About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Thursday, September 8, 2011

RAIA 11 WA PAKISTANI NA BANGLADESHI KURUDISHWA MAKWAO

RAIA 11 WA PAKISTANI NA BANGLADESHI KURUDISHWA MAKWAO
Na Stephano Mango ,Songea.

WATU kumi na moja ambao ni raia wa Pakstani na Bangladesh waliokuwa wamekamatwa katika kijiji cha Magwamila kilichopo wilayani Songea mkoani Ruvuma wakitokea Msumbiji ambako walifukuzwa na askari wa Nchi hiyo kwa kupigwa na mijeredi sehemu mbalimbali za miili yao na kujeruhiwa wanatarajiwa kurejeshwa kwenye Nchi zao kwa kupitia ofisi za balozi za Nchi hizo hapa nchini.

Afisa uhamiaji wa Mkoa wa Ruvuma Koku Rwebandiza akizungumza jana na mtandao huu wa http://www.stephanomango.blogspot.com/ amesema kuwa raia hao wa Pakistan na Bangladesh kwa sasa hivi wanafanyiwa taratibu za kuwarejesha kwani walipokamatwa huko katika kijiji cha Magwamila walikutwa wakiwa na hati za kusafiria ambazo zilionekana kuwa na utata.

Rwebandiza alisema kuwa hati hizo za kusafiria ambazo walikutwa nazo watu hao ambao ni Raia wa Bangladesh na Pakstan hazioneshi ni lini waliingia Tanzania wakati wakitokea kwenye Nchi zao wala hazionyeshi ni lini waliondoka hapa Nchini na kuelekea Msumbiji ambako walikamatwa wakiwa katika eneo la Lichinga na askari wa Nchi ya Msumbiji.

Alisema kuwa kutokana na hali hiyo idara ya uhamiaji  mkoani Ruvuma imelazimika kuwarejesha raia hao kwenye balozi za Nchi zao ambazo ndizo zitakazoangalia ni namna gani zitawarudisha kwenye nchi zao.

Rwebandiza alisema kuwa raia hao kumi na moja wa nchi za pakistan na Bangaladesh walikamatwa mwanzoni mwa wiki huko katika kijiji cha magwamila kilichopo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji ambapo inadaiwa walifukuzwa toka msumbiji kwa kupigwa mijeredi sehemu mbalimbali za miili yao na kunyang'anywa mali zao zote walizokuwa nazo pamoja na fedha na askari wa nchi ya Msumbiji kisha waliletwa hadi mpakani na kufukuziwa kijijini hapo huku wakiwa na majeraha.

Hata hivyo afisa uhamiaji Rwebandiza alisema kuwa raia hao baada ya kuwahoji walieleza kuwa wao walitoka Pakstan kwa pamoja kwa usafiri wa Ndege hadi Tanzania kupitia uwanja wa ndege wa kimataifa wa jijini Dar es salaamu na baadae walitafuta usafiri wa basi hadi Mtwara ambako nako walifanikiwa kupata usafiri wa malori hadi wakafanikiwa kuvuka msumbiji ambako walinaswa na askari wa Nchi hiyo.

Raia hao ambao walikamatwa ni wapakistan watano ambao ni Hassan Bilali (20), Fawad Yassin (20), Mohamed Hawadhi(20),Haftari Hussein (24) na Hassad Hawadh (45) na raia toka Bangladesh waliokamatwa ni sita ambao ni Shahed Alzani (29) ,Amar Hamad (25),Garuan Khalifa(40),Mohamed Parvaz(35) ,Shajar Meya (28) na Sao Meya (28) .

MWISHO.

WANAHARAKATI WALALAMIKIA MIGOGORO YA ARDHI KUKWAMISHA MAENDELEO NCHINI

WALALAMIKIA MIGOGORO YA ARDHI KUKWAMISHA MAENDELEO

Na Juma Nyumayo, Dar es Salaam

MIGOGORO ya Ardhi inayoendelea katika mikoa mbalimbali nchini imetajwa kuwa ni kikwazo kikubwa cha maendeleo ya wanawake katika harakati zao za kujikwamua kiuchumi pia kuleta ukombozi wa mwanamke na maendeleo stahiki hapa nchini.

Hayo yameibuliwa na washiriki wa warsha inayoendelea katika Ukumbi wa Kitivo cha Uhandisi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakati wa uwasilishaji wa mada ya mifumo na vikwazo vinavyozuia wanawake kujikwamua kiuchumi.

Akiwasilisha Mada hiyo, Mwezeshaji toka TGNP, Rehema Mwateba alisema ni vyema washiriki wakaeleza hali halisi ya umiliki wa ardhi na migogoro inayendelea kujitokeza hivi sasa ikilinganishwa na mifumo iliyopo katika kumkomboa mwanamke kimapinduzi.

Mshiriki mmojawapo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Morogoro,Kibena Kingo, ametolea mfano wa mapigano yanayoibuka mara kwa mara na yanayoendelea wilayani kwake kati ya wafugaji na wakulima, ambapo chanzo kikiwa ni matumizi ya Ardhi na kwamba mgogoro huo ni mkubwa.

Imeelezwa wafugaji hao wanaotokea mikoa ya kaskazini na kati wanalishia wanyama wao mazao ya wakulima bila kujali na hivyo kuwakwaza wananchi wenyeji ambao wengi wao ni wakulima wa mazao ya chakula.

"Mgogoro wa ardhi ni mkubwa na waathirika wakubwa ni wanawake na watoto, hata hivyo ni lazima hatua zichukuliwe ili kutatua migogoro hii kabla hayajatokea mauaji makubwa," alishauri Kingo.

Wakati kingo akielezea mgogoro wa ardhi Morogoro bado Mwezeshaji toka TGNP Darus Badi alipaza sauti yake na kuthibitisha kuwa mtandao huo una rekodi ya migogoro ipatayo 60 ya ardhi katika mkoa huo na kwamba kuna haja ya kulichukulia uzito tatizo hilo.

" Tuna migogoro tunayoijua kule Morogoro na tukiwa kama wanaharakati lazima tushirikiane kuchukua hatua," alisema Badi.

Naye Makamu Mwenyekiti wa halamashauri ya Mbinga Prisca haule alisema migogoro mingi ya ardhi huko Mbinga imeibuka kutokana na wakazi wa huko kutafuta maeneo ya kulima baada ya kuishiwa ardhi maeneo ya milimani.

"Kuna migogoro ya ardhi katika familia na nje ya familia kupigania ardhi ya kulima," alisema na kubainisha kuwa bado kuna mipango mibovu na sera isiyoeleweka katika umiliki wa ardhi.

Hata hivyo lawama azikuachwa kwa wawekezaji katika vitalu vya mbuga za wanyama hadi migodi ya madini kama ya Buzwagi, Geita hadi huko Namtumbo kwenye Urani( Uranium) ambako wananchi wa kawaida na hasa wanawake wanaona kama mchezo wa kuigiza wasijue kinachoendelea kwenye ardhi yao.

Lawama kibao zimeelekezwa pia kwa Mamlaka za vijiji na Miji kugawa ardhi kwa upendeleo na hasa kwa wale wanaotoa kitu kidogo kwaajili ya kupata viwanja vya makazi na kuwaacha kabisa wanawake nyuma.

Wakati wa Ufunguzi wa warsha hiyo, Mkuu wa Taasisi ya Mafunzo ya Jinsia ya TGNP, Dkt. Diana Mwiru, aliwaasa washiriki kujadili mada mbalimbali kwa lengo la kujenga uelewa na kusaidi jamii tunapoelekea kusherehekea tamasha la Jinsia na Mika 50 tangu Tanganyika kupata Uhuru wake.

Dkt. Mwiru,alisema, katika miaka 50 iliyopita wanawake wa nchi hii wameendelea kuachwa nyuma katika kumiliki na utoaji wa maamuzi juu ya rasilimali  ikiwa ni pamoja na ardhi.
Mwisho

WATATU WAJITOKEZA KUGOMBEA UDIWANI KATA YA MATIMILA WILAYA YA SONGEA

                                Kaimu Mkurugenzi wa Wilaya ya Songea Anna Mbogo

Na Gideon Mwakanosya,Songea.

WATU watatu wamejitokeza kuchukuwa fomu akiwemo katibu wa Mbunge wa Jimbo la Peramiho Menansi Komba za kuwania nafasi ya kiti cha udiwani kata ya Matimila Wilaya ya Songea vijijini Mkoa wa Ruvuma baada ya kuachwa wazi na aliyekuwa diwani wa kata hiyo Joseph Komba (CCM) kufariki dunia kwa ajari ya pikipiki.

Akizungumza na mwandishi wa mtandao huu wa http://www.stephanomango.blogspot.com/ jana ofisini kwake Mkurugenzi wa uchaguzi jimbo la Peramiho Anna Mbogo amewataja waliochukuwa fomu kuwa ni Eliutelius Pili  wa chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Juma Gawaza wa chama cha wananchi CUF na Menansi Komba wa chama cha Mapinduzi(CCM).

Mbogo amesema kuwa hata hivyo mwisho wa kurudisha fomu hizo ni septemba 9 mwaka huu majira ya saa 10 jioni na kwamba kampeni zitaanza rasmi septemba 10 hadi Oktoba 1 mwaka huu majira ya sa 12 jioni.

Hata hivyo amewataka wananchi wa kata hiyo kujitokeza kwa wingi kwenye uchaguzi mdogo wa kujaza nafasi ya udiwani siku ya oktoba 2 mwaka huu kwani kumekuwepo na mazoea ya kutojitokeza kwenye zoezi la upigaji kura hali inayopelekea udororaji wa demokrasia nchini.

Mkurugenzi wa uchaguzi wa jimbo hilo ambaye pia ni kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya ya Songea  Mbogo amesema kuwa uchaguzi mdogo wa kujaza nafasi ya kiti cha udiwani katika kata ya Matimila unatarajiwa kufanyika oktoba 2 mwaka huu kufuatia kifo cha aliyekuwa diwani wa kata hiyo  Joseph Komba aliyefariki kwa ajari ya pikipiki wakati anaendesha kijijini hapo Machi 9 mwaka huu.