About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Friday, September 20, 2013

WAZIRI AMTISHA JK

Na, Betty Kangonga

WAZIRI wa Sheria na Katiba, Mathias Chikawe amemtisha Rais Jakaya Kikwete akisema kuwa endapo hatasaini muswada wa sheria ya marekebisho ya sheria ya mabadiliko ya katiba wa mwaka 2013, atakuwa ameingia kwenye mgogoro na Bunge.

Muswada huo uliopitishwa hivi karibuni na wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) pamoja na Augustine Mrema wa TLP (Vunjo), unapingwa vikali na vyama vya upinzani pamoja na makundi mbalimbali ambayo sasa yanamshinikiza rais asiusaini kuwa sheria.

Makundi hayo ambayo yamepata msukumo wa vyama vitatu vya CHADEMA, CUF na NCCR-Mageuzi ambavyo wabunge wake walikataa kuujadili muswada huo wakipinga uchakachuaji uliofanyika wa kuongeza vifungu na kutoishirikisha Zanzibar, tayari yametishia kwenda kortini ikiwa watapuuzwa.

Akizungumza jana na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Chikawe alisema kuwa ni vyema makundi mbalimbali yakaacha kumlaghai Rais Kikwete ili asiusaini muswada huo.

Kwa mujibu wa Chikawe, iwapo Rais Kikwete ataliafiki suala hilo la wapinzani na makundi mengine, na kuacha kutia saini muswada huo, atakuwa ametengeneza mgogoro na mhimili wa Bunge kutokana na chombo hicho kukamilisha kazi yake.

Alisema kuwa taratibu zote zilifuatwa kuhusiana na kupitishwa kwa muswada huo, na kudai kushangazwa na baadhi ya makundi yanayopiga kelele.

“Hao wanaolalamikia juu ya jambo hilo hawatendi haki kwani sheria zote zilifuatwa na hayo mapendekezo wanayotoa ya kutaka Rais Kikwete asitie saini sio sahihi hata kidogo, huko ni kutaka ‘kumblack mail’ na kumsababishia mgogoro na Bunge,” alisema.

Waziri Chikawe alisema kuwa ameshangazwa na baadhi ya matamshi yanayotolewa juu ya kuwepo kwa fujo au kumwagika damu na kusema jambo hilo haliwezi kufanikiwa kama halijapangwa.

“Fujo zinapangwa, hivyo wale wanaotaka kumwaga damu ni vyema wakajitaja na kusema kuwa ‘sisi tutamwaga damu’ kwa kuwa naamini damu haiwezi kumwagika yenyewe,” alisema.

Waziri huyo alisema kuwa ni vyema wale wanaotaka kuzunguka kwa wananchi na kufanya udanganyifu juu ya suala hilo, wangekubali kuwasilisha hoja hizo ndani ya Bunge na si mahali kwingine.
Kuhusu Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria kutopeleka muswada huo kwa wananchi wa Zanzibar, 

Chikawe alisema kuwa utaratibu uliotumika ni hisani tu, kwani hakuna sheria inayotaka muswada wa aina yoyote kupelekwa kwa Watanzania.

“Utaratibu wa kupitisha muswada huo sio huo tu, bali zipo njia nyingi ambapo anaweza kuandika anayohitaji na kuwasilisha kwa kamati ya Bunge na wapo waliofanya hivyo,” alisema.
Chikawe aliongeza kuwa inawezekana Kamati ya Katiba na Sheria ikawa na  sababu za kushindwa kuwafikia wananchi wote, lakini kwa upande wao walipokea maoni ya Serikali ya Zanzibar yaliyotolewa Mei 27, mwaka huu.

Alisema kuwa moja ya pendekezo lililotolewa na Serikali ya Zanzibar ni juu ya kuongezwa kwa siku 20 kati ya 70 zinazotakiwa kutumiwa na Bunge Maalumu la Katiba.
Chikawe alisema kuwa ni vyema yale yanayoenda kutolewa kwenye mkutano wa wapinzani kesho katika viwanja vya Jangwani, yangepelekwa bungeni kwa kuwa hata wakitoa katika viwanja hivyo haitasaidia.


ju