About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Thursday, March 15, 2012

RC MANYANYA AWAPONGEZA MADAKTARI WA RUKWA KWENYE KIKAO CHA KAMATI YA USHAURI YA MKOA

Na, Stephano Mango, Rukwa
MKUU wa Mkoa wa Rukwa Mhandisi Stella Manyanya amewapongeza Madaktari  na wauguzi wote nchini  ambao walifanya kazi zao kwa umakini mkubwa na uadilifu katika kipindi chote cha mgomo wa kwanza na wa pili ulioitishwa na chama cha Madaktari Tanzania (MAT) na kumalizika hivi karibuni
Akizungumza jana kwenye kikao cha Kamati ya mkoa wa Rukwa kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi ya Mkuu wa mkoa huo alisema kuwa Madaktari na wauguzi wa Rukwa wametujari na kutuheshimu sana
Mhandisi Manyanya alisema kuwa wanataaluma hao wamejari uhai wa watanzania wenzao kwa kudiriki kufanya kazi yao ya kuwatibu wagonjwa na kutoa huduma stahiki za kiafya bila kinyongo wakati wenzao wakiwa kwenye mgomo
Alisema kuwa kitendo chao cha kuwajali  wananchi katika kipindi hicho kigumu hivyo , mkoa unajipanga ili kuona namna bora ya kuwapongeza Madaktari na wauguzi wa mkoa wa Rukwa kwa heshima na utu waliouonyesha katika wakati huo na sasa ambapo mgomo nchi nzima umemalizika
Alieleza kuwa wakati wa mgomo maeneo mengine huduma zilisitishwa na kupelekea watu wengi kupata usumbufu, ulemavu wa maisha, vifo na madhara mengine mengi hali ambayo imelitia doa Taifa hili ambalo linajali misingi ya haki za binadamu
"Watanzania tunapaswa tuimarishe maadili ya kazi zetu na kujali utu wa binadamu kwani inasikitika Madaktari na wauguzi wanashindwa kuwahudumia wagonjwa na badala yake wanaendekeza mgomo wenye maslahi binafsi huku wakiwaacha wagonjwa wakifa kwasababu ya kushindwa kumaliza madai yao kwa njia ya kukaa mezani"alisema Mhandisi Manyanya
Alifafanua zaidi kuwa haki ya kuishi ni haki kubwa kuliko zote na kwamba hakuna mtu mwenye mamlaka ya kuondoa uhai wa mwenzake kwa sababu yoyote ile kwani mwenye uwezo na mamlaka hayo ni mwenyezi mungu peke yake ni vema kazi yake tukamuachia yeye
Aliesema kuwa mkoa wa Rukwa unampongeza Rais Jakaya Kikwete kwa kumaliza mgomo huo wa Madaktari nchini na kuahidi kutekeleza baadhi ya madai yao  hilo ndilo jambao ambalo watanzania wengi walikuwa wanarisubiri kutokana na kuchoka kwa madhara yaliyokuwa yanajitokeza kutokana na mgomo huo ,hivyo Madaktari wale waliogoma warejee kazini na kuendelea na kazi wakati madai yao yanafanyiwa kazi na Serikali
MWISHO

KIKAO CHA KAMATI YA USHAURI YA MKOA WA RUKWA CHAMALIZIKA KWA KUWEKA MIKAKATI MBALIMBALI YA MAAZIMIO

 Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhandisi Stella Manyanya akitoa hotuba ya ufunguzi wa kikao cha RCC

HOTUBA YA UFUNGUZI YA MKUU WA MKOA WA RUKWA INJINIA STELLA MANYANYA KWENYE KIKAO CHA KAMATI YA USHAURI YA MKOA WA (RCC) TAREHE 14/ 03/ 2012

Mhe. Mwenyekiti wa CCM, Ndugu H. Matete,
Katibu Tawala wa Mkoa, Ndugu Salum M. Chima,
Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa,
Waheshimiwa, Wakuu wa Wilaya,
Bibi Joyce Mgana,
na Dr.
Rajabu Lutengwe,
Wah. Wabunge,
Meya, na Wenyeviti wa Halmashauri zote za Mkoa wa Rukwa,
Wakurugenzi,
Wakuu wote wa Idara,
Wageni Waalikwa,
Mabibi na Mabwana.
Rukwa Ruka!, Sumbawanga Ng’ara!
·        Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuweka hai.
·        Pili napenda kuwakaribisha katika Kikao hiki, na poleni kwa safari kwa wale mliotoka mbali.
Nachukua pia nafasi hii kuwakaribisha watumishi wageni wote waliohamia katika Mkoa wetu katika kipindi cha kuanzia Oktoba mpaka leo.  Ni imani yangu kuwa wataungana na viongozi, pamoja na watumishi wenzao kuhakikisha kuwa Rukwa inaruka na Katavi inaimarika zaidi.

Waheshimiwa wajumbe,
Nichukue pia nafasi hii kwanza kuwashukuru sana ninyi Wajumbe kwa niaba ya wananchi wote kwa jinsi tulivyoshirikiana katika matukio yote makuu na ya muhimu katika Mkoa wetu wa Rukwa na Katavi.  Naishukuru sana Kamati yangu ya Ulinzi na Usalama, Chama cha CCM na Vyama vya Siasa, Wakuu wa Idara mbalimbali, Watumishi wote, Wafanyabiashara, Wawekezaji na Wananchi wote kwa ujumla, kwa kufanikisha shughuli hizo kwa umakini mkubwa.
Shughuli kuu zilizofanyika ni pamoja na:-
1.      Kongamano la Uwekezaji la Ukanda wa Ziwa Tanganyika ambalo lilifanyika tarehe 17/10/2012 mjini Mpanda, Kongamano hilo lilifunguliwa na Mgeni wetu rasmi Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  Waliohudhuria wengine ni pamoja na Mheshimiwa Mizengo Peter Pinda Mbunge wetu, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mary Nagu, Waziri wa Uwezeshaji na Uwekezaji katika Ofisi ya Rais, Mabalozi 34 kutoka nchi mbalimbali, Wakuu wa Mikoa 3 kutoka Kigoma, Mheshimiwa Issa Machibya, ambaye pia alikuwa muandaaji wa Kongamano, Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mheshimiwa Fatma Mwase, na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Mheshimiwa Joseph Simbakalia, pia Wadau mbalimbali wa makampuni na mashirika ya umma, na kwa namna ya pekee wananchi wenyewe.
Kwa upande wa Vyama vya Siasa, Chama Tawala CCM chini ya Mwenyekiti wake wa Mkoa Ndugu H. Matete walishiriki, pamoja na Chama cha Chadema.
2.      Mapokezi ya Mwenge yalifanyika kwa ufanisi mkubwa.
3.      Tulifanya Tamasha la Wana Rukwa na Katavi kuanzia tarehe 25 – 27/11/2011 katika kijiji cha Makumbusho Jijini Dar es Salaam. 
Tamasha hilo lilifana sana, hivyo napenda kuwapongezeni wote mlioshiriki katika kuandaa tamasha hilo, wakiwemo wazee wa mila, Viongozi wa Serikali pamoja na Wafanyabiashara wetu, na nimtaje ndugu Sumri kwa kutuweka vizuri kiusafiri

Aidha, nawashukuru na kuwapongeza sana Wana Rukwa na Katavi, waishio Dar es Salaam, chini ya Mwenyekiti Bibi Mwangaza Mwanisongole kwa kufanikisha tamasha hili kwa kiwango kikubwa.
Tamasha hili lilifunguliwa na Mheshimiwa Dkt Mohammed G. Bilal Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kufungwa na Mheshimiwa Mizengo Peter Pinda (Mb) na Waziri Mkuu.
4.     Miaka 50 ya Uhuru tuliadhimisha mjini Namanyere katika Halmashauri ya Wilaya ya  Nkasi 9/12/2011.
5.     Tulipata Mgeni, ambaye ni Makamu wa Rais Dkt Mohammed Gharib Bilal kuanzia tarehe 18 – 24/2/2012 katika mikoa yetu ya Rukwa na Katavi.  Ziara yake ilikuwa ya mafanikio makubwa kutokana na ushirikiano mkubwa kati ya Chama Tawala na Serikali, Vyama vingine vya Siasa pamoja na wananchi wote waliohudhuria kwa wingi kwenye mikutano, kwa utulivu na heshima kubwa.  Nawashukuruni sana.
6.  Maadhimisho ya siku ya Wanawake duniani yalifanyika tarehe 8/3/2012 Mjini Sumbawanga, na yalikuwa mazuri.
         Pamoja na taarifa hizo ili ngoma inoge kuna wenyewe, hivyo basi nawashukuru sana Waandishi wa habari wa Mkoa wangu wa Rukwa pia Katavi pamoja na rafiki zao wa vyombo mbalimbali kwa jinsi wanavyotuunga Mkono na kuisaidia serikali ya Mkoa wa Rukwa, na taifa kwa ujumla. Pia navishukuru vikundi vya ngoma.
Mambo mengine muhimu.
1.   Barabara zetu zinaendelea kujengwa vizuri kwa kiwango cha lami, japo katika zile tunazogharimia sisi wenyewe (Serikali ya Tanzania) zinakabiliwa na upungufu wa fedha kutokana na majukumu mbalimbali ya serikali ikiwemo umeme, madeni ya watumishi kama Madaktari, Walimu n.k.
2.   Mkoa umeanzisha mpango wa Sumbawanga Ng’ara tuuunge mkono pamoja na Halmashauri zote zing’are.
3.   Napenda kuwataarifu kuwa madaktari wetu wa Mkoa wa Rukwa pamoja na wauguzi wote wa Mkoa wetu kwa kweli hawakugoma kabisa katika migomo yote miwili.  Wametujali sana wana Rukwa, na wametupa heshima kubwa sana na wamethamini sana uhai na maisha yetu.  Mkoa utaangalia namna bora zaidi ya kuwapongeza. Lakini kwa kuanzia naomba niwapongeze wote katika Kikao hiki.
Kwa namna ya pekee nakiomba kikao hiki kiazimie pongezi kwa Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi alivyoshughulikia mgomo huu wa madaktari na kwa kuridhia kutupatia Mkoa mpya wa Katavi baada ya Mkoa wetu kugawanywa.
Waheshimiwa wajumbe, kutokana na ukubwa wa jiografia na maumbile ya Mkoa wetu tunashauri kuwa serikali ione uwezekano wa kuongeza ukomo wa bajeti.  Na kwa vile Mkoa wa Rukwa umegawanywa, basi ni vema Mkoa wa Rukwa uendelee na ukomo wa zamani na Mkoa wa Katavi upewe ukomo mpya. 
Waheshimiwa wajumbe, katika kuandaa bajeti ya mwaka huu kama ilivyoelezwa na Katibu Tawala wetu ndugu Chima, Mkoa unaazimia kuweka kipaumbele katika kumaliza miradi iliyopo na kuwa na miradi michache ili ikamilike na kutoa matukio badala ya kuwa na miradi mingi isiyoisha.  Hali hiyo ni kuharibu fedha kidogo tunayopata bila kupata matukio mazuri.
Waheshimiwa wajumbe tunayo mengi ya kujadili, muda hautoshi, na naona hali ya RAS wetu kimfuko ni mbaya, lakini kikao hiki ni muhimu sana ikizingatia kuwa ni dira ya bajeti.  Naomba tuchangie kwa makini ili kuufanya mkoa wetu uruke.
Kikao kimefunguliwa

 Baadhi ya wajumbe wa kikao hicho, Ignas Malocha Mbunge wa Jimbo la Kwela, Ally Kessy Mbunge wa Jimbo la Nkasi Kaskazini, na Suleiman Kakoswe Mpanda Vijijini wakifuatilia kikao hicho.
 Baadhi ya wajumbe na wageni waalikwa wa kikao hicho wakisikiliza neno la ufunguzi wa kikao hicho likitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhandisi Stella Manyanya (hayupo pichani).

Meneja wa Sido Mkoa wa Rukwa Martin Augustino Chang'a akiwa anafuatilia kwa umakini kikao hicho. Wengine ni baadhi ya wataalamu katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Rukwa.