About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Wednesday, January 29, 2014

LOWASSA HATARINI KWA TAMKO LA VIJANA



 Paul Christian Makonda,Katibu wa Hamasa na Chipukizi.
“..Chama Cha Siasa chochote duniani hubomoka kutokana na migongano iliyokithiri ya muda mrefu. Uzoefu wa vyama vikubwa vilivyoporomoka umeonyesha hivyo! Chama lazima kidhibiti uchu wa madaraka wa baadhi ya viongozi wake na ndani ya serikali yake...” – Dr Eginald P. Mihanjo
“..Chama cha siasa ni itikadi. Chama cha siasa ni siasa kwa maana halisi ya neno lenyewe siasa –“siasa”. Ni mahali ambapo watu wenye madhumuni mamoja yaliyoainishwa waziwazi hukutana na kuwa kitu kimoja. Chama cha siasa sio mkusanyiko wa “majini dume yenye tamaa”, - majini ambayo yametanguliza mbele tamaa kufa na kupona-tamaa ya kutengeneza pesa au kupata vyeo kwa gharama yoyote! – Dr Bashir Ally

UTANGULIZI:
Hili ni tamko la vijana makini wa jumuiya ya umoja wa vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) kuunga mkono juhudi na utendaji wa sekretarieti ya halmashauri kuu ya Chama Cha Mapinduzi ikiongozwa na Katibu Mkuu Komredi Abdulrahaman Kinana.

Maneno ya utangulizi yamebeba dhima ya tamko hili, kufuatia taarifa zilizoripotiwa kwenye baadhi ya vyombo vya habari vikiwanukuu baadhi ya wanachama wa Chama Cha Mapinduzi, wakiwatuhumu Viongozi wa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM, Katibu Mkuu Ndugu Abdulrahaman Kinana na Katibu wa Itikadi na Uenezi Ndugu Nape Moses Nnauye.

Sisi Vijana tunatambua kuwa tuhuma hizo na maneno hayo ya hovyo yametolewa kwa nia ovu yenye kulenga kuwakatisha tamaa Viongozi hao wa Chama. Tunafahamu kuwa upo mkakati wa kiuhaini ulioandaliwa na kuratibiwa na “mtandao” ndani ya Chama ambao umejipanga kuendesha uhaini huo.

Sisi vijana wa UVCCM tunatambua na kuthamini juhudi za Katibu Mkuu na Sekretarieti yake katika kukijenga na kukiimarisha Chama kwa kuisimamia barabara misingi na shabaha ya kuundwa kwake, katika umri wetu hatukuwahi kuona Chama kikiwa karibu na wananchi kwa kufuatilia, kusikiliza na kushiriki katika utatuzi wa kero, shida na changamoto zao kama ilivyo katika kipindi hiki chini ya Comrade Kinana na timu yake. Juhudi hizi ni za kuungwa mkono na kamwe si za kubezwa na mwanaCCM muadilifu, muaminifu na mwenye mapenzi ya kweli kwa Chama.

Juhudi za kukiimarisha Chama kutoka ngazi za chini, kwa mabalozi ni mkakati bora kuwahi kutekelezwa na Chama, kukirudisha Chama kwa wanachama ni kutimiza lengo la kuundwa kwa Chama hiki, Chama hiki ni cha wanyonge, masikini wa Taifa hili, HAIWEZEKANI matajiri watake kukihodhi na waratibu mikakati ya kukihujumu kwa pesa zao hali sisi vijana tukitazama, tunasema tutakilinda Chama chetu na tutawalinda viongozi wetu waadilifu.

Ni hawa ambao wanabezwa leo ndio wameweza kurudisha Imani ya wananchi kwa Chama, Imani na matumaini ambayo tayari yalishaanza kupotea na Chama kuonekana si tena cha wanyonge, wakulima na wafanyakazi wan chi hii.

Ni Comrade Kinana na timu yake ndio waliozunguka kwenda kukutana na wakulima wa Pamba kule mikoa ya Kanda ya ziwa na kumpeleka balozi wa China na kumshawishi kujenga viwanda ili kuboresha manufaa kwa wakulima.

Ni Comrade Kinana na timu yake ndio waliokwenda Kusini kukutana na wakulima wa Korosho na kushirikiana nao pamoja na bodi kutatua tatizo la Korosho.

Ni Comrade Kinana na timu yake ndio walioibua hoja na kero za wafugaji, walimu na wananchi kwa ujumla, na kuwataka viongozi wa Serikali kuhakikisha wanawajibika kwa wananchi walipa kodi wa Taifa hili.

Kupinga mafanikio ya Ziara hizo ni kupinga utetezi wa wanyonge.

Mtu anayebeza ziara hizo na kuwaita Viongozi waliozifanya waropokaji na wahuni wahuni ni mtu mjinga, mtu wa hovyo,hana maadili, asiyekipenda Chama, mhaini na mzandiki anayepaswa kuchukuliwa hatua kali za kinidhamu ili iwe fundisho kwa wengine.

TAMKO hili limezingatia wosia wa Baba wa Taifa, muasisi wa Chama Cha Mapinduzi Mwl Julius Kambarage Nyerere katika kitabu Chake TUJISAHIHISHE.

“Inapofikia wasimamizi wa Kanuni za Chama wanapigwa vita ya wazi kwa uamuzi wao wa kukisimamia Chama, tafsir yake ni moja tu watu wanaowapiga vita hawakitakii mema chama chetu.”

Imetolewa na Paul Christian Makonda.

Katibu wa Hamasa na Chipukizi.

Monday, January 27, 2014

WAFANYABIASHARA MANZESE WAUCHARUKIA UONGOZI WAO



Na, Stephano Mango, Songea
WAFANYABIASHARA  wa Soko la Manzese B lililopo katika halmashauri ya Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma wameutaka Uongozi wao ujiudhuru mara moja kutokana na utawala mbovu wanaoufanya na kuendeleza vitendo vya hujuma katika soko hilo

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na waandishi wa Habari jana katika viwanja vya soko hilo walisema viongozi hao wamekuwa wakishirikiana na Viongozi wa Halmashauri ya Manispaa kukiuka maadili ya uongozi na kusababisha migogoro ya mara kwa mara inayopelekea uvunjifu wa amani

Walisema kuwa toka kuwepo kwa mpango wa ujenzi wa vibanda 68 vya Soko hilo, viongozi wamekuwa wakifanya vikao vya siri vya kuwahujumu wafanyabiashara waliopo sokoni hapo kwa kupanga mipango ya kuwanyang’anya ili vibanda hivyo wapewe wafanyabiashara  vigogo ambao hawafanyi biashara katika soko hilo

Walisema kuwa mipango hiyo ya siri imezua malalamiko makubwa sana miongoni mwa wafanyabiashara kwani makubaliano ya awali yalikuwa ni lazima wafanyabiashara waliopo wapewe kipaumbele katika ujazaji wa mikataba katika ujenzi huo

“ Tunashangaa kuona viongozi wa Soko na Viongozi wa Halmashauri wanatoa mikataba kwa siri kwa wafanyabiashara vigogo kutoka maeneo mengine kinyume na utaratibu kitendo ambacho kimetusikitisha sana kwani hakijawa na uhalali wa kidemokrasia zaidi ya ubabe”

Walisema hali hiyo inaonyesha wazi kabisa kuwa kuna vitendo vya rushwa, ukiukwaji wa haki za binadamu kwani mara kwa mara wafanyabiasha wakihoji uhal wa mambo ambayo yanafanywa na viongozi hao wanatishiwa kwa maneno ya kuudhi

Akizungumza na Waandishi wa Habari Mwenyekiti wa Soko hilo Omary Masai alisema kuwa yeye sio msemaji wa jambo hilo kwani linafanywa Mstahiki Meya wa Halmashauri Charles Mhagama hivyo kwa maelezo zaidi atafutwe yeye

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Misufini ambako soko hilo lipo Salumu Mfamaji alisema kuwa ujenzi huo unafanywa kihuni kwani kuanzia viongozi wa Serikali ya Mtaa na Serikali ya Kata haijashirikishwa na kuwa jambo hilo linaonekana limegubikwa na rushwa

Mfamaji alisema kuwa amewasiliana na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea Nachoa Zakaria na wataalamu wake kusitisha mara moja ujenzi huo mpaka pale mkutano wa wafanyabiashara utakapoitishwa ili waweze kutendewa haki ikiwemo ya kuonyeshwa ramani ya Soko hilo na mikataba

Naye Meya wa Manispaa hiyo Charles Mhagama alipohojiwa kuhusiana na malalamiko ya Wafanyabiashara alisema kuwa tatizo hilo lipo lakini alidai kuwa msababishaji mkubwa ni Diwani wa kata hiyo na ndio maana Halmashauri imeamua kusimamia yenyewe ujenzi huo

Hata hivyo juhudi za kumtafuta Mkurugenzi wa Halmashauri kupitia simu yake ya kiganzani Nachoa Zakaria ziligonga mwamba kwani simu yake ilikuwa inaita tu bila kupokelewa

MWISHO