About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Saturday, March 17, 2012

RAIS KIKWETE, VIJANA MITAANI WANAKUULIZA HIVI............................?



                    Rais wa Tanzania Jakaya Kikwete

Na Stephano Mango, Songea

RAIS Jakaya Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, naomba leo nitumie nafasi hii kuzungumza nawe juu ya mambo machache ambayo nimekuwa nikisikia vijana wanayazunguza na kutamani kuyafikisha kwako juu ya serikali yako na namna wanavyokutazama katika nafasi yako juu ya mustakabali wa maisha yao chini ya jua hili.

Hivyo ninaomba ufahamu kuwa vijana wengi wana mengi ya kusema nawe kama ilivyo kwa watanzania wengi, tatizo kubwa ni namna ya kufikisha kauli yao hiyo kwako. Hivyo mimi naomba nibebe wajibu huo wa kuwa kipaza sauti cha vijana kwa kufikisha kauli yao kwako.

Awali ya yote napenda kukupa pole kutokana na majukumu mengi ya kuwatumikia watanzania, majukumu uliyokabidhiwa na wananchi kupitia sanduku la kura mnano tarehe 14.12.2005 ambayo mpaka leo bado unayo.
Mheshimiwa Rais, kwa muda mrefu sasa vijana wa kitanzania wamekuwa wakilalamika juu ya mazingira magumu yanayowakabili katika harakati zao za kimaisha. Hii inatokana na jinsi hali ilivyobadilika tofauti na matarajio waliyokuwa nayo juu yako kabla na baada ya kuchaguliwa kwako kuwa rais wa awamu ya nne wa Tanzania.
Hivyo wamekuwa wakijiuliza kama ni kweli kuwa ile kauli ya “Maisha bora kwa kila Mtanzania” na ile ya “Tanzania yenye neema yawezekana” inawahusu wao au ni kwa wale wachache tu walio katika mazingira ya kujichukulia Chao Mapema.
Ninakumbuka wakati unapiga kampeni na kuomba kura kwa watanzania mwaka 2005 na mwaka 2010 ulikuwa na kauli mbiu nzuri juu ya vijana kuwa utawawezesha Vijana kujiajiri
Mheshimiwa Rais, wakati uliporudi jijini Dar es salaam baada ya kuteuliwa Mjini Dodoma kuwa mgombea wa CCM katika uchaguzi mkuu wa 2005, ulipata mapokezi makubwa sana ambapo pamoja na mambo mengine ulikutana na kilio cha vijana juu ya matatizo mbalimbali yanayowakabili.
Hivyo walipoongea nawe katika Ukumbi wa Diamond Jubilei ulisema kuwa umesikia kilio chao na hivyo uliahidi kujitahidi kutafuta namna ya kuwasaidia vijana hao kutoka katika hali ngumu ya maisha inayowakabili.
Hata hivyo hali imekuwa ni tofauti na matarajio yao tangu serikali yako iingie madarakani. Swali la vijana ni je ulikuwa unawalaghai au kuna vitu ulivyokutana navyo ikulu vikakwamisha dhamira yako njema uliyokuwa nayo dhidi yao?
Swali hili limekuwa likiulizwa kwani mambo yanayoendelea kwa vijana baada ya kuingia madarakani serikali yako yamewakatisha tamaa na wengi wamekuwa wakijuta kwani hawakutarajia kuona hayo hasa kwa kuzingatia kuwa eti (ulikuwa mshikaji wao) katika hali ngumu ya maisha.
Vijana wamekuwa wakiuliza kuwa je zile ajira milioni moja ulizoahidi kila mwaka bado zipo au zinachukuliwa na wawekezaji wa nje au ni kwa vijana wapi, na kwa wale uliowaahidi kuwawezesha kujiajiri ni hao serikali yao iliyoamua kuwafukuza mjini kwa kuwa wanachafua miji kwa kutembeza bidhaa mikononi na kuuza mitumba katika maeneo ambayo mnadai si maeneo si rasmi?
Je ni wapi mlipowatengea vijana hao penye nafasi na miundo mbinu bora na wakakataa kwenda? au ndio Machinga Complex yenye kiza kinene?
Mheshimiwa Rais, hivi karibuni nilikuwa jijini Dar es salaam, ambapo kwa bahati nzuri nilipata nafasi ya kuzunguka katika maeneo mengi ya jiji hilo, kwa sehemu kuwa vijana waliokuwa wakifanya biashara zao za kuuza mitumba na bidhaa nyingine (maarufu kama wamachinga), wameondolewa na kupelekwa katika maeneo yasiyo na biashara wala miundo mbinu,
Matokeo yake wengi wamekata mitaji yao kiasi cha baadhi yao kuamua kujiua baada ya kubomolewa kwa vibanda vyao bila kujua kama huko walipokuwa wanapelekwa ni sehemu sahihi au la, pia zoezi hilo limehamia pia kwa wapiga debe na makondakta wasio na shughuli maalum katika vituo mbalimbali vya daladala.
Hata hivyo licha ya hatua hiyo kuchukuliwa kwa ajili ya vijana hao ambao nao ni wahitaji na wamekuwa wakitegemea kupata riziki kupitia maeneo hayo, bado hakuna hatua mbadala zimechukuliwa katika kuwasaidia wahusika hao ili wasiende kufanya zile biashara za kutegemea mtaji wa nguvu zao (wizi, ujambazi, umalaya na ukahaba).
Zoezi hili si la jijini Dar es salaam tu, bali ni katika maeneo yote ya nchi yetu. Kwa sehemu kubwa inaonekana kuwa tumehamisha tatizo kutoka sehemu moja na kulipeleka sehemu nyingine, kwani hakuna mbinu mbadala za kuwasaidia hao tuliowaondoa mjini.
Mheshimiwa Rais, pamoja na kauli nzuri za viongozi wetu juu ya kuwataka vijana kurudi vijijini kwa ajili ya kujiingiza katika kilimo kwanza na ufugaji lakini ukipita katika maeneo mengi ya vijijini utakutana na hali mbaya ya maisha ya huko na wala hakuna miundo mbinu mizuri wala pembejeo kwa wale wote wanaoamua kujikita katika sekta hizo muhimu.
Na kwa wale wachache wanaojifanyia shughuli hizo, bado hawapati soko wala mazao yao hayanunuliwi kwa wakati na kama wanauza mazao yao basi ni kwa wafanyabiashara ambao wananunua mazao hayo kwa bei ya chini na hivyo kuwa ni hasara kwao,nani atawasaidia hao katika mikakati yao ya kujikwamua kiuchumi?.
Vijana wanauliza, mbona wao hata kama wamejiunga katika vikundi vya watu wasiopungua hamsini hawawezi kupata mikopo ili nao wafanye biashara zitakazowanyanyua kiuchumi na hivyo kuitwa wajasiriamali wa ndani? Kwani kila wakifanya hivyo hawafanikiwi, kwa hili unasemaje mheshimiwa rais?

Mheshimiwa Rais, vitendo vya unyanyasaji na kuwaua vijana na wachimbaji wadogo vinavyofanywa na wachimbaji wakubwa ambao wengi si raia katika maeneo mbalimbali ya migodi ya madini yetu ni sehemu ya kilio cha kila mara huku serikali yako ikifumbia macho bila kutoa walao kauli ya kukemea matendo hayo ni sehemu ya swali ambalo vijana wamekuwa wakiuliza.
Wao wana nafasi na kauli gani katika kujinufaisha na ujtajiri huo ambao ni sehemu ya neema kubwa Mwenyezi Mungu aliyoitunukia Tanzania na sasa inachukuliwa na wageni kama mali isiyo na wenyewe? Ni vema ukawajibu vijana hata hili.
Kuna vikundi mbalimbali vya vijana katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu wanaoishi na VVU, lakini pamoja na wao kukaa kama familia, bado hawapati misaada itakayowawezesha walao kuwa na miradi ya kuwapatia mapato ili waweze kujikimu kimaisha
Kwani iwapo vijana hawa wasipopata misaada ni hatari sana kwa maisha ya watanzania wengine kwani wanaweza kuamua kusambaza VVU kwa makusudi bila kujulikana licha ya kuwa wamekuwa wazi kuwa wanaishi na VVU.
Kwasababu ,wengi wao wamekuwa wakitongozwa na wanaume/wanawake wengine kwa kuwa hawajionyeshi na kwa kweli wengi wao ni wazuri wa sura na miili na afya zao ni nzuri na wala huwezi kuwatilia shaka kama hutaelezwa kuwa wanaishi na VVU. Hili pia ni swali la vijana kwako.
Mheshimiwa Rais, nina mengi ya kuzungumza nawe kwa niaba ya vijana wa Tanzania, hata hivyo naomba uniruhusu niseme kuwa umefika wakati wa kuwasiliza vijana, kwani kilio kikubwa cha vijana ni kutokusikilizwa.
Hivyo ninakuomba sana ujitahidi pamoja na ratiba yako kutingwa na shughuli nyingi za nchi, utenge walao siku moja ili ukae na vijana wa Tanzania uwasikilize kwani nina imani kuwa wana mambo mengi ya kusema nawe.
Ninayasema haya kwa kuwa mpaka sasa hakuna waziri yeyote wa Wizara ya Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana au hata manaibu mawaziri wao, aliyewahi kupanga na kukaa na vijana na kuwasikiliza katika kilio chao.
Fahamu kuwa kwa sehemu kubwa inawezekana kuwa mengi huyafahamu na wala hujayasikia yote, lakini ukipata nafasi ya kuwasikiliza vijana utafahamu hayo na mengi zaidi ambayo ulikuwa hujayasikia.

Mheshimiwa Rais, nimalizie kwa kusema kuwa, vijana wanahitaji kusikia jambo jipya, wengi wanatamani kupata nabii mpya wa kuwaokoa na wala habari za kisiasa si za lazima kwao kwani wengi wana maisha magumu, hawajui watakula nini kesho na wala maisha yao watayaboresha vipi.
Hivyo unaombwa kubeba wajibu huo kwa nguvu mpya ili vijana wakiri kuwa sasa wameuona ukombozi ulio tayari kwao. Ni matarajio ya vijana kusikia kitu juu ya hayo na mengine mengi ambayo hayajaandikwa hapa ili waweze kujua kuwa wewe ni mkombozi wao au wasubiri mwingine.
Mwandishi wa Makala
Anapatikana 0715-335051
www.stephanomango.blogspot.com