About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Wednesday, July 6, 2011

Mkuu wa kituo cha michezo kanda ya kusini Vicent Mbaya akifafanua jambo wakati wa mafunzo ya maafisa mipango miji,wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi Msaidizi wa michezo nchini Juliana Yassoda,wa pili ni Afisa elimu Taaluma mkoa wa Ruvuma Frezier Zombe,wa kwanza kulia ni Afisa Michezo mkoa wa Ruvuma Hassan Katuli,wa pili ni mkufunzi wa michezo nchini Mohamed Madenge

MAAFISA MIPANGO MIJI NI NGUZO MUHIMU KWA MAENDELEO YA MICHEZO
Na Stephano Mango,Songea
SUALA la michezo lina mchango mkubwa sana katika maendeleo ya nchini yoyote ile duniani lakini sote ni mashahidi kuwa michezo mingi inayoshirikisha watu wengi haichezwi kwa ufanisi kutokana na kutokuwepo maeneo ya kutosha kwa ajili ya michezo hiyo

Maeneo mengi ambayo yalikuwa yametengwa kwa ajili ya michezo na burudani yamevamia na kupewa matumizi tofauti mbali na yale yaliyokusudiwa na hivyo kuwanyima wananchi fursa ya kucheza michezo

Viwanja vingi vilivyopo nchini vimekosa matunzo kutoka kwa mamlaka husika na wadau wa michezo nchini kwani miundombinu yake imekuwa chakavu na kusababisha viwanja hivyo kushindwa kukidhi haja ya matumizi yake

Ili michezo iweze kuendelea inahitaji kuwepo kwa viwanja kwani sheria namba moja ya kila michezo ni viwanja na vifaa vya kuchezea michezo kwa kutambua hilo juni 20 hadi 24,2011 Wizara ya Habari,Vijana,Utamaduni na Michezo kupitia Kituo cha Michezo Kanda ya Kusini

Kiliandaa mafunzo ya ushiriki wa Maafisa Mipango Miji katika maendeleo ya michezo nchini ambapo wadau kutoka katika Halmashauri za Miji,Manispaa na Majiji kutoka katika mikoa ya Shinyanga,Mbeya,Iringa,Mwanza,Ruvuma,Rukwa,Morogoro walihudhuria mafunzo hayo

Akizungumza kwenye mafunzo hayo yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Chama cha Walimu Tanzania(CWT) tawi la Ruvuma Mkuu wa Kituo cha Michezo Kanda ya Kusini Vicent Mbaya alisema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea wa kuthubutu Maafisa Mipango Miji juu ya kutenga,kujenga na kutunza viwanja ambavyo vinatengwa kwa matumizi ya michezo

Mbaya alisema kuwa pia mafunzo hayo yalilenga kuwaunganisha pamoja wataalamu wa Mipango Miji na wa michezo ambapo mada mbalimbali ziliwasilishwa ikiwemo ya historia ya michezo Duniani na Tanzania,namna ya kutoa ushauri wakati wa ujenzi wa viwanja vya michezo kwa maafisa Mipango Miji ,ustawishaji wa viwanja vya michezo

Alisema kuwa mada zingine ni Tasnia ya michezo(Sports Industry)Sera ya maendeleo ya michezo na utawala bora,Uongozi na utawala katika michezo,Viwanja vya michezo katika michezo,Upimaji wa viwanja vya michezo na Tathimini na majadiliano mbalimbali

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Maendeleo ya Michezo Nchini Juliana Yassoda akitoa salamu zake kwenye mafunzo hayo alisema kuwa  Serikali ya awamu ya tatu na nne zimelipa msukumo mkubwa suala la miundombinu ya michezo ili watanzania waweze kupata fursa ya kucheza michezo

Yassoda alisema pia waweze kuibua vipaji katika michezo ili kujenga afya zao,kupambana na umasikini,kuchelewesha uzee,kuongeza umri wa kuishi na hivyo kufanikisha dhana ya maisha bora kwa kila mtanzania kwani ushahidi katika hilo ni uamuzi wa Serikali kujenga uwanja wa kisasa mpya uliopo Dar es Salaam
                                                                                                                                                                                                              
Alisema kuwa katika kuleta maendeleo ya michezo nchini,Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010 ibara ya 201 kipengele cha michezo,kipengele kidogo cha (g),(i) na(1)vinatutaka kuimarisha,kulinda na kutenga maeneo ya wazi kwa ajili ya maendeleo ya michezo

Alieleza kuwa washiriki wa mafunzo wanatakiwa kuisoma vizuri ilani hiyo,kuitafakari na kuifanyia utekelezaji ili michezo iweze kuendelea kwani sote tunajua ya kuwa michezo bila viwanja haiwezi kuchezeka kwa kuwa sheria namba moja ya kila michezo ni viwanja na vifaa vya kuchezea michezo

Akifungua mafunzo hayo Afisa Elimu Taaluma mkoa wa Ruvuma Frezier Zombe alisema kuwa mafunzo hayo yanalenga kuwawezesha washiriki ambao ni Maafisa mipango miji,Mameneja wa viwanja,Wizara ya Habari,Utamaduni na Michezo na Kituo cha Michezo Kanda ya Kusini kutambua changamoto mbalimbali katika kutenga,kujenga na kutunza viwanja vya michezo

Zombe aliwaasa washiriki kutambua wajibu wao katika kusimamia maendeleo ya michezo kulingana na utekelezaji wake na kazi za kila siku ndani ya mamlaka husika ikiwa ni pamoja na kutambua na kutafakari manufaa ya michezo katika nyanza mbalimbali kama vile kiuchumi,kijamii na kiafya

Alisema kuwa washiriki wanapaswa kutumia vema muda huo wa mafunzo kutambua mahitaji halisi ya ukubwa wa viwanja,eneo linalostahili kujengwa kiwanja na uelekeo wa uwanja

Akizitaja changamoto mbalimbali zilizojitokeza wakati wa mafunzo Afisa Michezo wa Mkoa wa Ruvuma Hassan Katuli alisema kuwa licha ya washiriki kujadili mada mbalimbali zilizopangwa zimejitokeza changamoto kadhaa

Katuli alizitaja changamoto hizo kuwa ni pamoja na kutokuwepo kwa mawasiliano kati ya Wizara Mama ya Michezo na Halmashauri,kubadilika kwa matumizi kwa viwanja vya michezo kuwa matumizi mengine bila kufuata taratibu husika

Alisema kuwa halmashauri kuwa na uhaba wa fedha za kulipia fidia hususani viwanja vya michezo na maeneo ya wazi,mwamko finyu wa halmashauri pamoja na jamii juu ya umuhimu wa michezo katika kujenga na kukua kijamii

Alieleza kuwa changamoto nyingine ni uhaba wa wataalamu wa kusimamia michezo(maafisa michezo)kuanzia ngazi ya kata na halmashauri,jamii kuwa na mwamko mdogo juu ya tasnia ya michezo kutoka ngazi ya familia hadi Taifa

Alisema pia kukosekana kwa warsha mbalimbali za kujadili michezo katika ngazi mbalimbali za Serikali,idadi ndogo ya washiriki hasa (Maafisa mipango Miji) kutokana na waandaaji kushindwa kugharamia malazi,chakula na nauli kwa washiriki

Akitoa mapendekezo kwa Serikali kutokana na changamoto hizo kwa niaba ya washiriki wote wa mafunzo hayo Afisa Mipango Miji Halmashauri ya Manispaa ya Iringa Wickriph Benda alisema kuwa wanasiasa waheshimu maoni na maamuzi ya wataalamu yanapotolewa kwa lengo la kukuza michezo nchini

Benda alisema kuwa kuwepo na mijadala,warsha mbalimbali kuanzia ngazi ya mtaa hadi Taifa juu ya umuhimu wa michezo,Serikali iajiri Maafisa michezo kuanzia ngazi ya kata,kuwepo kwa ushirikiano kati ya Wizara mama ya michezo,Tamisemi,Halmashauri na wadau mbalimbali wa michezo

Wizara mama ya michezo na halmashauri zitenge fedha kwa ajili ya kulipa fidia ya kutwaa ardhi ambayo itatumika kwa ajili ya viwanja,utaratibu wa kubadilisha matumizi ya ardhi ufuatwe kwa kufuata ushauri wa Maafisa mipango miji

Mwandishi wa Makala haya
Anapatikana kwa 0755-335051
Baruapepe;stephano12mango@yahoo.com