Msingi Wilayani humo Mwl. Rashid Mandoa alitumia nafasi hiyo kuwahimiza wanachama hao kukopa kwa busara na kulipa kwa busara mikopo hiyo.
Wakitoa nasaha kwa nyakati tofauti katika mkutano huo Afisa Ushirika wa Wilaya hiyo Jalia Msangi na Katibu wa chama cha Walimu Wilaya ya Tunduru Mwl. Lazaro Saulo waliwahimiza wanachama hao kuwa waumini wa chama hicho kwa kukubali kwa hiari zao kuongeza makato kulingana na malengo ya kila mwanachama na kujiletea maendeleo kulingana na mahitaji yao.

Walisema kulingana na taratibu na sheria zinazosimamia ushirika pamoja na kuweka utaratibu wa kujiunga na chama husika pamoja na kuwekwa kwa mikakati yake pia kuwe na utaratibu wa kuwaruhusu wanachama kuchangia fedha kulingana na mahitahi tu.
Akifunga Mkutano huo Mwenyekiti wa umoja huo Mwl. Hassan Nakoma pamoja na kuwahimiza wanachama hao kuendelea kuwashawishi wanachama wapya kujiunga na umoja huo pia aliwataarifu wanachama hao kuwa ujenzi wa Ofisi ya chama hicho umepangwa kupitia uwezo wao wa ndani baada ya mfadhiri wao Daimu Mpakate kushindwa kutimiza masherti ya umoja huo
Mwisho

Saturday, April 28, 2012

WAWILI WAFA PAPO HAPO NA WATATU WAJERUHIWA VIBAYA

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma Michael Kamuhanda
Na Gideon Mwakanosya, Songea
WATU  wawili wamefariki dunia na wengine watatu akiwemo dereva wa gari hilo  wamejeruhiwa vibaya mkoani Ruvuma baada ya kugongwa na gari katika  eneo la Mahenge katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea baadaya ya kugongwa na gari la Jeshi la wananchi (JWTZ)  la Makao makuu ya brigedi Chandamali
Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma Michael  kamuhanda amesema kuwa tukio hilo limetokea  majira ya saaa mbili na nusu asubuhi huko kwenye barabara ya Songea na Namtumbo ambapo aliwataja waliokufa kuwa ni Stumai Moyo (20) na Tabia Bilali (23) wote wakazi wa eneo la Mahenge wa Songea mjini na walio jeruhiwa vibaya ni Amina Moyo (2) na Issa Moyo (65) wote wakazi wa Mahenge ambao baada ya kutokea ajali hiyo walikimbizwa katika Hospitali ya mkoa ambako wamelazwa
 Alifafanua zaidi  kuwa gari hiyo Landlover Discova yenye namba za usajili 1513 JW 97  iliyosababisha ajali na kuuwa watu wawili papohapo na wengine wawili kujeruhiwa vibaya.
 Alieleza zaidi kuwa gari hiyo iliyokuwa ikiendeshwa na  MT 97812 SGT Kelvin Muhagama ilikuwa ikitoka Makao makuu ya Brigedi Chandamali na kuelekea Songea mjini  
 Kamanda Kamuhanda alibainisha zaidi kuwa chanzo cha ajari hiyo ni mwendo kasi ambao ilimsababisha dereva wa gari hilo kushindwa kumudu usukani
Naye Mganga mfawidhi wa Hospitali ya mkoa songea  Dr. Mathayo Chanangula amethibitisha kupokea maiti za watu wawili ambazo kwa sasa zimehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali hiyo  na majeruhi  watatu ambao wawili kati yao wamelazwa kwenye wodi za majeruhi na majeruhi mmoja ambaye ni mtoto wa umri wa mika 2 Amina Moyo amekimbizwa katika Hospitali ya Mision ya Peramiho kwa matibabu zaidi baada ya Hospitali hiyo kukosa mashine ya Ex –ray kwani imeonekana kuwa Amina ameumia kichwani ambako kunahitaji kupata vipimo vya Ex –ray ambapo kwa sasa hivi huduma hiyo inapatikana katika Hospitali ya Mision ya Peramiho
Dr. Chanangula alifafanua zaidi kuwa kwa muda mrefu hospitali ya mkoa songea haina kabisa huduma ya Ex –ray tangu mashine hiyo ilipo haribika na kwamba kwa hivi sasa wanasubiri mafundi kutoka ufiripino waje kitengeneza jambo ambalo limeonekana kuwa kero kuwa kwa wakazi wa songea ambao wamefika kupatiwa huduma hiyo lakini wamekuwa wakielekezwa kwenda Hospitali ya Mision ya Peramiho ambayo iko umbali wa kilometa 25 toka Songea mjini
 Mwisho.  

WAKULIMA WA KOROSHO WAGOMA KUPOKE MALIPO NUSU NUSU YA FEDHA ZAO

MKUU WA WILAYA YA TUNDURU JUMA MADAHA
Na Steven Augustino ,Tunduru

BAADHI ya wakulima wa korosho katika vyama vya msingi vya wakulima wa zao hilo wamegoma kupokea fedha za malipo yao huku wakidai kuto kuwa na imani na maelekezo yanayotolewa na viongozi wao.

Mgomo huo umefuatia kuwepo kwa maelekezo kuwa mkulima anayedai Shilingi 1200 kwa malipo ya korosho hizo atatakiwa kupokea mkononi Shilingi 850  na makulima anayedai Shilingi 350 atatakiwa kupokea Shilingi 200 huku kukiwa na maelekezo kuwa fedha nyingine watalipwa baada ya kuwasili kwa fedha zingine.

Wakiongea kwa nyakati tofauti miongoni mwa wakulima hao Mahamudu Ponera wa chama cha Msingi Nakayaya mashariki na Maghreth Mingwe walisema kuwa kitendo cha viongozu hao kuyumbisha malipo hayo kinalenga kuendelea kuichafulia sifa Serikali.

Walisema msimamo wao wa kukataa kupokea fedha hizo unatokana na wakulima kuelezwa kuwa baada ya kupokea fedha hizo watatakiwa kuacha Stakabadhi za malipo hayo na kubakia wakiwa hawana vielelezo vyovyote vinavyo onesha kuwepo kwa madai mengine katika vyama hivyo.

Alipo takiwa kuzungumzia hali hiyo Meneja wa Chama Kikuu cha wakulima wa wa Wilaya ya Tunduru  Iman Kalembo alithibitisha kuwepo kwa hali hiyo na kwamba msimamo wakutoa malipo hayo umetokana na fedha zilizofika kuwa ni kidogo hivyo wao hawakuona mkulima wa kumuacha wakati wa malipo hayo na kusisitiza kuwa fedha zikifika wakulima wote watakamilishiwa malipo yao.

Nae Mkuu wa Wilaya ya Tunduru Juma Madaha alipotakiwa kuzungumzia kero hiyo alidai kuwa hakubaliani na utekelezaji wa zoezi hilo na kuongeza kuwa msimamo wa Serikali ni kulipa fedha zote na siyo kidogo kidogo na kwamba kama kuna kosa lilifanyika na viongozi hao ni uzembe wa viongozi wenyewe.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na Afisa Ushirika wa Wilaya ya Tunduru Msangi alisema kuwa malipo hayo yanatokana na Benki kutoa Tsh. 2,587,506,900 zimepangwa kughalimia malipo ya Kilo 1200 tu kati ya Kilo  7,367,689 zilizopokelewa katika maghala kati ya Kilo
7,570,000 zilizo zalishwa na akulima hao katika msimu wa mwaka 2011/2012.

 Msangi aliendelea kueleza kuwa mchanganuao wa malipo hayo unaonesha kuwa kiasi kingi ne cha Shilingi 119,759,340 zitalipwa awamu ya pili na kwamba hali hiyo inatokana na taratibu za malipo hayo kuchelewa kupelekwa Benki.

Alisema fedha hizo zinatokana na malipo ya kilo 560,101 ambapo kati yake kilo 53,347 zenye thamani ya Shilingi 64,016,400 ni korosho za daraja la kwanza na shilingi 55,742,940  zinatokana na kilo 506,754 za daraja la pili.

Mwisho

Thursday, April 26, 2012

SHEREHE ZA UZINDUZI WA SONGEA GLOBAL NETWORK ZILIVYOFANA KATIKA UKUMBI WA AGOPAL

Katibu Mtendaji wa Songea Global Network John Kasembo akizungumza na mmoja wa wanachama wa mtandao huo

Kushoto ni Mtaalamu na mmiliki wa Kampuni ya kufunga Aluminium Songea Wailes Sebastian akiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Elimark Eng.Co. Ltd Emanuel Nehemia Chapa

Mwenyekiti wa Songea Global Network Sakina Jamal akiwa na Mhasibu wa Mtandao huo Rehema Ayub wakati wa halfa ya uzinduzi wa mtandao huo
Miongoni mwa wanachama wa mtandao huo

Miongoni mwa wanachama wa Songea Global Network ambao walikuwa wanakamati wa chakula wakisubiri kuhudumia msosi

Mwenyekiti wa Songea Global Network Sakina Jamal akifungua mziki na mmoja wa wanachama wa Songea Global Network


Sasa ni kusaka lumba kwenda mbele na yeyote anayetaka kucheza kiduku ruksa

Mpaka kielewekeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeee

Mtandao wa Songea Global Network uwe chachu ya maendeleo
NA STEPHANO MANGO,SONGEA
WAHENGA walishanasihi kwamba, “Moyo usiokuwa na shukrani hukausha mema yote.” Hii inamaanisha kuwa tutakuwa wezi wa fadhila  kama hatutamshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa fadhili, rehema na mapendo kwa kutujalia sote uhai na afya na kutujalia nafasi hii adimu na adhimu ya kuandika na kusoma makala haya.
Nawashukuru wasomaji wote wa gazeti hili makini kwa kuendelea kulisoma na kutoa maoni yenu kwa mwandishi binafsi na wakati mwingine kwa viongozi wa Bodi ya Uhariri ili kuweza kuboresha kazi husika kwa lengo la kukidhi mahitaji ya wasomaji
Aprili 21 mwaka huu, nilialikwa kuhudhuria uzinduzi wa Mtandao wa Songea Global Network katika viwanja vya Hotel ya Agopal ambapo mgeni rasmi katika uzinduzi huo alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu ambaye aliwakilishwa na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma Seligius Ngahi.
Tukio hilo la kihistoria la uzinduzi wa mtandao lilihudhuriwa na watu wa kada mbalimbali lilikuwa ni mwanzo mpya wa wanachama wake kuifikia ndoto ya kuanzishwa kwake kwani walitaka, wakatakana na sasa hawana budi kuendeleza mipango waliojiwekea ili kuweza kuleta mafanikio waliokusudia toka awali wakati wanapanda mbegu ya kuanzisha mtandao huo.
Mtandao huo kama vilivyo vikundi vingine au chama chochote, una viongozi wake wakuu kwa maana ya Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, Katibu Mtendaji, Mhasibu na Kamati ya Utendaji, ambao watahakikisha malengo ya kuanzishwa kwa mtandao yanafikiwa kwa kushirikiana na wanachama wa mtandao huo.
Akizungumza katika uzinduzi huo Mwenyekiti wa Songea Global Network (SGN) Sakina Jamal alisema kuwa malengo la kuanzisha mtandao huo ni kwanza, kusaidiana na kujaliana kwa shida mbalimbali mfano. Misiba, dharura.shida ni sehemu ya maisha ya binadamu.
Jamal alisema kuwa pili, kufahamiana na kupanua mtandao katika dunia hii ya utadawazi ambapo watu wanatafuta kuungana na kushirikiana katika maisha ya kila siku ,kwasababu ujifungia ni kuukumbatia umaskini wa mawazo na fikra.
Alisema tatu, kuwezeshana na kujengana kimawazo, kiushauri na kiuchumi, nne, kufunguliana  fursa za kusaidiana kadri ya utaalamu na kazi ya kila mmoja na tano, baadaye kuwa na SACCOS itakayotuwezesha kiuchumi: kuweka akiba, kukopa.
Alieleza zaidi kuwa hadi tunazindua rasmi mtandao unajumla ya wanachama 20 wakiwamo watu wa fani mbalimbali: wajenzi, mainjinia, mafundi, wahasibu, wanafunzi,madaktari, wajasiriamali, wafanyakazi wengine wa serikali.
Alisema ni mseto ulioiva wa wanachama wenye nia ya kushikamana na kutimiza ndoto ya mafanikio, udugu, ushirikiano na utajiri kwani tumedhamiria kuwa mbegu imara itakayoweza kutoa matunda stahiki katika siku za usoni kama tulivyojiwekea malengo, pia tunawakaribisha wanachama wapya kujiunga katika mtandao ili uwe na nguvu kubwa ,hivyo kwa yoyote yule anayetaka na kukubaliana na malengo tuliyojiwekea tunamkaribisha.
Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Songea Global Network John Kasembo akielezea historia ya kuanzishwa kwa mtandao huo wakati wa hafla ya uzinduzi huo alisema kuwa ,mtandao ulianza kama wazo la kukutana na kufanya hafla ya kuuaga mwaka 2011.
Kasembo alisema kuwa baada ya kukaa tukasema hapana, tulitajirishe wazo letu kwa kuanzisha mtandao utakao tuunganisha wote hata baada ya sherehe kama umoja wenye nia ya kusaidiana wakati wa shida na raha, kushauriana na kujengeana uwezo ili sote tufanikiwe.
Alisema baada ya majadiliano mapana na ya kina, tulikubaliana sote tuanzishe mtandao au umoja huo tukaupa jina la Songea Global Network (SGN) ambapo leo ndio siku tuliyokubaliana ya kupanda mbegu imara na safi ya mtandao huu ili umee na kuwa faida kwetu sisi wanachama na kuutangaza mkoa wetu wa Ruvuma kupitia mtandao wetu huu.
Alifafanua kuwa tulichagua jina hili SGN kwa sababu lina dhima ya kuunganisha watu wa kada mbalimbali bila kubagua umri, kazi, kabila, jinsia, rangi, dini wala itikadi. Anayekubali malengo yetu na kuwajibika kuchangia dira yetu, huyo ni mwanachama mzuri kwetu.
Alieleza zaidi kuwa leo tunavyopanda rasmi mbegu ya mtandao wetu (SGN), tunatumia fursa hii kukumbushana wanamtandao masharti ya kufanikiwa ili tuendelee mbele zaidi kufikia malengo na ndoto yetu ni kujitoa kweli,kupenda kweli mtandao,kuwa na ndoto na kutoa michango ya dhati bila kuchoka
Alisema kuwa ni kweli kuja pamoja ni mwanzo. Kufanya kazi pamoja ni umoja. Kudumu katika umoja ni maendeleo. Kuunganisha vipaji vyetu ni kuwa timu moja. Hatimaye kustahimili pamoja ni ushindi wa mtandao wetu huu.
Alieleza zaidi kuwa wanachama tukikaribisha upendo wa kweli tutafanikiwa katika malengo yetu na kutajirisha mtandao wetu kwa maendeleo ya mkoa wa Ruvuma, hivyo tunawajibika kutafakari na kuchukue hatua.
Alisema inapendeza, inakubalika, inawezekana na inahitajika kuwa na mtandao imara usiokatika network na kufanikiwa kweli. Ni kweli wahenga wa Ghana walishatuasa kwa methali yao kuwa, “Unaweza kumlaumu mtu kwa kukuangusha chini lakini ujilaumu mwenyewe kwa kukataa kunyanyuka.”
“Naomba wanamtandao tulioamua kuanzisha kwa hiari mtandao huu tusikalie kumlaumu mtu au kujilaumu wenyewe na badala yake tudhamirie na kuwa na bidii ya kunyanyuka leo na kuendeleza ndoto na mtandao wetu. Bila shaka linaloonekana haliwezekani litawezekana, milima isiyokweeka itakweeka na miti isiyopandika itapandika”alisema Kasembo.
Alisema kuwa tumuombe Mungu ili idumu, iote na ifanikiwe mbegu ya SGN ambapo sote tuchangie maendeleo yetu na ya taifa letu la Tanzania. Karibuni sote tufurahie jambo hili adhimu na tuchangie kila mmoja kwa nafasi na uwezo wake, kiushauri na kirasilimali aliyonayo kwa  mafanikio ya SGN.
Alisema kuwa wanachama tushikane mikono tuanze safari yetu kwa hatua ya kwanza leo, kwani hata Waswahili wanasema, “Safari ya maili elfu huanzia na hatua moja.” Na hakika ni kweli.  Tumethubutu kubuni na kuanzisha mtandao, tumeweza kuanzisha mtandao huu na sasa tunanuia kusonga mbele na mtandao tuliouanzisha.
Naye mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu  katika hotuba yake iliyosomwa na Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Ruvuma Seligius Ngahi alisema leo nashuhudia ndoto ikizaa jambo la uhalisia nayo ni Songea Global Network, nawapongeza sana kwa ndoto yenu, juhudi, nia na dhamira ya kuanzisha na kuendeleza mtandao wenu huu wenye malengo mliyojipangia ninyi wenyewe
Mwambungu alisema kuwa Chama au kikundi chochote cha watu hujengwa na mambo makuu matatu. Kwanza ni mahudhurio ya watu au wanachama, katiba na michango ya wanachama (rasilimali, ushauri, muda, fedha na nguvu).
Alifafanua kuwa kama mwanzo wa chama chenu napenda niwaombe tokea mwanzo kuwa kama mnanuia kweli ustawi, mafanikio na maendeleo ya mtandao wenu basi jibidisheni nyote kuhudhuria vikao bila kuchoka wala kudharau kwani mtu mmoja una thamani kwa mtandao huu.
Alisema tena jitahidini kuunda na kuwa na katiba imara itakayokuwa dira na mwongozo wa kufikia mafanikio ya malengo mliyojiwekea. Na Zaidi jalini na kujitoa sadaka nguvu, akili, utashi, rasilimali muda na michango yenu ya hali na mali katika kujenga, kukuza na kustawisha mtandao wenu. Haya kwenu ni ya msingi na ya kuzingatia kati ya mengi kama mnataka kuwa na mtandao imara na wenye nguvu.
“Nami najiunga rasmi katika mtandao pia naunga mkono jitihada mlizozianzisha kwa kutoa sh,300,000 ili ziwe chachu yaw engine kujitoa kwa lengo la kutimiza malengo ya kuanzishwa kwake”alisema Mwambungu
Alieleza zaidi kuwa natambua kuwa mtandao ili uendelee mbele kuwa wenye nguvu, wenye mafanikio na watu wengi inapaswa kuutangaza, kuulinda, kuukuza, kuustawisha, kujivunia na kuufurahia. Tumieni fursa hii kufanya yale yote mtakayoona yanausaidia mtandao wenu kustawi na zaidi epukeni yale yote yanaweza kuvunja na kudhoofisha mtandao kama ubinafsi, dharau, chuki, fitina na majungu. Haya ni sumu kwenu!
Alisema kuwa leo mmeitangazia Songea, Ruvuma, Tanzania na dunia kuwa mna ndoto kubwa ya mafanikio. Kwa kawaida kuanzisha kazi ni rahisi kuliko kuiendeleza na kuimalizia. Mmeanza kwa kishindo, sasa msirudi nyuma. Daima kwenda mbele kwa kasi na viwango ili ndoto yeni itimie. Inawezekana, timizeni wajibu wenu.
Hakika wanamtandao wamethubutu,kubuni na kuanzisha mtandao, wameweza kuanzisha mtandao huu na sasa wanahitaji kusonga mbele ili uweze kuwa msaada wa ushauri, msaada wa kiuwezeshaji na msaada wa rasilimali watu wenye upeo na ndoto kwa mkoa wetu wa Ruvuma
Kuzaa si kazi, kazi ni kulea. Leeni mtandao huu uwe taa ya kutoa giza la umasikini na uwe chumvi ya kuleta ladha kwa mafanikio yenu na mkoa wa Ruvuma. Kama wengine waliweza kwanini nyie mshindwe?Hapana, kataeni msamiati wa kushindwa na siku zote neno msamiati wa kwanza uwe ni USHINDI DAIMA. Heri na mafanikio kwenu na Hongereni sana.Nyie mbele sisi nyuma
Mwandish wa Makala
Anapatikana 0715-335051
www.stephanomango.blogspot.com



WAKULIMA WALALAMIKIA KUTOZWA USHURU WA MAZAO TOKA SHAMBANI



                             
MKUU WA WILAYA YA TUNDURU JUMA MADAHA
Na Augustino Chindiye, Tunduru


WAKATI wakulima wa mazao ya Chakula Wilayani Tunduru mkoani Ruvuma wakilalamikia
kutozwa ushuru mkubwa kupitia vizuizi vilivyo wekwa na Wakala aliyeshinda zabuni ya kukusanya ushuru wa mazao ameahidi kuto msaidia mtumishi yeyote atakaye bainika kukiuka maelekezo yake.

Pamoja na kuitolewa kwa kauli hiyo Meneja wa kampuni ya StetyBussiness inayo kusanya ushuru huo katika halmashauri ya Wilaya ya Tunduru Rashid Akbal aliwafananisha watumishi hao na mafisadi ambao wamekuwa wakiichafulia kasi ya Utendaji Serikali ya jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Kampuni yangu inafanya kazi kulingana na maelekezo tuliyosaini katika Mkataba na Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya Wilaya hiyo” alisema Akbal na akatumia nafasi hiyo kuwaomba wakulima watakao fanyiwa vitendo viovu na watumishi hao kutoa taarifa zenye ushahidi kwake ili waweze kuwawajibisha.


Akbal ambaye alikuwa akijibu swali la kwanini kampuni yake inatoza ushuru hadi wakulima wa kawaida wanaobeba kuanzia debe mbili aliendelea kueleza kuwa maelekezo yaliyotolewa kwa wafanyakazi wa
kampuni hiyo ni kutoza wafanyabiashara wanaonunua mazao ya wakulima tu na si kuwatoza hadi wakulima wanao rudisha mazao yao kutoka shambani.

Akizungumzia hali hiyo Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya hiyo Mary Ding`ohi mbali na kukiri kupokea malalamiko mengi juu ya tozo hizo alisema kuwa ofisi yake ina andaa utaratibu wa kumwita mzabuni huyo na kumpatia maelekezo upya zikiwa ni juhudi za kuondoa kero hiyo.


Alisema katika maelekezo ya awali mzabuni huyo alielekezwa kukusanya kiwango kisicho zidi asilimiaa 5% kutoka kwa wafanyabishara hao wa mazao ya Chakula na kwamba mkataba huo pia uliwaondoa katika tozo hiyo wakulima wanaorudisha mazao yao kutoka shambani baada ya kuyavuna.


Akizungumzia kero hiyo katibu wa Umoja wa Chama Cha wauzaji na wanunuzi wa mazao ya wakulima (WAMANATU) Wilayani Tunduru Athuman Milanzi alisema kuwa katika uchunguzi wao wamebaini kuwa kero hiyo inasababishwa na Mzabuni huyo kulazimisha kukusanya tozo hiyo kwa zaidi ya asilimia 5 iliyo kubaliwa katika mkataba wao.


Mwisho

Tuesday, April 24, 2012

SONGEA GLOBAL NETWORK YAZINDURIWA NA MKUU WA MKOA WA RUVUMA SAID MWAMBUNGU

HOTUBA YA UFUNGUZI WA SONGEA GLOBAL NETWORK (SGN) KWENYE UKUMBI WA AGOPAL – SONGEA TAREHE 21/04/2012.
Mh. Mwenyekiti,
Mh. Katibu
Mh. Mhasibu
Ndugu Wanamtandao,
Ndugu Wageni waalikwa,
Mabibi kwa Mabwana.

ASALAAM ALYEIKUM! TUMSIFU YESU KRISTO!

Kwanza, Nampenda nianze kwa Kumshukuru Mungu kwa Baraka na Neema zake alizotujalia na kuweza kutufikisha hapa kwa ajili ya kufanya tukio muhimu la uzinduzi wa mtandao wenu huku tukiwa na afya njema na furaha.

Pili, naomba niwashukuru sana kwa kunialika kuja kuungana nanyi katika siku hii muhimu ya kuzindua mtandao wenu (Songea Global Network). Mmenipa heshima na kunionyesha upendo kwa mwaliko wenu. Asanteni sana!

Tatu, naomba nitumie fursa hii kuwapongeza sana kwa ndoto yenu, juhudi, nia na dhamira ya kuanzisha na kuendeleza mtandao wenu huu wenye malengo mliyojipangia ninyi wenyewe. Leo kweli nashuhudia ndoto ikizaa jambo la uhalisia nayo ni Songea Global Network, hongereni sana!

Chama au kikundi chochote cha watu hujengwa na mambo makuu matatu. Kwanza ni mahudhurio ya watu au wanachama, katiba na michango ya wanachama (rasilimali, ushauri, muda, fedha na nguvu). Kama mwanzo wa chama chenu napenda niwaombe tokea mwanzo kuwa kama mnanuia kweli ustawi, mafanikio na maendeleo ya mtandao wenu basi jibidisheni nyote kuhudhuria vikao bila kuchoka wala kudharau kwani mtu mmoja una thamani kwa mtandao huu. Tena jitahidini kuunda na kuwa na katiba imara itakayokuwa dira na mwongozo wa kufikia mafanikio ya malengo mliyojiwekea. Na Zaidi jalini mtandao wenu na kujitoa sadaka nguvu, akili, utashi, rasilimali muda na michango yenu ya hali na mali katika kujenga, kukuza na kustawisha. Haya kwenu ni ya msingi na ya kuzingatia kati ya mengi kama mnataka kuwa na mtandao imara na wenye nguvu.

Mmeunda mtandao kwa malengo mliyoyataja kama kusaidiana, kufahamiana, kujengeana uwezo na kushauriana n.k. Mie natambua kuwa mtandao ili uendelee mbele kuwa wenye nguvu, wenye mafanikio na watu wengi inapaswa kuutangaza, kuulinda, kuukuza, kuustawisha, kujivunia na kuufurahia. Tumieni fursa hii kufanya yale yote mtakayoona yanausaidia mtandao wenu kustawi na zaidi epukeni yale yote yanaweza kuvunja na kudhoofisha mtandao kama ubinafsi, dharau, chuki, fitina na majungu. Haya ni sumu kwenu!

Ntatolea lugha ya picha ya mtandao wenu. Mfano mtandao wa simu wa Vodacom unawauunganisha watu wenye line za Vodacom na wengine. Promotion zikitoka zinawapata wote na mtandao ukikatika hasara ni kwa wote. Vivyo nanyi, muwe na nia ya kuleta faida ya wote na kuepa yanayowaletea hasara wote. Hili limo ndani ya uwezo wenu.

Leo mmeitangazia Songea, Ruvuma, Tanzania na dunia kuwa mna ndoto kubwa ya mafanikio. Kwa kawaida kuanzisha kazi ni rahisi kuliko kuiendeleza na kuimalizia. Mmeanza kwa kishindo, sasa msirudi nyuma. Daima kwenda mbele kwa kasi na viwango ili ndoto yeni itimie. Inawezekana, timizeni wajibu wenu.

Naomba tuendelee kuchangia mtandao huu sisi sote tuliopo ili uweze kuwa msaada wa ushauri, msaada wa kiuwezeshaji na msaada wa rasilimali watu wenye upeo na ndoto kwa mkoa wetu wa Ruvuma. Kufanikiwa kwa Songea Global Network ni kufanikiwa kwa mkoa wa Ruvuma. Katika maisha mafanikio yanapimwa kuanzia mtu mmoja mmoja. Kama kikundi endeleeni kuutanganza vyema mkoa wetu wa Ruvuma. Mti hauwezi kujifanya kinyago mpaka umechongwa. Basi chongeni vyema mtandao wenu ili uzae matunda mema na bora sana.

Mimi kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa natoa au Mkuu wa Mkoa ametoa kiasi cha Tsh 300, 000/= kuachangia umoja na mtandao huu wa wanasongea wenye nia njema ya kuwa kisima cha ushauri, uwezeshaji na watu wanaopenda kuitangaza Ruvuma kwa mafanikio katika yale wanayoyafanya. Naomba na wengine tuliopo hapa ambao hatujauchangia mtandao huu kila mmoja agusike na ajitolee hapa ili kuuchangia mtandao wetu kwani “Peke yetu tunafanya machache, pamoja tunafanya mengi,” alisema Hellen Keller, Mwanafasihi wa Marekani.

Mwisho, naomba niwatakie kila jema katika makuzi ya mtoto mliyemzaa leo Songea Global Network. Kuzaa si kazi, kazi ni kulea. Leeni mtandao huu uwe taa ya kutoa giza la umasikini na uwe chumvi ya kuleta ladha kwa mafanikio yenu na mkoa wa Ruvuma. Kama wengine waliweza kwanini nyie mshindwe?Hapana, kataeni msamiati wa kushindwa na siku zote neno msamiati wa kwanza uwe ni USHINDI DAIMA. Heri na mafanikio kwenu na Hongereni sana. Sasa natamka rasmi kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa Mhe. Said Mwambungu kuwa nimeuzindua rasmi mtandao wenu wa “SONGEA GLOBAL NETWORK.”

Mungu Ibariki Ruvuma,
Mungu Ibariki Songea Global Network
Asanteni kwa kunisikiliza.

RISALA YA WANAMTANDAO KWENYE UFUNGUZI WA SONGEA GLOBAL NETWORK (SGN) KWENYE UKUMBI WA AGOPAL – SONGEA TAREHE 21/04/2012.

Mh. Mgeni Rasmi,
Mh. Mwenyekiti,
Mh. Viongozi,
Ndugu Wanamtandao,
Ndugu Wageni waalikwa,
Mabibi kwa Mabwana.

HABARI ZA JIONI NYOTE!

Wahenga walishanasihi kwamba, “Moyo usiokuwa na shukrani hukausha mema yote.”  Tutakuwa wezi wa fadhila  kama hatutamshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa fadhili, rehema na mapendo kwa kutujalia sote uhai na afya na kutujalia nafasi hii adimu na adhimu ya kushiriki tukio hili la kihistoria uzinduzi wa mtandao wetu wa “SONGEA GLOBAL NETWORK.”

Tena, tusheheneze shukrani zetu nyingi kwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Mh. Said Thabit Mwambungu ambaye amebariki tukio hili liwepo kwa kumtuma mwakilishi wake Kaimu Afisa Tawala wa Mkoa wa Ruvuma ndugu… Seligius Ngahi …….kuja kuwa Mgeni wetu Rasmi. Naye akakubali kwa hiari na utayari. Asante sana ndugu kwa kukubali kuwa Mgeni Rasmi.

Hali kadhalika, tunawashukuru wale wote waliojitolea kufanikisha uanzishwaji wa mtandao huu. Wanamtandao wenyewe na wadau wageni waalikwa mabibi kwa mabwana. Asanteni sana. Tujipogeze pia wanamtandao kwa kufanikisha ndoto yetu leo walau ya kupanda mbegu ya Songea Global Network. Tulitaka na tukataka sana, tumefanikiwa sana leo kuanza rasmi safari yetu ya kuifisha ndoto yetu mbali.

Kila asubuhi Tanzania, swala huamka. Anajua kwamba ni lazima akimbie kwa kasi kuliko simba anayekimbia kwa kasi sana ama sivyo atauawa. Aidha, kila asubuhi simba huamka. Anajua kwamba ni lazima kumkimbiza swala anayekimbia polepole ama sivyo atakufa kwa njaa. Haijalishi kama wewe ni simba au swala…jua linapochomoza, ni vema kukimbia!
Nasi Wanamtandao wa kila kada tunaitwa leo, sasa na hapa tulipo tukimbie kwa kasi katika kuunganisha mtandao na kujiendeleza ama sivyo tutakufa kwa njaa au kuangamiza taifa letu!

Mhe, Mgeni Rasmi na Wageni waalikwa mabibi kwa mabwana,
Awali kabisa, Mtandao wetu ulianza kama wazo la kukutana na kufanya hafla ya kuuaga mwaka 2011. Lakini baada ya kukaa tukasema hapana, tulitajirishe wazo letu kwa kuanzisha mtandao utaotuunganisha wote hata baada ya sherehe kama umoja wenye nia ya kusaidiana wakati na shida na raha, kushauriana na kujengeana uwezo ili sote tufanikiwe. Baada ya majadiliano mapana na ya kina, tulikubaliana sote tuanzishe mtandao au umoja huo tukaupa jina la SONGEA GLOBAL NETWORK (SGN). Leo ndio siku tuliyokubaliana ya kupanda mbegu imara na safi ya mtandao huu ili umee na kuwa faida kwetu sisi wanachama na kuutangaza mkoa wetu wa Ruvuma kupitia mtandao wetu huu.

Tulichagua jina hili SGN kwa sababu na dhima ya kuunganisha watu wa kada mbalimbali bila kubagua umri, kazi, kabila, jinsia, rangi, dini wala itikadi. Anayekubali malengo yetu na kuwajibika kuchangia dira yetu, huyo ni mwanachama mzuri kwetu. Tunatumia fursa hii kuwaomba wanachama wengi wajiunge zaidi ili kuupa nguvu mtandao wetu. Tena hata wewe Mgeni Rasmi tunakuomba leo ujiandikishe kama mwanamtandao ili tuufanikishe mtandao wetu. Karibu sana!

Sisi wanamtandao tupo watu wa fani mbalimbali: wajenzi, mainjinia, mafundi, wahasibu, wanafunzi,madaktari, wajasiriamali, wafanyakazi wengine wa serikali, n.k. Ni mseto ulioiva wa wanachama wenye nia ya kushikamana na kutimiza ndoto ya mafanikio, udugu, ushirikiano na utajiri!

Mhe, Mgeni Rasmi na Wageni waalikwa mabibi kwa mabwana,
Tumeamua kuanzisha mtandao huu kwa MALENGO yafuatayo
Kwanza, kusaidiana na kujaliana kwa shida mbalimbali mfano. Misiba, dharura. Hata Bill Gates ana shida zake. Shida ni sehemu ya ubinadamu.
Pili, kufahamiana na kupanua mtandao katika dunia hii ya utadawazi ambapo watu wanatafuta kuungana na kushirikiana katika maisha ya kila siku. Kujifungia ni umaskini wa mawazo na fikra.
Tatu, kuwezeshana na kujengana kimawazo, kiushauri na kiuchumi.

Nne, kufunguliana  fursa za kusaidiana kadri ya utaalamu na kazi ya kila mmoja.

Tano, baadaye kuwa na SACCOS itakayotuwezesha kiuchumi: kuweka akiba, kukopa.

Mafanikio ya malengo haya yanawezekana kadri tutakavyoendelea kuisimamia ndoto yetu kwa dhati. Ipo hadithi ya siku moja ambapo:
Watu walimuona sungura kashika fimbo na anatembea kwa haraka sana. Wakamuuliza sungura unaenda wapi mbona hauko kawaida? Naye akajibu kuwa naenda kuumuua tembo.  Utaweza sungura? Naye akajibu ndiyo, nitajaribu!

Tuchukue wajibu wa kutekeleza mipango yetu kikamilifu na kutibu matatizo yetu wenyewe kwa ujasiri kwamba tunaweza kumuua tembo wa matatizo yanayotukabili katika kujiendeleza na kuujenga mtandao wetu. Yupo Mshairi maarufu wa Uskochi Robert Louis Stevenson aliyewahi kusema, “Usipime siku yako kwa yale uliyoyavuna bali kwa yale uliyoyapanda.” Malengo hayo yametufanya tuamue kupanda mbegu ya Songea Global Network ili baadaye tuvune mbegu ya mafanikio na utajiri wa ndoto yetu kwa maslahi ya wanachama na ustawi wa mkoa wetu wa Ruvuma ambao sisi ni wakazi.

Mhe, Mgeni Rasmi na Wageni waalikwa mabibi kwa mabwana,
Leo tunavyopanda rasmi mbegu ya mtandao wetu (SGN), tunatumia fursa hii kukumbushana wanamtandao masharti ya kufanikiwa ili tuendelee mbele zaidi kufikia malengo na ndoto yetu.
·         Kujitoa kweli
·         Kupenda kweli mtandao
·         Kuwa na ndoto
·         Kutoa michango ya dhati bila kuchoka

Ni kweli kuja pamoja ni mwanzo. Kufanya kazi pamoja ni umoja. Kudumu katika umoja ni maendeleo. Kuunganisha vipaji vyetu ni kuwa timu moja. Hatimaye kustahimili pamoja ni ushindi wa mtandao wetu huu.

Kuna Hadithi, Upendo, mafanikio na Utajiri : tukikaribisha upendo wa kweli tutafanikiwa katika malengo yetu na kutajirisha mtandao wetu kwa maendeleo ya mkoa wa Ruvuma. Tutafakari na tuchukue hatua.

Inapendeza, inakubalika, inawezekana na inahitajika kuwa na mtandao imara usiokatika network na kufanikiwa kweli. Ni kweli wahenga wa Ghana walishatuasa kwa methali yao kuwa, “Unaweza kumlaumu mtu kwa kukuangusha chini lakini ujilaumu mwenyewe kwa kukataa kunyanyuka.” Naomba wanamtandao tulioamua kuanzisha kwa hiari mtandao huu tusikalie kumlaumu mtu au kujilaumu wenyewe na badala yake tudhamirie na kuwa na bidii ya kunyanyuka leo na kuendeleza ndoto na mtandao wetu. Bila shaka linaloonekana haliwezekani litawezekana, milima isiyokweeka itakweeka na miti isiyopandika itapandika.

Tumuombe Mungu ili idumu, iote na ifanikiwe mbegu ya SGN ambapo sote tuchangie maendeleo yetu na ya taifa letu la Tanzania. Karibuni sote tufurahie jambo hili adhimu na tuchangie kila mmoja kwa nafasi na uwezo wake, kiushauri na kirasilimali aliyonayo kwa  mafanikio ya SGN. Tushikane mikono tuanze safari yetu kwa hatua ya kwanza leo, kwani hata Waswahili wanasema, “Safari ya maili elfu huanzia na hatua moja.” Na hakika ni kweli.  Tumethubutu kubuni na kuanzisha mtandao, tumeweza kuanzisha mtandao huu na sasa tunanuia kusonga mbele na mtandao tuliouanzisha.

SGN safi, safi sana, SGN juu, juu sana!

Mungu Ibariki Tanzania
Mungu Atubariki sote.
Asanteni sana kwa usikivu wenu wa makini!

Naomba kuwasilisha!

KWA NIABA YA WANAMTANDAO WA SONGEA GLOBAL NETWORK. Imeandaliwa na Kusomwa na JOHN M. KASEMBO: 0755 417 074 / 0712 120 775: jmkasembo@gmail.com


 Mgeni rasmi aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu, Seligius Ngahi akiteta jambo na Mwenyekiti wa Mtandao wa Songea Global Network Sakina Jamal wakati wa hafla ya uzinduzi wa mtandao huo iliyofanyika kwenye ukumbi wa Agopal
 Katibu Mtendaji wa Songea Global Network John Kasembo akitafakari jambo wakati wa hafla hiyo
 Mhasibu wa Mtandao wa Songea Global Network Rehema Nasibu akiendelea na utaratibu stahiki katika hafla hiyo
 Wanakamati ambao pia ni wanachama wa Mtandao wa Songea Global Network wakiwa na Mwenyekiti wa Mtandao huo Sakina Jamal katika viwanja vya Agopal
 Wanachama wa Mtandao wa Songea Global Network wakijadiliana jambo wakati wa hafla hiyo

 Wanachama wa Mtandao wa Songea Global Network wakijadiliana jambo wakati wa hafla hiyo


 Wanachama wa Mtandao wa Songea Global Network wakijadiliana jambo wakati wa hafla hiyo


Wanachama wa Mtandao wa Songea Global Network wakijadiliana jambo wakati wa hafla hiyo

WANANCHI WAHAHA KATIZO LA UMEME MANISPAA YA SONGEA



        MENEJA WA TANESCO MKOA WA RUVUMA MONICA KEBARA
Na Stephano Mango,Songea
 
KUFUATIA kuendelea kuwepo kwa tatizo la umeme la kukatika mara kwa mara katika halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma baadhi ya wananchi wameendelea kuelekeza kilio chao kwa uongozi wa shirika la umeme Tanzania(TANESCO) mkoa wa Ruvuma kwa kushindwa hata kutoa taarifa kwa wateja kuhusu katizo hilo ambalo limeonekana kukithiri.
 
Uchunguzi uliofanywa na www.stephanomango.blogspot.com kwa zaidi ya mwezi mmoja umebaini kuwa baadhi ya maeneo ya mji wa Songea yamekuwa yakipata huduma hiyo kwa kiasi kidogo ikiambatana na mgawo usioweza kuelezwa kwa sababu baadhi wamekuwa wakipata huduma hiyo usiku wa manane na alfajiri umeme unakatwa jambo ambalo limesababisha malalamiko mengi ya wateja dhidi ya shirika hilo mkoani Ruvuma.
 
 Uchunguzi huo pia umebaini kuwa katika taasisi za afya ikiwemo hospitali ya Serikali ya mkoa na kituo cha afya cha Mjimwema zimelazimika kutafuta namna nyingine ya kupata nishati ambayo inapaswa kutolewa na shirika la umeme mkoani humu namna hiyo mbadala ya kukabiliana na changamoto iliyofanywa uongozi  wa taasisi hizo za tiba kuwa na jenereta kwa ajili ya kuwezesha kuendelea kujitoa huduma wakati shirika la umeme likiwa limekata huduma hiyo.
 
 Baadhi ya mashine za kusaga nafaka ambazo zipo katika baadhi ya maeneo ya Manispaa hiyo zimeshindwa kutoa huduma kwa muda muafaka na kusababisha wananchi walio wengi kulazimika kutembea umbali mrefu kufuata huduma nje ya Manispaa yakiwemo maeneo ya Lilambo,Shule ya Tanga na Mletele ambako kuna mashine za kusaga nafaka zinazotumia mafuta ya Dizeli na kusababisha bei ya huduma hiyo kupanda mara mbili ikilinganishwa na awali.
 
Wakizungumza kwa nyakati tofauti baadhi ya wamiliki wa mashine za kusaga na kukoboa nafaka wamesema kuwa kitendo cha shirika la umeme mkoani humu kushindwa kutoa huduma hiyo kwa wakati mbali ya kusababisha usumbufu kwao lakini kimekuwa kikiwakosesha mapato ambayo wanayatumia kulipa kodi kwenye mamlaka ya mapato Tanzania(TRA) ambao wanatekeleza wajibu wao wa kukusanya mapato kwa mujibu wa kanuni.
 
 Akizungumza Julius Mlawa(Mtazamo) kuhusiana na hali hiyo alisema huenda akalazimika kusitisha kwa muda kutoa huduma ya usagaji na ukoboaji wa nafaka kama hali hiyo ya ukosefu wa umeme wa uhakika haitafanyiwa kazi na shirika hilo la umeme mkoani humu kwa sababu mbali ya kukosa mapato lakini imekuwa ni usumbufu kwa wananchi ambao wanahitaji huduma hiyo.
 
 Mmoja wa wamiliki wa mashine za kusaga nafaka katika nafaka katika eneo la Manzese ambaye hakutaka jina lake litajwe alisema kitendo cha shirika hilo kutotoa taarifa ya kuwepo kwa mgawo au katizo la umeme na badala yake limekuwa likikata umeme hovyo na kusababisha uharibifu wa mitambo yao.
 
Akizungumza kuhusiana na hali hiyo mganga wa mkoa Dkt.Daniel Malekela amesema kuwa wamelazimika kutafuta jenereta kubwa kwa ajili ya kuendelea huduma hiyo muhimu katika hospitali ya mkoa wa Ruvuma iliyopo mjini Songea kwa sababu huduma za upasuaji na maabara zinahitaji nishati ya umeme muda wote lakini shirika halifanyi hivyo na halitoi taarifa ya katizo kwa muda muafaka.
 
Naye mkurugenzi wa Manispaa ya Songea Nachowa Zakaria alisema kuwa halmashauri hiyo iliangalia uwezekano wa kutatua tatizo hilo kwenye kituo cha afya cha Mjimwema mjini hapa kwa kununua jenereta ambalo linasaidia kwa kiasi kutoa huduma hiyo kwa wananchi walio jirani na kituo hicho cha afya.
 
Kwa upande wake Meneja wa shirika la umeme mkoa wa Ruvuma Mhandisi Monika Kebara alikiri kuwepo kwa tatizo hilo na alisema hivi sasa huduma hiyo ya umeme inatolewa kwa mgawo kwa sababu uwezo wa ufuaji wa umeme umepungua sana kutokana na kuharibika kwa mitambo ya kuzalisha umeme iliyopo Kibulang,oma mjini hapa.
 
 Alisema kituo hicho kina mashine saba za kuzalisha umeme lakini kwa hivi sasa ni mashine tatu ndizo zinazofanya kazi hiyo kwa kutoa Megawati 2.6 wakati mahitaji ni Megawati 5 hasa ikizingatiwa kuwa katika mji wa Songea shirika hilo lina wateja elfu kumi na mbili.
 
Mwisho.

Monday, April 23, 2012

MBARONI KWA KUBAKA NA KUMWEKA MIMBA BINTI WA MIAKA 17

KAMANDA WA POLISI MKOA WA RUVUMA MICHAEL KAMHANDA

Na Gideon Mwakanosya, Songea
JESHI la Polisi mkoani Ruvuma limemtia mbaroni Baraka Makeo (19) mkazi wa eneo la Chandamali katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea kwa tuhuma za kumbaka msichana mwenye umri wa miaka kumi na saba mkazi wa Bombambili ambaye jina lake limehifadhiwa kinyume na sheria.
Akizungumza na www.stephanomango.blogspot.com  jana ofisini kwake Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma Michael Kamuhanda alisema kuwa tukio hilo lilitoke April 16 mwaka huu majira ya saa kumi na mbili jioni huko katika eneo la Bombambili mjini hapa.
Alisema inadaiwa kuwa siku hiyo ya tukio msichana huyo ambaye jina lake limehifadhiwa alikutwa akiwa amewekwa kinyumba  na mwanaume huyo Makeo baada ya kutafutwa kwa muda mrefu na wazazi wake ambao wanadai kuwa aliondoka nyumbani kwao kwa mazingira ya kutatanisha na hawakujua alipoelekea tangu wiki moja iliyopita.
Alifafanua zaidi kuwa taarifa ya kuto kuonekana kwa msichana huyo ambaye jina lake limehifadhiwa ilishatolewa katika kituo kikuu cha Polisi cha Songea mjini na Polisi  kwa kushirikiana na ndugu huyo waliendelea kumtafuta hadi april 16 mwaka huu alipokutwa amewekwa kinyumba na mtuhumiwa Makeo.
Alieleza zaidi kuwa baada ya msichana huyo kukutwa nyumbani kwa Makeo Polisi iliamua kumchukua na kumpeleka katika Hospitali ya mkoa ya Songea kwa uchunguzi zaidi ambako iligundulika kuwa msichana huyo ana mimba ya miezi mitano ambayo inadaiwa kuwa alipewa na mtuhumiwa .
 Kamanda Kamuhanda alifafanua zaidi kuwa mtuhumiwa Makeo anatarajiwa kufikishwa Mahakamani mara tu upelelezi wa tukio hilo utakapo kamilika .
Mwisho.

Friday, April 20, 2012

ADAIWA KUJINYONGA KWA SABABU ZA WIVU WA KIMAPENZI


       KAMANDA WA POLISI MKOA WA RUVUMA MICHAEL KAMHANDA

Na Augustino Chindiye, Tunduru

MSONGO wa mawazo uliotokana na wivu wa kimapenzi umesababisha kifo cha Mkazi wa Mtaa wa Kasuguru Mjini Tunduru aliyefahamika kwa jina la Said Issa (43) aliyefariki dunia baada ya kujinyonga.

Taarifa za tukio hilo zinaeleza kuwa kabla ya kukumbwa na umauti Marehemu Issa alitoweka na kupotelea kusiko julikana March 31 Mwaka huu kabla ya mwili wake kuokotwa April 16 mwaka huu ukiwa vipande vipande kutokana na kuharibika vibaya.

Taarifa hiyo iliendelea kufafanua kuwa kutokana na mwili wake kuharibika vibaya ambapo mashuhuda hao walikuta baadhi ya viungo vikiwa vimetawanywa katika maeneo tofauti huku vingine vikiwa vimeanza kuliwa na wanyama na kufanikiwa kumzika akiwa hana kichwa

Akizungumzia mkasa huo mdogo wa marehemu Isaa Matumla alisema kuwa marehemu kaka yake huyo alianza kuchanganyikiwa siku chache baada ya kuachwa na Mkewe ambaye alidaiwa kuchukua uamuzi huo kwa lengo la kupumzika maisha ya shida waliyo kuwa wakiishi kwa muda mrefu kutokana na mumewe huyo kutokuwa na uwezo kifedha.

Alisema kufuatia mkasa huo Marehemu alionesha kuchanganyikiwa kiakili na kuwa mlevi wa kupindukia hatimaye akaamua kuchukua uamuzi huo wa kukatisha maisha yake kwa kujinyonga akiwa mafichoni katika msitu ulozunguka mashamba ya Shule ya Sekondari Tunduru.

Mganga aliyeufanyia uchunguzi mwili wa Marehemu Issa Dkt. Joseph Ng`ombo alidai kuwa chanzo cha kifo hicho kilisababishwa na tukio la kujifunga kamba shingoni na kujining`iniza juu ya mti kabla ya mwili wake kuanguka chini na kuharibika vibaya.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma Mchael Kamuhanda mbali ya kuthibitisha kuwepo kwa tukio hilo alisema kuwa polisi bado wanaendelea na uchunguzi wa kifo hicho.

Mwisho