About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Sunday, August 14, 2011

MAHINDI HAYA ENDAPO YATAHIFADHIWA KWA MADAWA MAKALI KAMA VILE KIMATILA HUENDA YAKASABABISHA AFYA ZA WALAJI KUWA MATATANANI KUTOKANA NA SUMU KALI ILIYOPO KWENYE DAWA HIYO,HIVYO NI VEMA MAMLAKA HUSIKA IKACHUKUA HATUA MADHUBUTI KUKOMESHA HALI HIYO




WAKULIMA SONGEA WATUMIA MADAWA MAKALI KUHIFADHIA MAHINDI
Na Stephano Mango,Songea
WAKULIMA wa Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma wamekuwa wakitumia dawa ya aina ya Kimatila ambayo ni hatari kwa afya za binadamu kuhifadhia mahindi katika kipindi hiki cha msimu wa mavuno.

Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima  kwa kipindi cha mwezi mmoja umebaini kuwa dawa hiyo imekuwa ikitumika kuhifadhia mahindi ambayo wakulima huichanganya na mahindi ili yasiharibiwe na wadudu waharibifu

Tanzania Daima imefanya uchunguzi kwenye Vijiji vya Mpitimbi, Lyangweni, Peramiho, Sinai, Litapwasi na Mpandangindo na kubaini kuwa wakulima wamekuwa wakitumia dawa hiyo inayotumika kwenye zao la kahawa ili lisishambuliwe na wadudu na wao huweka  kwenye mahindi ili yasiliwe na wadudu.

Akizungumza na Tanzania Daima mmoja wa wakulima wanaotumia dawa hiyo kuhifadhia mahindi Pilimina Ngonyani Mkazi wa Kijiji cha Litapwasi anasema amekuwa akitumia dawa hiyo kwa miaka mingi ambapo anasema chupa moja ya dawa hiyo wanayonunua kwa Tsh.2000 wanaichanganya na lita 20 za maji na kuchanganya na mahindi kilo 300.

Mkulima mwingine Alfonce Hyera wa Mpitimbi anasema yeye amekuwa akitumia dawa hiyo kwa kuwa inauzwa bei rahisi na pia inatunza mahindi kwa muda mrefu bila kushambuliwa na wadudu ukilinganisha na dawa yenyewe ya kuhifadhia mahindi iitwayo Super Actellic Powder ambayo huuzwa Tsh.2500 ya unga ambayo huchanganywa na mahindi kilo 300.

Mkulima huyo anafafanua kuwa dawa ya kimatila hutunza mahindi kwa mwaka mmoja bila kushambuliwa na wadudu wakati dawa yenyewe ya kuulia wadudu Super Actellic Powder hutunza mahindi yasishambuliwe na wadudu kwa muda wa miezi sita.

Tanzania Daima iliongea na Boharia wa Wakala wa Hifadhi ya Taifa ya Songea Alfred Ndunguru ili kujua kama hifadhi ya chakula wanatumia dawa gani na wananchi wafanyaje ili mazao yao yawe salama na pasitokee madhara ya kiafya kwa binadamu.

Ndunguru alisema wao kama hifadhi wanatumia Dawa ya unga na maji (Actelic ) alisema utumiaji wake kuchanganya mahindi  kisha kupulizia kwa kutumia bomba maalum na vifaa kinga hewa isiwadhuru ambapo wakulima wao wanachanganya mbegu za mahindi kwenye dawa kwa kumwagia mahindi kienyeji kitu ambacho ni hatari kwa afya zao na za walaji.

Alibainisha zaidi kuwa mbegu ya mahindi ikilowanishwa kwenye dawa ina madhara kwasababu dawa itakuwa imepenya kwenye mahindi,hivyo hata mahindi yakikobolewa bado sumu ipo ndani ya punje ya mahindi , alishauri Serikali ione umuhimu kuliona hilo ili kunusuru maisha ya binadamu.

Alisema ni vema Wakuu wa Mikoa na Halmashauri zake zikatenga bajeti ya kutoa Elimu ya kutunza mazao kwa wakulima, mara baada ya mahindi kukauka yakiwa shambani na kuvunwa tayari kwa kuyahifadhi.

Naye Afisa Ubora msaidizi wa  Mazao wa hifadhi ya Chakula ya Taifa Ruhuwiko Songea Braison Henricki Kiama alisema mazao ya mahindi Mkoani Ruvuma hayana ubora hii ni kutokana na wakulima kuvuna mahindi yao kabla ya kukauka pia wanavuna mahindi na kuto yapepeta.

Alifafanua zaidi kuwa madhara ya kutopepeta kunasababisha mahindi yawe na fangasi wajulikanao kama Afratokisini pia inaweza kusababisha kansa kwa watumiaji wa mahindi kawaida yanatakiwa yawe yamekauka unyevu 13.00 mpaka 13.05 (moisture content).

MWISHO

Moja ya vyoo vinavyolalamikiwa na wanachuo na wakufunzi katika Chuo cha Ualimu Matogoro ambapo kama hatua za makusudi hazitachukuliwa huenda kukaibuka magonjwa ya mlipuko








CHUO CHA UALIMU SONGEA KIPO HATARINI KUPATA MAGONJWA YA MLIPUKO
Na Stephano Mango,Songea
WANACHUO wa chuo cha Ualimu Songea,Wakufunzi na wafanyakazi katika chuo hicho wapo katika hatari ya kupata magonjwa mbalimbali ya mlipuko ukiwemo ugonjwa wa kuhara,kipindupindu na magonjwa mengine ya hewa kutokana na uchafu wa vyoo chuoni hapa
 
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili katika chuo hicho umebaini kuwa kwa muda mrefu vyoo vya utawala vinaendelea kutumika inngawa vyoo hivyo havijafanyiwa ukarabati kutokana na uchakavu wake na kwamba hata mabomba ya maji katika vyoo hivyo hayafanyika kazi
 
Imebainika kuwa katika vyoo hivyo vya jikoni,dukani,utawala nje,utawala ghorofani vimekuwa chakavu na vimeandikwa kuwa vimefungwa kutoka na ubovu mkubwa lakini kutokana na uhaba wa vyoo chuoni hapo bado vinatumika
 
Uchunguzi uliofanywa katika vyoo vya madarasa ya mwaka wa pili Diploma,bweni la wasichana la Nyerere,mabweni ya Wavulana ya Aggrey,Mandela na Nkuruma vina hali mbaya sana na miuondombinu ya maji imechakaa na kusababisha utandu mkubwa wa uchafu katika sahani za vyoo hivyo
 
Vyoo vingi vimekutwa vikiwa na ndoo ambazo zimekuwa zikitumika kuwekea maji zikiwa tupu na karatasi zimekuwa zikizagaa chooni wakati vyoo hivyo vinapaswa kutumia maji badala ya karatasi
 
Kutokana na uchunguzi huo vyoo vingi chuoni hapo vimekutwa vikiwa vimebandikwa vikaratasi vinavyosomeka kuwa vyoo hivyo vimefungwa lakini kutokana na uhaba wa vyoo vimeendelea kutumika hali ambayo inaweza kuhatarisha afya za watumiaji
 
Uchunguzi umebaini kuwa vyoo hivyo vimekuwa vikisafishwa kwa nadra tena bila sabuni wala madawa maalum ya kusafishia hali inayopelekea kuwa na harufu kubwa kwa watumiaji wa vyoo hivyo na watu wanaoishi pembezoni mwa chuo na kusababisha adha kubwa
 
Juhudi za kumpata Mkuu wa Chuo hicho hazikuzaa matunda kwa madai kuwa uongozi wa Chuo na viongozi wa Chama cha Walimu wa Wilaya Manispaa ya Songea walikuwa wamejifungia ndani kutokana na mgomo wa wakufunzi unaoendelea chuoni hapo
MWISHO


MBUNGE WA JIMBO LA MBINGA MAGHARIBI KAPTENI JOHN KOMBA AKIZUNGUMZA NA WAHANGA WA KIMBUKA KATA YA MBAHA AMBAPO ALITOA MSAADA WA MABATI 500 YENYE THAMANI YA SHILINGI MILIONI 7.5



MOTO WATEKETEZA NYUMBA YA MBUNGE  KAPTENI KOMBA
Na Stephano Mango,Songea
MOTO umetekeza nyumba ya mbunge wa jimbo la Mbinga Magharibi mkoani Ruvuma Kapteni John Komba na kusababisha mtu mmoja ambaye ni mfanyakazi wa benki ya wananchi Mbinga(MCD) Emmanuel Kumbulu(38) kujeruhiwa vibaya wakati akijaribu kujiokoa.
Baadhi ya wakazi wa kijiji cha Lituhi akiwemo kaimu Afisa mtendaji wa kata ya Lituhi Joseph Chawala amewaambia waandishi wa habari jana kwa njia ya simu kuwa taarifa ya tukio hilo ilimfikia majira ya saa 11 alfajiri leo na alipofika nyumbani kwa kapteni komba alikuta nyumba ikiendelea kutektea kwa moto.
Chawala alisema kuwa jitihada za kuzima moto huo hazikuweza kufanikiwa kwa sababu ya vifaa duni vilivyokuwa vikitumika kuzima moto na kukosekana kwa huduma ya kikosi cha zimamoto kumechangia nyumba hiyo kuteketea.
Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu tukio hilo kamanda wa polisi wa mkoa wa Ruvuma Michael Kamuhanda amethibitisha kuungua kwa nyumba hiyo iliyoko katika kijiji cha Lituhi wilayani Mbinga ambayo ni mali ya mbunge Kapteni John Komba.
Kamanda Kamuhanda amesema kuwa chanzo cha moto huo ni betri za umeme jua(sola) zilizokuwa zikitumika kutoa nishati ya umeme kwenye nyumba na nyingine zikiwa zimehifadhiwa kwenye moja ya vyumba cha nyumba hiyo ambazo zilipata hitilafu na kusababisha moto ulioteketeza nyumba yote na mali zilizokuwemo.
Akizungumzia kuhusu thamani ya nyumba na mali zilizoteketea kwa moto Kamuhanda amesema thamani bado haijajulikana bali kinachojulikana ni kuwa nyumba imetekea na kila kitu kilichokuwemo ndani na thamani yake itajulikana baada ya mawasiliano na mmiliki wa nyumba hiyo kapteni komba.
 Naye mkuu wa wilaya ya Mbinga kanali mstaafu Edmund Mjengwa akizungumza na waandishi wa habaro kwa njia ya simu kuhusu tukio hilo amesema kuwa yuko safarini mkoani Mbeya na taarifa ya ajali hiyo ameipata baada ya kupigiwa simu na uongozi wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga.
Amesema kuwa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya itakutana kujadili tukio hilo ili kuweza kupata taarifa sahihi na chanzo cha ajali hiyo ya moto iliyoteketreza nyumba na mali zote za mbunge huyo.
 Kwa upande wake Mbunge wa jimbo la Mbinga Magharibi Kapteni John Komba alipoulizwa kwa njia ya simu alithibitisha kuteketea kwa nyumba yake na mali zilizokuwemo na kusema kuwa taarifa ya tukio hilo imemkuta akiwa Mbamba bay alikokuwa amekwenda kwenye ziara ya kuwasuhukuru wapiga kura wake kwa kumchagua.

Wakati Taifa likijiandaa kusherekea MIAKA 50 ya UHURU wakina Mama hawa wanapepeta pumba za Mpunga katika eneo la Bombambili Mjini Songea kwa ajili ya kupata chenga za Mchele ili waweze kupata chakula cha kujikimu,wakina mama hao wanalazimika kufanya kazi kwa Wafanyabiashara mbalimbaliza kuanika Mpunga,kuanua na kupeleka mashine ambapo mshahara wao ni kuzoa pumba na kuondoka nazo








MIAKA 50 YA UHURU UMASKINI WA KIPATO UMEONGEZEKA MARA DUFU
Na Stephano Mango,Songea
WATANZANIA wamebakiza siku chache kusherehekea miaka 50 ya uhuru wa nchi yao baada ya kuupata disemba 9,1961 wakati huo nchi ikijulikana kwa jina la Tanganyika kabla ya kuungana na Visiwa vya Zanzibar

Mwaka huu Tanzania inasherehekea miaka hiyo baada ya waliokuwa viongozi wenye uzalendo stahiki wa taifa hilo changa walipofanikiwa kuwaondoa wakoloni wa Kiingereza kwa njia ya mazungumzo na kuwaacha watanzania wajiendeleze wenyewe

Katika hilo hatuwezi kumsahau muasisi wa mazungumzo ya amani na kiongozi mzalendo wa kwanza wa taifa hili,Baba wa taifa hayati Mwalimu Julius Nyerere aliyepigania haki za Watanzania kabla na baada ya uhuru bila ya kumwaga damu

Kwa mantiki hiyo kamusi ya Kiswahili sanifu,tolea la pili la mwaka 2004 iliyotolewa na Taasisi ya uchunguzi wa Kiswahili Dar es Salaam inatafsiri neno uhuru kama hali ya kutotawaliwa na mtu au nchi nyingine na pia inafafanua ni hali ya kufanya mambo bila kuingiliwa

Kupitia tafsiri hii waasisi wa taifa letu walipigana dhidi ya utawala wa kikoloni ili kutuondoa katika hali ya kutawaliwa na wazungu sehemu zote yaani kiuchumi,kisiasa na kiutamaduni ambapo jambo hili lilifanikiwa na kumdhihilishia aliyekuwa mtawala wetu kwamba tuko tayari kujitegemea

Licha ya kusherehekea miaka hiyo kuna haja ya kujihoji kwa kina kama neno uhuru lilivyotafsiriwa kwenye kamusi tajwa hapo kwani binafsi nafikiri kuwa maana ya uhuru inapoteza maana yake kwani hali ya maisha ya watanzania inadhihirisha jambo hilo

Watanzania wanaamnini kuwa hawako huru kwani watawala wanakazana kuwarudisha kwenye mfumo rasmi wa ukoloni tuliokuwa nao awali kabla ya kukombolewa na waasisi wa taifa hili miaka 50 iliyopita

Iliamini kuwa Taifa letu lina rasilimali nyingi sana ambazo zingetumika kuliendeleza taifa kiuchumi,kielimu,kisiasa na kiutamaduni ili wananchi wake wawe na maendeleo stahiki kutokana na kufaidi rasilimali zao

Badala yake nchi yetu kutokana na mipango mibaya inayotungwa na watawala wetu ambao kimsingi wanapaswa kuitwa wakoloni weusi imebaki ikiwa omba omba wa kila kitu kutoka kwa wakoloni weupe ambao ndio tuliowanyang’anya nchi ili tuweze kujitawala wenyewe

Wengi sasa tunaamini kuwa uhuru tulio nao ni ule wa kupandisha bendera ya taifa yenye rangi nne na kuimba wimbo wa taifa wa mungu ibariki Tanzania kutoka na viongozi wetu tulio wapa dhamana kutuongoza kuuza nchi vipande vipande na kutegemea misaada kutoka kwa wakoloni ambao walifukuzwa na waasisi wetu wakati wakidai uhuru

Jambo hilo halihitaji kuomba muongozo kwa mtu yoyote yule kwani inajidhihirisha waziwazi kwa kila mtanzania ambaye anapumua vizuri kutokana na uhai alionao kwani ukitathimini uchumi wan chi yetu utagundua wazi kuwa unamilikiwa,kuendeshwa na mataifa ya nje

Watanzania wamebaki wakiduwaa kutokana na mifumo mibovu ya nchi inayowaacha wananchi wake wakishangaa na kushindwa kujinasua katika shughuli zao za uzalishaji mali kutokana na sera mufilisi zinazowabana wananchi na kupelekea kuvipuuza vitu vinavyozalishwa na watanzania

Kutokana na mifumo hiyo mibovu wafanyabiasha kutoka nje ya nchi wanapewa fursa nyingi katika nchi yetu nasi tunakuwa watumwa katika shughuli zao huku za kwetu zikiendelea kudharauliwa kwa maneno kadha wa kadha

Ndio maana nchi yetu leo inategemea bidhaa nyingi kutoka nchi mbalimbali duniani kama vile mchele tunategemea kutoka Thailand,mafuta kutoka Kenya,nyama Afrika kusini,kijiko,sahani,nguo,viatu kutoka China na bidhaa zingine kutoka nchi nyingine nyingi

Jambo hilo linaendelea kuwatesa wananchi katika lindi kubwa la umasikini wa kipato kutokana na bidhaa zao wanazozalisha zinakosa soko kunakosababisha na ukosefu wa masoko stahiki kwa sababu ya mifumo nyanyaji kwa watanzania iliyowekwa kwa makusudi na viongozi wetu

Licha ya kusherehekea miaka hiyo 50 ya uhuru bado watanzania wengi wanakabiliwa na umasikini wa kipato ingawa Serikali imekuwa na mipango na mikakati mingi mfu katika kukuza uchumi wa nchi na kupunguza umaskini

Kwani tafiti nyingi zinazoendelea kufanya na wadau mbalimbali zinaendelea kuonyesha wazi kuwa hali ya maisha ya mtanzania ni mbaya sana kiuchumi kwani wapo baadhi yao wanatumia chini ya shilingi mia 600 kwa siku kutokana na ugumu wa upatikanaji fedha

Rekodi zinaonyesha kuwa uchunguzi wa bajeti ya kaya wa mwaka 2007(2007 Household Budget Survey-HSB) unaonyesha kuwa umaskini umepungua kidogo sana toka asilimia 38.6 mwaka 1990,asilimia 35.7 mwaka 2001 mpaka asilimia 33.3 mwaka 2007

Kwa kuwa idadi ya watanzania inaongezeka kwa asilimia 2.9 kila mwaka na idadi ya watu maskini imeongezeka kwa milioni moja na nusu toka watu milioni 11.4 mwaka 2001 na kufikia watu milioni 12.9 mwaka 2007

Izingatiwe kuwa kigezo kilichotumiwa na HBS 2007 cha mtu mzima kutohesabiwa kuwa siyo maskini ni kutumia shilingi 641 au zaidi kwa siku akiwa Dar es Salaam,shilingi532 au zaidi kwa siku akiwa katika miji mingine na shilingi 469 au zaidi akiwa vijijini

Ni wazi kigezo ni cha chini mno na bado idadi ya watu maskini imeongezeka kwa mujibu wa hotuba ya bajeti ya kambi ya upinzani bungeni mwaka huu wa 2011 kwani kigezo kilichokubalika kimataifa kuwa matumizi ya chini kabisa kwa mtu mzima asihesabiwe kuwa ni maskini wa kutupwa ni dola moja kwa siku

Benki ya dunia inakadiliwa kwa kutumia kipimo hiki umaskini Tanzania umeongezeka toka asilimia 73 ya watanzania wote mwaka 1990 mpaka kufikia asilimia 89 mwaka 2000 na kwamba kwa kutumia kigezo hicho hicho takwimu za uchunguzi wa bajeti ya kaya wa mwaka 2007 zaidi ya watanzania 90 katika kila watanzania 100 ni maskini wa kutupwa

Katika hilo ikumbukwe kuwa taifa letu mara baada ya kupata uhuru lilikuwa na ndoto kuu tatu ambazo ni kutokomeza ujinga,umaskini na maradhi jambo ambalo miaka 50 ya uhuru limeshindwa kutekeleza ndoto hizo kwani kutimizwa kwa ndoto hizo kungefanya kuwa taifa lililoendelea na linalojitegemea

Tunapokumbuka na kuthamini mchango wa wale wote waliotimiza wajibu wao wakati huo wa kupigania uhuru,tunapaswa kuamini kuwa nasi tunaweza kuutimiza wajibu wetu kama funzo katika kukabiliana na changamoto za leo na kesho ili taifa letu lisitopee kwenye utumwa

Taifa tulilonalo leo si lile la wakati wa uhuru ni wazi kuwa limepiga hatua kijamii,kisiasa,kiuchumi,amani,umoja na mshikamo miongoni mwa wananchi ni vielelezo vya baadhi ya mafanikio ambayo taifa limepata na kuyadumisha tangu uhuru

Ingawa hatua tuliyopiga kimaendeleo kama taifa haiwiiana hata kidogo na uhuru wetu wa miaka 50 kwani maendeleo yetu yamekuwa yakisuasua na maliasili za nchi zimekuwa zikipukutika kwa kasi kubwa kwa kiasi kikubwa tumeshindwa kuutumia uhuru wetu kupunguza umaskini

Kwani Tanzania ni moja ya nchi 10 zilizo maskini kabisa duniani kwa kipimo cha kimataifa cha umaskini kwani asilimia 57.8 sawa na watu milioni 20.2 wanaishi chini ya dola moja kwa siku na asilimia 89.9 sawa na watu milioni 31.5 wanaishi chini ya dola mbili kwa siku

Hali hiyo inatisha kwani hatuwezi kuwa na mshikamano wa kweli wa kitaifa ikiwa ukuaji wa uchumi unawanufaisha watu wachache na kuwaacha zaidi ya watanzania milioni 36 wakiwa maskini wa kutupwa

Takwimu zinaonyesha kuwa watanzania wenye lishe duni na utapiamlo wameongezeka toka asilimia 28 ya watanzania wote mwaka 1990 na kufikia asilimia 41 mwaka 1995 na kupungua kiasi kufikia asilimia 35 mwaka 2007

Miaka 50 ya uhuru ni aibu kuona  watu wanaolala na njaa wakiongezeka kila siku iendayo kwa mungu kwani wameongezeka toka milioni 7.4 mwaka 1990 na kufikia milioni 14.4 mwaka 2007 wakati rasilimali zao zikitumika ipasavyo wangeweza kuisha maisha mazuri na kufanya taifa kuwa na ustawi stahiki

Kutokana na kasi yetu ndogo ya maendeleo,tafiti zinakadilia kwamba kwa kasi ya sasa ya ukuaji wa uchumi kwa asilimia sita kwa mwaka,italichukua taifa miaka 18 zaidi kuweza kuwanyanyua wananchi kutoka kwenye wastani wa kipato cha chini ya dola moja kwa siku hadi kufikia dola mbili za Marekani kwa siku

Tunapaswa kuelewa kwamba kama tutashindwa kuchukua maamuzi sahihi na hatua madhubuti katika kuchochea uwajibikaji na ufanisi hata baada ya miaka 18,bado watanzania watakuwa maskini kwani hawataweza kujikimu kikamilifu kutokana na mifumo mibovu ya utawala inayoachilia mfumuko wa bei katika bidhaa mbalimbali

Ili ndoto ya uhuru itimie kuna haja ya msingi ya kuutazama upya mfumo wetu wa utawala,kujua ni kwanini umeshindwa kutuwekea mazingira ya kutupatia maendeleo ya haraka

Licha ya kuwa na rasilimali za kutosha na uhuru wa miaka 50 kwani inaaminika wazi wazi kuwa Tanzania huru yenye maendeleo na inayojitegemea  inawezekana endapo kila moja wetu akitimiza wajibu wake

Mwandishi wa Makala haya
Anapatikana simu 0755-335051
Barua pepe;stephano12mango@yahoo.com