About


Karibu ujiunge na chuo cha kisasa cha Easy Tech.Computer kwa mafanikio yako,Walimu waliobobea katika fani hiyo wanapatikana chuoni hapo

elimak

elimak

Pages - Menu

Monday, January 17, 2011

Mhandisi Manyanya wapili kulia akiwa na Balozi wa Sweden aliyemaliza muda wake Nchini Tanzania Staff Herrstom (aliyevaa mgolole)

DK. GAMA MWANADIPLOMASIA, MWANASIASA ATAKAYEKUMBUKWA DAIMA.


DK. GAMA MWANADIPLOMASIA, MWANASIASA ATAKAYEKUMBUKWA DAIMA.

Na Stephano Mango, Songea.

Disemba 16 mwaka huu tunatimiza mwaka mmoja tangu Tanzania iondokewe na mwanasiasa mahili kiongozi shupavu na mwana michezo maarufu Dk. Lawrence Mtazama Gama.

Kuna mengi ambayo watu wanaweza kumzungumzia mtanzania mwenzetu huyo ambaye alifariki dunia Disemba 16 mwaka 2009 kutokana na maradhi ya kansa ya mapafu katika hospitali ya Agha khan Jijini Dar es salaam.

Mwili wa marehemu Dk. Gama ulisafirishwa toka Dar es salaam hadi Songea na kupelekwa kijijini kwake Amani makoro Wilayani Mbinga Mkoani Ruvuma ambako alizikwa Disemba 20, 2009 ambapo msiba mazishi hayo yaliudhuriwa na maelfu ya watu akiwemo Rais Jakaya Kikwete na viongozi wa kada tofauti hapa nchini.

Inaaminika kuwa kifo ni njia ambayo mwanadamu yeyote duniani hawezi kukiepuka ndio maana vitabu vitakatifu vya kidini vinakielezea kifo kwa kukifananisha na dhoruba.

Kwamba kinakuja ghafla, muda wowote na hakuna ajuaye siku wa saa ambayo kifo kitamuondoa hapa duniani hii inamaana kuwa binadamu hana mawasiliano na ujio wa kifo.

Kifo cha Dk. Gama kilionekana kuwagusa watu wengi wa kada tofauti kutokana na kazi kubwa aliyoifanya katika kipindi cha uhai wake katika nyanja za michezo, elimu,utamaduni, siasa na uchumi.

Oliver Mhaiki ambaye ni katibu mkuu Wizara ya sheria na katiba anamwelezea Dk. Gama kuwa alikuwa ni mtu mwenye hekima na upendo wa hali ya juu katika maisha yake kwani hakuwa mtu wa kukurupuka  katika kujadili jambo.

Kila wakati alikuwa akisikiliza kwa umakini na kujenga hoja anapozungumza jambo la msingi na kudhihirisha uzalendo wake halisi kwa Taifa letu.

Alikuwa akichukia kwa nguvu zake zote vitendo vya ufisadi na watu wanaopewa nafasi za uongozi kujilimbikizia mali badala ya kuwatumikia wananchi

Huyo ndiye Dk. Lawrence Gama kisima cha maarifa, taaluma na ushauri kilichokauka ilhali watu bado wanahitaji kuendelea kuchota hekima na busara zake ambaye tulimpenda lakini mwenyezi Mungu alimpenda zaidi.

Mhaiki anasema, Dk. Gama atakumbukwa kwa mengi aliyoyafanya katika enzi ya uhai wake, katika kuboresha mawasiliano , Dk. Gama alisimamia kikamilifu ujenzi wa barabara ya lami kutoka makambako hadi Songea katika miaka ya 1980s.

Usafiri wa Songea hadi Dar es salaam ulikuwa ni zaidi ya siku mbili na sasa hutumia masaa 12, ambapo jitihada hizo pia zimesaidia kuongeza wawekezaji wa ndani na nje katika Mkoa na hivyo kuongeza ustawi wa wananchi wa Mkoa wa Ruvuma.

Dk. Gama akiwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma atakumbukwa katika uhamasishaji wa viongozi na wananchi katika kujiletea maendeleo.

Alikuwa kiongozi na muandaaji wa mpango mkakati wa maendeleo ya Mkoa kupitia agizo la mlale mwaka 1977 lililoainisha fursa na vikwazo, changamoto na mikakati ya kupambana na umasikini ulioukabili Mkoa wa Ruvuma .

Mhaiki anasema, mkazo mkubwa wa agizo hilo uliwekwa katika kuboresha kilimo ambapo kwa sasa ni kilimo kwanza na matokeo ya jitihada hizo Mkoa uliweza kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara.

Toka wakati huo Mkoa wa Ruvuma ulipoingizwa kwenye orodha ya Mikoa minne(4) ya awali iliyoongoza katika uzalishaji wa mazao ya chakula yakiwemo mahindi nay a  biashara ( The big four) inaendelea kushikilia hadi saa.

Dk. Gama alitambua kuwa ustawi wa familia (kaya) huanzia katika kuwepo na makazi bora, hivyo alihamasisha wananchi kujenga nyumba bora kwa kutumia matofali ya kuchoma na hadi sasa ni wastani wa asilimia 70 ya wananchi wanaishi katika nyumba bora.

Marehemu Dk. Gama alikuwa kiongozi shupavu na mkereketwa wa maendeleo na atakumbukwa  kwa mengi na watanzania na wananchi wa Ruvuma kwa ujumla kwani alifanikiwa kuacha alama ambazo hazifutiki kamwe.

Mhaiki anasema, Dk. Gama alikuwa akifanya kazi kwa vitendo na si kwa maneno tu au mwenye kudandia mafanikio ya wengine  na kuyatumia kujiimarisha kiuongozi au kisiasa kama viongozi na wanasiasa wengi wa leo wanavyofanya.

Bali Dk. Gama enzi za uhai wake amefanya mambo mengi na kuuweka Mkoa wa Ruvuma kwenye mafanikio makubwa katika sekta ya kilimo,michezo,utamaduni,elimu,afya na uchumi.

Kwani enzi za uhai wake akiwa kiongozi wa kwa nyadhifa tofauti na kutambua umuhimu wa afya ya binadamu alifanikiwa kushawishi upatikanaji wa fedha na kuhamasisha ujenzi wa hospitali ya Mkoa wa Ruvuma , kituo cha afya cha mji Mwema, na Zahanati zingine nyingi.

Enzi za uhai wake Dk Gama alishiriki kikamilifu katika ujenzi wa barabara za lami ndani ya mji wa Songea , Soko kuu la Songea ambalo hapo awali liliungua moto na kusimamia ujenzi wa soko jipya na la kisasa, masoko madogomadogo ya Bombambili, Manzese, Lizaboni ,Mfaranyaki na Majengo .

Marehemu Dk. Gama licha ya kuwa msomi mwenye kiwango cha shahada  ya uzamili (Ph. D) alikuwa tegemeo kubwa kwa wanajamii wa Mkoa wa Ruvuma na Taifa kwa ujumla kwani hilo linajidhihirisha kutokana na mchango mkubwa alioutoa katika medani za elimu, uongozi na ushauri wa kitaaluma kwenye fani mbalimbali,

Kwani alifanikiwa kuhamasisha ujenzi wa shule nyingi za msingi na sekondari kwa kuzitaja chache ni shule ya msingi Misufini, Kitanda, Lugongolo, Bombambili, Majengo, Samora, na nyingine nyingi ambapo shule za sekondari ni Msamala, Ruvuma,Makita,Londoni,Karembo,Mletele,na nyingine nyingi.

Pia alifanikiwa kujenga ofisi mbalimbali za serikali na taasisi zake ambazo mpaka leo zimekuwa ni alama tosha kwa kizazi kilichopo na kijacho katika kumuenzi marehemu Dk. Gama kwa mchango wake aliouonyesha enzi ya uhai wake.

Mhandisi Stella Manyanya ambaye ni Mbunge wa viti maalum Mkoa wa Ruvuma pia ni Mwenyekiti wa ushauri wa kamati ya Makumbusho ya Taifa ya Majimaji anamuelezea Dk. Gama  kama kiongozi aliyeonyesha njia kwa kufanya mambo mengi ambayo yanapaswa kuenzishwa na kuendelezwa kikamilifu.

Manyanya anasema, Dk. Gama alizaliwa na kulelewa na familia ya kichifu kwa maana wazazi wake walikuwa machifu walioheshimika sana na kabila la wangoni ambapo naye Dk. Gama alisimikwa kuwa chifu na baadaye alimkabidhi uchifu Exaveli Zullu kuwa chifu wa wangoni mpaka sasa.

Licha ya kuzaliwa , kulelewa na kusimikwa uchifu , Manyanya anasema Dk. Gama atakumbukwa na kuenziwa kwa mchango wake wa kuthamini mila,desturi na  tamaduni za kabila la wangoni.

Anasema Dk. Gama enzi za uhai wake aliwaenzi kikamilifu Mashujaa waliouawa wakati wa vita vya Majimaji kwani alifanikiwa kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa Makumbusho na kuhamasisha ujenzi huo uliokamilika mwaka 1980.

Pamoja na kukamilisha ujenzi wa jengo hilo la Makumbusho aliweza kuzijenga sanamu 12 za machidu wa kingoni, sanamu ya askari wa jeshi la wananchi wa Tanzania na sanamu ya Mwl. J.K. Nyerere.

Pia Dk. Gama kwa kushirikiana na Padri Chengula wa kanisa katoliki la Songea ambaye kwa sasa ni marehemu na baadhi ya wazee walifanikiwa kukusanya vifaa vilivyotumika kupigania wakati wa vita vya majimaji kutoka kwenye maeneo ya Maposeni, Matimila na Namanditi ambako kuna historia kubwa ya kabila la wangoni.

Manyanya anasema, vifaa vilivyo kusanywa ni Chikopa (ngao), Chibonga (rungu), Chinjenje (kishoka) jiwe lililotumika kusagia nafaka, nguo za magome ya miti na viti vilivyotumiwa na Chifu Mputa Gama ambapo vifaa hivyo vimehifadhiwa ndani ya jengo la Makumbusho ya Taifa ya Majimaji Songea na kuwa kivutio kikubwa kwa utalii wa kiutambaduni na kihistoria .

Katika sekta ya michezo , wadau wa michezo wanaendelea kumkumbuka Dk. Gama kwa ujenzi wa viwanja vya michezo vyenye ubora mkubwa nchini kama vile uwanja wa Majimaji , uwanja wa Zimanimoto uliopo Songea Mjini, uwanja wa Ally Hassani Mwinyi uliopo Tabora.

Dk. Gama ataendelea kukumbukwa kwa mipango yake ya kisanyansi aliyotumia kuanzisha timu mbalimbali na kuinua vipaji vya wachezaji vijana na kutengeneza timu zilizoleta ushindani mkubwa wakati huo ikiwemo timu ya Milambo ya Tabora chini ya wachezaji wake mahiri wakati huo Feruzi Telu , Jumanne Mikidadi, pamoja na wengine.

Timu ya Majimaji iliokuwa tishio wakati huo nchini na nchi jilani chini ya wachezaji wake mahiri Actavian Mrope, Peter Tino, Mchunga Bakari, Hussein Mwakakuruzo, Samli Ayub , Celistin Skinde Mbunda na wengineo .

Licha ya kushiriki katika kuleta maendeleo ya waruvuma na nchi kwa ujumla marehemu Dk. Gama atakumbukwa kwa michango yake aliyotoa aliposhika nyadhifa mbalimbali nchini .

Dk. Lawrence Mtazama Gama  alizaliwa Januari 19 mwaka 1935 katika kijiji cha Amani Makolo Wilayani Mbinga Mkoa wa Ruvuma na kubahatika kupata elimu katika vipindi tofauti, mwaka 1944 – 1947 alipata elimu ya msingi katika shule za likwambi -  Maposeni na Magagula  Wilaya ya Songea ambapo alihitimu masomo ya darasa la nne na mwaka 1948 – 1952 alipata masomo katika shule ya kati ( middle school) ya Peramiho.

Mwaka 1953 – 1954 alipata elimu ya sekondari katika shule ya Ndanda iliyopo Wilayani Masasi Mkoani Mtwara na mwaka 1969 alijiunga na chuo kikuu cha Dar es salaam ambapo alisomea sheria.

Mwaka 1983 – 1985 alijiunga na chuo ckikuu cha Karlmarx nchini Ujerumani na kupata shahada ya siasa na uchumi na mwaka 1985 – 1987 alipata shahada ya kwanza ya uzamili na mwaka 1987 – 1989 alipata shahada ya uzamili (Ph. D) katika fani ya siasa na uchumi katika chuo hicho hicho.

Dk. Gama alipata mafunzo mbalimbali kwa nyakati tofauti katika nchi za Marekani, Ireland, Uingereza, Israel,na nchi nyingine na kufanikiwa kutunukiwa vyeti mbalimbali na nishani za uongozi uliotukuka.

Dk. Gama amewahi kushika nyadhifa mbalimbali ndani ya chama cha mapinduzi (CCM) 1994 – 1996 alikuwa katibu mkuu wa CCM ambapo mwaka 1995 – 2000 alikuwa mjumbe wa NEC na mwaka 1996 – 2005 alikuwa Mbunge wa Songea Mjini.

Pia Dk. Gama amewahi kushika nyadhifa mbalimbali serikalini ambapo mwaka 1960 – 1962 alikuwa Mratibu msaidizi wa Polisi, mwaka 1963 – 1965 alikuwa msaidizi wa Mkurugenzi wa JKT akitokea Jeshi la Polisi mbali ya wadhifa huo pia aliwahi kuwa Mkuu wa vikosi vya JKT Mgulani, Ruvu pamoja na kufanya kazi Makao makuu ya JKT

Mwaka 1970 – 1973 alikuwa mkuu wa jeshi la kujenga Taifa hapa nchini ambapo mwaka 1973 – 1976 alikuwa mkurugenzi wa idara ya usalam wa Taifa na mwaka 1976 – 1977 alikuwa mkuu wa mkoa wa Dodoma na mbunge wa kuteuliwa.

Mwaka 1977 – 1989 alikuwa mkuu wa Mkoa wa Ruvuma na Mbunge wa kuteuliwa na mwaka 1989 – 1994 alikuwa mkuu wa Mkoa wa Tabora na Mbunge wa kuteuliwa na mwaka 1996 aliteuliwa kuwa mkuu wa Mkoa wa Morogoro.

Marehemu Dk. Gama aliacha Mjane, watoto 16, wajukuu 22 na vitukuu 2 na kwa mambo hayo aliyoyafanya na mengine mengi ataendelea kukumbukwa  kwa kila namna na kazi zake zitaendelea kuwa alama isiyofutika kwa watanzania wakiwemo wananchi wa mkoa wa Ruvuma.

Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi, pumzika Dk. Gama rekodi yako ya utumishi kwa Taifa itakukumbukwa na kuenziwa daima ,kwani Bwana alitoa na bwana ametwaa jina lake lihimidiwe na pengo lake halitazibika .

Mwandishi wa makala hii
Anapatikana kwa simu 0755 – 335051
Barua pepe: Stephano12mango@yahoo.com.




UTALII WA WANAFUNZI RUVUMA NI CHACHU YA WADAU KUTEMBELEA HIFADHI NCHINI
Na Stephano Mango,Songea

UTALII ni sekta inayokua na kutoa ajira takribani milioni 200 na inachangia dola za kimarekani trilioni 3.6 katika uchumi wa dunia.
Ambapo kati ya mwaka 2000 hadi 2006 idadi ya watalii wa kimataifa iliongezeka kutoka milioni 681 hadi 862.
Mapato yatokanayo na watalii wa kimataifa yaliongezeka kutoka dola za kimarekani 496 hadi dola bilioni 623 katika kipindi cha miaka hiyo.
Takwimu hizo ni za kimataifa hivyo kwa mujibu wa mchanganuo huo, Tanzania iko katika nafasi ya tano kwa mapato ya utalii katika nchi za Afrika kutokana na idadi ya watalii kuongezeka.
Sekta hiyo inachangia asilimia 17.2 ya pato la taifa (GDP) na inachangia karibu asilimia 25 ya jumla ya thamani ya mauzo yote ya nje.
Hata hivyo sekta hiyo ililiingizia taifa fedha za kigeni kwa wastani wa dola za marekani dola bilioni moja, mchango ambao ni mara tatu ya mchango wa sekta ya kilimo katika pato la taifa.
Kutokana na takwimu hizo sekta ya utalii imekuwa ya kwanza katika sekta zote zinazoliingizia taifa fedha za kigeni zinazotokana na mauzo ya bidhaa za nje.
Ingawa matarajio ya Serikali ni kuwa ikiwa wastani wa ongezeko la idadi ya watalii itakuwa kwa kati ya asilimia 10 na 20 basi Tanzania itapata watalii milioni moja ifikapo mwishoni mwa mwaka 2010.
Hata hivyo, kutokana na umuhimu wa sekta hiyo katika kukuza uchumi wa nchi kwa kuongeza wawekezaji, ajira na kupunguza umaskini kuna baadhi ya mikoa inaendelea kuhamasisha na kuvitangaza vivutio vya utalii katika maeneo husika kwa upana wake.
Miongoni mwa Mikoa yenye mikakati kabambe ya kuhakikisha vivutio vyake vyote vilivyopo katika Mkoa husika vinatangazwa ni Mkoa wa Ruvuma uliopo kusini mwa Tanzania.
Vivutio vilivyomo mkoani Ruvuma ni pamoja na poli la akiba la liparamba lenye kila aina ya wanyama na ndege, Ziwa Nyasa, Gereza la miti lililojengwa na wajerumani wakati wa vita dhidi ya Majimaji
Majengo ya Makumbusho ya mashujaa wa vita vya majimaji yenye zaidi ya miaka 100 ambayo ndani yake kuna sanamu za picha za mashujaa hao, zana zilizotumika kupigania vita hivyo, kaburi kubwa walilozikwa mashujaa 68.
Pango alilotumia kujificha nduna Songea Mbano, sehemu waliyonyongwa mashujaa wa vita hivyo, kaburi la mjerumani wa kwanza kunyongwa na wangoni Peramiho, jiwe la ajabu mbuji na vivutio vingine vingi,
Miongoni mwa hifadhi zenye upekee Nchini ni Ruhila Nature Reserve ambayo ina vivutio lukuki ambavyo vinaendelea kutangazwa kikamilifu ili vifahamike kwa watu wengi na kuongeza idadi ya utalii kusini mwa Tanzania na Taifa kiujumla.
Mkuu wa kikosi cha kuzuia ujangiri kanda ya kusini Metson Mwakanyamale anaelezea kwa ufasaha maana ya Ruhila Nature Reserve, mikakati iliyopo ya kuitangaza na changamoto zinazoikabili hifadhi hiyo.
Mwakanyamale alianza kwa kusema Ruhila ni jina la Mto ambao unapita katikati ya hifadhi hiyo, na ndio maana jina la mto huo limepewa heshima kubwa ya kubeba Nature Reserve iliyopo eneo hilo.
Mkuu huyo anafafanua kuwa Nature Reserve ni kipande cha ardhi chenye uoto wa asili ambacho kimetengwa kwa mujibu wa sheria stahiki lengo likiwa ni kuhifadhi uoto asilia ambao aupaswi kuharibiwa na shughuli za binadamu
Ruhila ni miongoni mwa hifadhi pekee nchini ambayo ni adimu kupatikana katika maeneo ya mjini lakini Mkoa wa Ruvuma umebahatika kuwa na eneo hilo zuri lenye vivutio vingi ambavyo watalii wa ndani na wa nje wanaweza kuja kuangalia pasipo kutumia fedha nyingi kwa ajili ya usafiri pindi wanapofanya utalii,kwani hifadhi hiyo ipo umbali wa kilometa 8 tu kaskazini Magharibi mwa mji wa Songea na ina ukubwa wa maili 311.
Akielezea historia ya hifadhi ya asili ya Ruhila Mkuu wa kikosi cha kuzuia ujangiri kanda ya kusini ambaye ndiye mkuu wa hifadhi hiyo Metson Mwakanyamale.
Alisema hifadhi hiyo ilianzishwa mwaka 1973 na mwaka 1974 ilizungushiwa uzio wa kilometa 8 ili kuzuia wanyama wasiende kwenye makazi ya watu wanaoishi kuzunguka eneo hilo na kuongeza kuwa hifadhi hiyo imezungukwa na vijiji 3 vilivyopo katika Manispaa ya Songea ambavyo ni Mkuzo, Mshangano na Chandarua.
Akizungumzia wanyama walioletwa wakati hifadhi hiyo inaanzishwa mwaka 1974 kutoka Arusha ni pamoja na Pofu 9, Ngorombwe 3, Nyumbu 9, Kuro 1 ambao hivi sasa hawapo na Pundamilia 10 ambao wamebaki 6.
Shughuli ya kuwaleta wanyama hao kutoka Arusha ilifanywa na mhifadhi Hashim Sariko mwaka 1975 ambaye kwa sasa ni Meneja mkuu wa pori la akiba la wanyama Liparamba wilayani Mbinga.
Mwakanyamale anasema kumbukumbu za mwaka 1981zinaonyesha kuwa wanyama walioletwa katika hifadhi ya Ruhila waliongezeka, ambapo Pofu waliongezeka kutoka 9 hadi 15.
Pundamilia waliongezeka kutoka 10 hadi 26, Nyumbu waliongezeka kutoka 9 hadi 13, Ngorombwe waliongezeka kutoka 3 hadi 5 na chatu ambao idadi yao haikuweza kupatikana ambao wameendelea kuongezeka kila mwaka,aliongeza kuwa watu wengi wa ndani na nje walipata fursa ya kujionea vivutio mbalimbali vilivyomo ndani ya hifadhi hiyo wakati huo.
Hata hivyo katika miaka ya 1986 na 1989 kasi ya matumizi ya hifadhi hiyo ilipungua sana ikilinganishwa na miaka ya nyuma, hii ilitokana na usimamizi usiozingatia utaalamu na kufanya baadhi ya vivutio kutoweka na kuharibika kwa miundombinu muhimu katika hifadhi hiyo.
Mwakanyamale alisema ili kuimarisha utalii wa ndani na wa nje katika hifadhi hiyo kulingana na Sera ya Taifa ya wizara ya Maliasili na utalii alianza kutengeneza uzio( fensi ya Senyenge) na mageti ili kuzuia wanyama wasitoke kutoka kwenye hifadhi kwenda kwenye makazi ya watu ili ulinzi wa vivutio vilivyomo visiharibiwe.
Ameeleza kuwa tayari ametengeneza (keji) bebeo la chui au simba mtoto ili atakapopatikana wasipate shida ya kumbeba ,mkuu huyo alisema pia licha ya wanyama ambao wanategemewa kuongeza uzuri wa hifadhi, kuna vivutio vingine ndani ya hifadhi hiyo.
Miongoni mwa vivutio hivyo ni miamba ambayo chatu huishi, maporomoko ambayo kobe huishi, chanzo cha mto Ruhila ambacho kimebeba jina la hifadhi na vivutio vingine vingi.
Hifadhi ina maeneo ya ufugaji nyuki pia ina vivutio vya wanyama wa aina ya Pundamilia, pongo, sungura, kobe, kakakuona,nyani na ngedere wa kila aina.
Vivutio vingine ni mandhari ya hifadhi hiyo ambayo ni ya kuvutia sana, mabwawa ya samaki, “ndege aina ya kanga, kware, bata, mwali na nyange, alisema Mwakanyamale”.
Ili kuimarisha utalii wa ndani Mwakanyamale anasema alifanya mawasiliano na Afisa Elimu wa Mkoa wa Ruvuma na wakuu wa shule za Mkoa wa Ruvuma ili waende katika hifadhi hiyo kwa ajili ya utalii wa mafunzo.
Tayari ofa hiyo iliyotolewa kwa Shule za msingi, Sekondari na Vyuo iliyoanza Disemba 2008 na kumalizika mwanzoni mwa mwaka 2010 imefanikiwa kwa asilimia 85 ambapo shule zaidi 86 zilifanikiwa kutembelea hifadhi hiyo ambapo shule 10 za kwanza kutembelea hifadhi hiyo zilipata mipira miwili kila moja.
Kwa mujibu wa mkuu huyo orodha ya ada ya kiingilio katika hifadhi hiyo kuanzia julai mosi 2009 ni kama ifuatavyo,ambapo ada ya mtu mwenye umri wa miaka 18 raia wa Tanzania kwa siku ni sh. 5,000 na raia wa kigeni atalipa dola za kimarekani 50.
Watoto wa miaka 5 hadi 17 raia wa Tanzania watalipa Shilingi 3000 ambapo raia wa kigeni watalipa dola za kimarekani 30 na watoto walio chini ya miaka mitano raia wa Tanzania na nje wataingia bure katika hifadhi hiyo.
Mwakanyamale anafafanua zaidi kuwa huduma ya kuongoza wageni kiofisi kwa gari raia wa Tanzania ni sh 30,000 na kuongoza kwa miguu kwa siku itakuwa ni sh 25,000 ,pia alisema kuongoza raia wa kigeni kwa gari kiofisi watalipa dola za kimarekani 30 na kuwaongoza kwa miguu kwa siku watalipa dola za kimarekani 25.
Alisema ada za kuchukua picha za kawaida na za video kwa siku kulingana na mpangilio maalum kutoka kwa mkuu wa hifadhi ya Ruhila siku moja hadi siku 89 ni kati ya dola za kimarekani 50 hadi 200.
Siku 90 hadi 179 ni kati ya dola za kimarekani 40 hadi 150 na siku 180 hadi 720 ni kati ya dola za kimarekani 30 hadi 100 ambapo ada ya kusajiliwa kwa muongozaji ni sh 50,000 kwa raia wa Tanzania na raia wa kigeni dola za kimarekani 2000.
Jitihada hizo tayari zimezaa matunda ambapo watalii 946 wametembelea hifadhi ya Ruhila kuanzia julai 2008 hadi septemba 2009. Pia alisema kuna shule 50 za msingi, sekondari 36, viongozi mbalimbali wa mkoa zaidi ya 80 na walimu walitembelea hifadhi hiyo.
Pamoja na uzuri wa hifadhi hiyo Bw Mwakanyamale alisema kumekuwa na ujangiri unaotokana na watu kukata miti kwa ajili ya kuezekea nyumba zao, kuni, kuchimba mizizi kwa ajili ya dawa za kienyeji, kukata nyasi na kuchoma moto ovyo.
Alizitaja changamoto zingine zinazoikabili hifadhi hiyo ni pamoja na uhaba na uchakavu wa nyumba za watumishi wa hifadhi hiyo, kwani kumbukumbu zinaonyesha tangu mwaka 1974 zilipojengwa hazijawahi kufanyiwa ukarabati. Pia nyumba zaidi ya 6 zinatakiwa kujengwa ili kukidhi mahitaji ya idara ya wanyama pori kanda ya kusini.
Changamoto nyingine ni barabara ya kwenda katika hifadhi hiyo yenye urefu wa kilometa 3.5 inahitaji kutengenezwa kwa kupandisha tuta na kuweka changarawe ili iweze kupitika wakati wote kwa uwakika.
Kwa upande wake mwanafunzik wa Shule ya sekondari ya Chandamali kidato cha pili Anuciata Mapunda mara baada ya kutembelea hifadhi hiyo na kujionea mandhari ya Ruhila Nature Reserve.
Alisema Ruhila ni eneo zuri ambalo linavutia sana na linaweza kuliingizia Taifa mapato makubwa endapo likiendelezwa kwa sababu eneo hili ni pekee nchini ambalo liko kilometa sifuri kutoka makazi ya watu hivyo watalii hawawezi kutumia gharama kubwa kufika eneo hilo.
Aliongeza kuwa ziara za masomo kwa wanafunzi huongeza chachu ya uelewa kwani kwa mwanafunzi ambaye mara nyingi amekuwa akisoma umuhimu wa utalii kupitia vitabu anakuwa na uelewa mdogo kwani hajawahi kufanya aina yoyote ya utalii hususani kwenye maziwa,mbuga za wanyama na hifadhi mbalimbali,lakini pindi atakapotembelea anakuwa na uelewa mkubwa na pale anapokuja kusoma kwenye vitabu au kusimuliwa/kuelezewa anakuwa na ufahamu mkubwa na hivyo kufanya uwezo wake kuwa mkubwa katika jambo hilo
Hata hivyo, Bw Mwakanyamale alisema ana mikakati mingi ya kuboresha hifadhi hiyo na ameiomba Serikali kumwezesha kikamilifu raslimali fedha ili aweze kukamilisha ujenzi wa miundombinu katika hifadhi hiyo na kuwataka wananchi kutembelea hifadhi zao ili waweze kujifunza tabia za viumbe, aina za viumbe hao na kujionea maliasili zilizopo katika maeneo yao na nchini kwa ujumla ili waweze kuvitunza na kuvitangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini kwa faida ya vizazi vilivyopo na vijavyo

Mwandishi wa Makala hii
Anapatikana kwa simu 0755-335051
Baruapepe;stephano12mango@yahoo.com

MHANDISI MANYANYA ALIYE DHAMIRIA KUBADILI MAISHA YA WANAWAKE RUVUMA


MHANDISI MANYANYA ALIYE DHAMIRIA KUBADILI MAISHA YA WANAWAKE RUVUMA
 
 Na,Stephano Mango,Songea.
 
HUWEZI kuzungumzia Wanawake jasiri hapa nchini bila kumtaja Mhandisi Stella Martin Manyanya ambaye ni Mbunge mbunge mtarajiwa wa Viti maalum Mkoa wa Ruvuma kupitia Chama cha Mapinduzi.
 
Ukibahatika kukutana na kuzungumza naye utabaini kuwa hana majivuno, anajiheshimu na anaheshimu wenzake pia bila kujali wadhifa wa mtu husika.  Mhandisi Manyanya anapendwa na wengi kutokana na tabia yake ya kuwa karibu na Wananchi katika hamasa mbalimbali za Kimaendeleo na harakati za utalii, ujasiliamali, elimu na michezo.
 
 Ujasiri wa Mhandisi Manyanya ulionekana pale alipoamua kujiuzulu kazi yake ndani ya shirika la Umeme Tanzania(Tanesco) Mwaka 2007/2008 wakati alipokuwa kwenye Kamati ya Bunge ya Uchunguzi wa Mkataba tata wa kampuni ya kufua umeme ya Rich Mond ili kuepusha mgongano wa kimaslahi baina ya kazi yake ndani ya Shirika hilo na ile ya bunge ambayo ilikuwa ikichunguza utata wa Rich mond.
 
Manyanya alikuwa Mwanamke pekee aliyekuwa kwenye kamati ya Bunge iliyochunguza Kampuni hiyo iliyoleta kitimtim Nchini hadi Baraza la Mawaziri likavunjika baada ya aliyekuwa Waziri Mkuu Edward Lowasa kujiuzulu.  Mbali ya mhandisi Manyanya ambaye alikuwa Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, wajumbe wengine walikuwa ni Dk. Harrison Mwakyembe (Mwenyekiti) Lukas Selelii, Mohamed Mnyaa na Herbert Mtangi.
 
Hii ikiwa ni mara yake ya kwanza kuingia bungeni lakini anaufahamu mkubwa ukilinganisha na baadhi ya Wabunge hasa wale wa rika lake na kwa wale wanaomfahamu wanasema mafanikio yake yametokana na kujiamini na kupenda kusimamia kile anachokiamini.
 
Nilibahatika kukutana na kufanya mahojiano naye hivi karibuni katika ofisi yake ya Better Life Tanzania iliyopo Mahenge, Songea Mjini Mkoani Ruvuma baada ya kuchukua muda mrefu toka tulipo panga ahadi ya kukutana kwa mahojiano, hii ilikuwa ni kutokana na muda mwingi kuwa katika huduma mbalimbali za kijamii kwenye Kata, Wilaya na Mkoa katika kushughulikia utekelezaji wake wa ilani kwa Wananchi na Chama chake.
 
Katika mahojiano yake na Gazeti hili alizungumzia historia yake, ambapo alisema alizaliwa agosti 4 mwaka 1962, Mwambao mwa Ziwa Nyasa katika Kijiji cha Kihagara, Wilaya mpya ya Nyasa, Mkoani Ruvuma.  Anasema yeye ni mtoto wa tano kati ya watoto Kumi na moja (11) waliozaliwa katika familia ya Mzee Martin Manyanya, amasema ameolewa na amebahatika kupata watoto watatu ambapo anaeleza kuwa Familia yake ndio faraja kubwa inayomwezesha kufanya kila kitu.
 
Mhandisi Manyanya hadi sasa ni mlezi wa Chama Cha Waandishi wa habari Mkoa wa Ruvuma (RPC), Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC), Mjumbe wa Kamati ya utekelezaji wa Jumuiya ya Wazazi Tanzania, Mjumbe wa bodi ya Makumbusho Mkoa wa Ruvuma na Mwenyekiti wa Kamati ya Ushauri ya Makumbusho ya Taifa na hivi karibuni alitetea nafasi yake ya ubunge wa Viti maalum mkoa wa Ruvuma ambapo alipigiwa kura 300 kati ya wajumbe 380 na kupelekea kuwa mshindi wa kwanza
 
Kitaalama Manyanya ni fundi mchundo (Technicianian) ambaye alikuwahi akifanya kazi katika Shirika la Madini la Taifa (Stamico) kuanzia Mwaka 1983 hadi 1986, ambapo baada ya hapo alijiunga na Chuo cha Ufundi cha Dar es salaam (DIT) na baada ya kupata Diploma aliajiriwa na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuanzia Mwaka 1992 hadi 1995 na alipata nafasi ya kujiunga na masomo zaidi Nchini Norway.
 
Manyanya anasema baada ya kurejea kutoka Norway aliendelea na kazi katika Shirika la Umeme Nchini ambako alifanya kazi hadi Novemba 2007 ndipo alipojiuzulu kufanya kazi ndani ya Shirika hilo mwaka huo,akiwa Mbunge wa Viti Maalum mkoa wa Ruvuma baada ya kuchaguliwa kuwa mmoja wa wajumbe wa kamati ya Bunge iliyochunguza Kampuni ya Richmond ili kuepuka mgongano wa kimaslahi baina ya Bunge na Tanesco.
 
Akizungumzia shughuli zake za uwakilishi kwa miaka mitano akiwa Mbunge wa viti maalum Mkoa wa Ruvuma Mhandisi Manyanya anasema kuwa alijikita zaidi katika elimu, afya,uchumi na uimarishaji wa Chama Cha Mapinduzi kupitia Jumuiya ya Wazazi na Wanawake (UWT) na kuendeleza sekta mbalimbali za Kijamii.
 
Anasema kwa upande wa elimu, amesimamia zaidi elimu kwa Wasichana ambao kwa asilimia kubwa wamekuwa nyuma kimaendeleo kutokana na wazazi wengi kutowathamini watoto wa kike ambao wengi wao wameishia kupata ujauzito mashuleni na wengine kuozeshwa.
 
Kutokana na hali hiyo amehamasisha na kuchangia mabati, saruji na fedha shilingi milioni 59 za ujenzi wa mabweni katika Shule nyingi za Sekondari zilizopo Mkoani Ruvuma ambapo baadhi ya shule hizo zimeanza ujenzi ilikupunguza tatizo la mimba kwa Wasichana na kujiingiza katika ndoa za utotoni.
 
Anasema sambamba na kuchangia ujenzi huo amekwisha toa elimu kwa wazazi na wananchi kupitia mikutano ya hadhara juu ya umuhimu wa elimu kwa Wasichana katika Wilaya ya Tunduru, Namtumbo, Songea vijijini na Mbinga na wilaya mpya ya Ziwa Nyasa. 
 
Anasema pia ametoa vifaa vya michezo kwa Shule za Msingi, Sekondari na vijiwe vya vijana katika Wilaya zote za Mkoa wa Ruvuma vyenye thamani ya Milioni 23 ili kuweza kupunguza muda wa vijana kuzurura na kushawishika kufanya vitu viovu, kama vile uasherati, matumizi ya pombe haramu na uvutaji wa madawa ya kulevya. 
 
Anasema dhamira yake tangu alipokuwa anaingia bungeni mwaka 2005 ilikuwa ni kuona viongozi na watendaji wa CCM wanafanya kazi katika Mazingira mazuri ambapo anasema amekarabati na kuweka samani za kisasa katika Ofisi za Jumuiya  zote za Chama katika Wilaya ya Songea,Mbinga,Songea vijijini ambapo pia ametoa sh. Million 1 kwa ajiri ya jumuiya ya UWT Wilaya ya Namtumbo ili waweze kununua kiwanja kwa ajiri ya ujenzi wa jengo la kitega uchumi cha Jumuiya hiyo.
 
Kuruthum Mhagama Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Ruvuma anasema Mhandisi Manyanya ameonyesha uongozi stahiki licha ya kuwanyanyua Wanawake wengi Kiuchumi kupitia Asasi isiyo ya kiserikali ya Better Life Tanzania kwani  ameweza kuvisaidia vikundi mbalimbali vya kijamii raslimali fedha na elimu ya Ujasiriamali.
 
Viongozi wengi wanatabia ya kusahau walikotoka ambapo wakikumbushwa wanaleta jeuli lakini Manyanya amekumbuka alikotoka na amedhamiria kwa dhati kubadili maisha ya Wanawake wa Mkoa wa Ruvuma na ndio maana katika uchaguzi wa Jumuiya ya UWT uliofanyika hivi karibuni Manyanya aliibuka na ushindi wa kishindo kwa kupigiwa kura na wajumbe 300 kati ya wajumbe 380 anasema Mhagama.
 
Manyanya ameshirikiana na wanawake wa Mkoa wa Ruvuma kufungua Asasi ya kiraia ya Better Life Tanzania inayowafundisha wajasiriamali wadogo na wakati mbinu mbalimbali za kuweza kujikwamua kiuchumi,ufugaji wa kuku wa kienyeji na wa kisasa, utengenezaji wa batiki, kilimo cha uyoga na kubadilishana mawazo kwa nia ya kujengana.
 
Manyanya ambaye pia ni Mkurugenzi wa Asasi hiyo anasema azma ya asasi hiyo nikuelimisha wananchi ili waweze kuchukua matatizo waliyokuwa nayo kama changamoto na kutafuta njia za kukabiliana nazo ambazo zitaweza kupunguza au kumaliza matatizo hayo na wakati huohuo kutengeneza ajira. Anasema kuwa asasi hiyo imekuwa ikiangalia fursa za Kiuchumi na namna ya kutumia fursa hizo katika kujikwamua na umasikini ambapo toka 2006 hadi sasa Wananchi zaidi ya 3000 wamefaidika na asasi hiyo kupitia sekta za Elimu na Kiuchumi.
 
Anasema wajasiriamali wengi hawafahamu namna ya kuandika miradi (Proposal) hasa pale Benki zinapowataka kufanya hivyo ili waweze kupata mikopo stahiki ambapo kwa utaratibu uliowekwa na kituo cha Better Life Tanzania kilichopo Mahenge Mjini Songea chini ya Mratibu wa Kituo hicho Genfrida Haule Wanawake 60 na vijana 43 wamefaidika na elimu ya uandikaji wa Miradi ya ujasiriamali.
 
Ili kuhakikisha kazi ya ujasiriamali anaifanya vyema Manyanya anasema aliamua kujiunga na kituo cha Ujasiriamali cha Chuo Kikuu cha Dar es salaam (UDEC) ambako alichukua digrii ya pili  (masters degree) ya masuala ya ujasiriamali. Anasema elimu hiyo aliyoipata anaitumia vyema kuwaelimisha Wananchi hasa Wanawake wa Vijijini wasiojua kuandika miradi ili na wao waweze kunyanyuka na kuweza kupata mikopo  katika Benki ambapo anasema elimu hiyo ameanza kuitoa katika Wilaya zote za Mkoa wa Ruvuma .
 
Akizungumzia kilimo cha zao la uyoga anasema kilimo hicho cha kisasa cha zao hilo na urahisi wa Kilimo hicho umewavutia watu wengi kukilima ambapo anasema toka 2006 hadi sasa kituo cha Better Life Tanzania kinahudumia wakulima 8000 katika Mkoa wa Ruvuma na wakulima 260 kutoka Mikoa ya Rukwa, Pwani, Iringa na Lindi.
 
Anasema kilo moja ya uyoga wenye ubora stahiki inauzwa kati ya shilingi. 6000 hadi 8000 kulingana na soko husika pamoja na ubora wa zao ambapo anasema zao hilo limeboresha familia nyingi na hasa wanawake wa Mkoa wa Ruvuma .
 
Anasema anaishukuru Kampuni ya Bia Tanzania TBL na mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kwa msaada wa fedha walizozitoa kwa ajili ya ujenzi wa Maabara ya kisasa ya kuzalisha mbeguza uyoga katika Kata ya Mshangano (Mkuzo)Mjini hapa kwani maabara hiyo ikikamilika itaweza kuleta mapinduzi makubwa ya kilimo cha zao hilo .
 
Mhandisi Manyanya alitumia mahojiano haya kuomba ridhaa ya wananchi ili aweze kuwawakilisha kwenye Ubunge wa viti maalum Mkoa wa Ruvuma kupitia Chama Cha Mapinduzi kwa awamu ya pili pia amechukua nafasi hiyo kuwaomba radhi wananchi wa Mbinga ambao walimtaka agombee jimbo moja kati ya majimbo mawili yaliyopo Wilaya ya Mbinga katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Octoba 31 mwaka huu.
 
“Nawaomba radhi wananchi wa Mbinga waliokuwa na kiu ya kunitaka niachane na viti maalum nikagomee jimbo nimelitazama na kulifikiria ombi lao kwa umakini mzito na ninaheshimu nia yao lakini naomba kuwaambia kuwa sijawatosa kwani mwaka 2015 nitafanya hivyo ila kwa sasa nitaongeza juhudi katika kutetea vilio vyao kwa Wabunge watakao chaguliwa nikiwa Mbunge wa Viti maalum”, alisema Manyanya.
 
Anasema kikubwa kinachomfanya asigomee jimbo kwenye uchaguzi wa Mwaka huu ni maombi yenye uzito mkubwa ya Wanawake ambao ameshaanza nao kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo, hivyo anataka aendelee kuwa nao kwa maendeleo zaidi kupitia umoja wa wanawake wa Tanzania (UWT)
 
Alisema awamu ya kwanza ilikuwa ni ya kujifunza na hivyo amejifunza mengi ambayo anatakiwa kuyatekeleza akiwa kamili kulingana na ndoto zake za kuongeza chachu na kasi ya maendeleo akiwa Mbunge wa viti maalum kwani huko ndiko ana fursa kubwa ya kutetea Mkoa mzima kuliko angekuwa Mbunge wa jimbo.
 
Naomba waniombee kupata kura ili nirudi Bungeni kwani nimejifunza na nipo tayari kuwatumikia na kwa sasa nitaendelea kuwatumikia katika viti maalum na nitatekeleza wajibu na kutimiza maombi yao nikiwa katika nafasi hiyo, alisema Manyanya.
 
Mwandishi wa Makala
Anapatikana  simu 0755-335051

Sunday, January 2, 2011

MASHUJAA WA VITA VYA MAJIMAJI WAKINYONGWA

Viongozi wa Kabila la Wangoni na Askari Waliokuwa Mstari wa mbele katika mapigano ya vita vya Majimaji Wakinyongwa Tarehe 27/02/1906 na Jumla  yao walionyongwa walikuwa 67  ambapo 66 walizikwa kwenye Kaburi moja ambalo walilichimba wenyewe bila kujua kuwa watakuja kuzikwa wenyewe na Mwingine ambaye ni Nduna Songea Mbano alizikwa kwenye Kaburi la Peke yake.

UJENZI WA MNARA WA MASHUJAA WALIONYONGWA NA WAJERUMANI NI KIELELEZO MUHIMU CHA KUWAENZI



Na, Stephano Mango, Songea

ENEO waliponyongwa viongozi na askari 67 walioshiriki kupigana vita vya Majimaji februari 27,1906 linatarajiwa kujengwa mnara wa kumbukumbu ili kuweka alama ya kudumu na wananchi waweze kupatambua na kupaenzi kikamilifu.

Philip Maligissu ambaye ni Mhifadhi kiongozi wa Makumbusho ya Taifa ya Majimaji Songea,akizungumza na Waandishi wa Habari ofisini kwake hivi karibuni anasema, eneo hilo ni muhimu sana kwa historia ya nchi yetu ambalo lipo nyuma ya ukumbi wa Songea Club  hivyo ni lazima uwekwe alama ya kudumu itakayotambulika kiurahisi na kuvuta hisia za mawazo ya watanzania wengi kwenda kupatembelea.

Alisema kuwa mnara huo unatarajiwa kuwa kumbukumbu muhimu na adhimu ya mashujaa wa vita vya majimaji,askari wanaopigana vita vya kagera na kufa kwa ajali njiani kwenye mlima wa Lukumburu wakiwa wanarudi nyumbani baada ya ushindi na  mashijaa waliopigana vita ya pili ya dunia.

Alieleza kuwa eneo hilo ni kumbukumbu muhimu katika historia,utamaduni na utalii ambapo ujenzi wa mnara utakapokamilika utawekwa majina ya mashujaa hao kwenye vibao vya shaba ili watu waweze kusoma na kuwaelewa wapiganaji hao.

Maligissu alibainisha kuwa kutawekwa fensi nzuri fupi na imara itakayowawezesha watu kuingia kwa utaratibu maalumu na kufanya shughuli za utalii na kupata elimu stahiki ya kihistoria na kuhusu uhuru wa mtanzania na mwafrika kwa kutumia vielelezo halisi.

Binafsi nakubariana na wazo la kujenga mnara katika eneo hilo,kwani historia ya mapambano ya kupinga utawala wa wakoloni na uhuru wa nchi yetu haiwezi kukamilika bila kuwataja mashujaa wa vita ya majimaji waliopoteza uhai wao kwa kuitetea nchi na hadhi yao kuanzia Julai 1905 hadi Agosti 1907.

Jina hilo la vita vya majimaji lilitokana na imani ya matumizi ya dawa iliyochanganywa na maji,punje za mahindi na mtama zilizosadikika kuwa zingempa mpiganaji kinga ya kutodhurika kwa shambulio la risasi za Wajerumani chini ya uhamasishaji wa mganga kinjekitile ngwale.

Vita hivyo vilidumu kwa miaka miwili kuanzia 1905 hadi 1907 na waanzilishi wa mwanzo wa vita hivyo walikuwa machifu na Mganga wa jadi katika jamii ya  wangindo na wamatumbi.

Baadaye vuguvugu hilo lilienea kwenye jamii nyingi ikijumuisha jamii za wamatumbi,wangindo,wamwera,wapogoro,wandendeule,wabena,wasangu,wangoni na nyingine,

Inaeleweka wazi kuwa toka mwanzo wakoloni kutoka ujerumani walijawa na shauku ya kunyonya raslimali kutoka makoloni yao ndio maana walilazimisha jamii za watu walioishi katika kuenea waliyoyachukua kuja tawala kwa nguvu,kushiriki katika uanzishaji wa mashamaba  ya mazao waliyoyahitaji katika viwanda vyao huko ulaya.

Vita vilipoanza katika vilima vya matumbi,kaskazini magharibi mwa kilwa julai  1905 na sababu kubwa ilikuwa ni wananchi kupinga vitendo viovu hasa vya kulazimisha kulima mazao ya biashara,kulipa kodi na unyanyasaji mwingine waliofanyiwa na mfumo wa utawala wa wajerumani.

Kwa muda wa miaka miwili wajerumani walishuhudia waafrika wakiwadhihirishia kwamba  dhana waliyokuwa nayo ya kuona Afrika ni bara la giza haikuwa sahihi hata kidogo.

Walilazimishwa kujua kwamba Afrika ina watu wenye dhamira,utashi na uwezo wa kutetea utu, uhuru na heshima yao,jambo lililowalazimisha wajerumani kuongeza wapiganaji kabla ya ushindi ili kukabiliana na mashambulizi ya mashujaa wa Afrika wa kusini  mashariki mwa Tanzania bara.

Wajerumani kwa juhudi kubwa na kwa kutumia bunduki na mbinu nyingine nyingi ikiwemo kuchoma moto mashamba na  maghala ya kuhifadhia chakula ya waafrika ili kudhoofisha uwezo wa kushambuliwa

Baada ya vita kusambaa askari na viongozi 67 walioshiriki vita walikamatwa na kufungwa jela na kuhukumiwa kunyongwa hadi kufa Februari 27 mwaka 1906.

Tarehe hiyo ilikuwa ni siku ya masikitiko makubwa kwa watu wa Ruvuma na Taifa kiujumla kwani watu 67 walinyongwa na kuzikwa katika kabuli moja lililochimbwa na wao wenyewe walipokuwa wafungwa bila kujua kuwa ndilo litatumika kuwazika wenyewe isipokuwa kiongozi wao Nduna Songea Mbano ndiye aliyezikwa kwenye kaburi la peke yake.

Mashujaa 66 walinyongwa na kuzikwa kwenye kaburi moja akiwemo chifu Mputa Gama na wasaidizi wake (nduna) kumi na mbili (12)  akiwemo nduna Songea mbano  ambaye alikuwa maarufu kuliko chifu mputa Gama alinyongwa na kuzikwa katika kaburi lake.

Akizungumzia tukio la kunyongwa mashujaa wa vita hivyo Makamu Mwenyekiti wa Baraza la mila na Desturi la Makumbusho ya Taifa ya Majimaji Songea,Ally Songea Mbano ambaye pia ni Mjukuu wa Nduna Songea Mbano aliyepewa heshima ya jina lake litumike katika kuuita mji wa Songea

Anasema kwa masikitiko kuwa unyongaji ulifanyika kwa awamu tatu yaani Februari 27, machi 20 na Aprili 12,1906 katika eneo la Songea Club lililopo kata ya Mjini Manispaa ya Songea na kwamba siku ya kunyongwa watu wengi walikusanywa na walisimamishwa mahali ambapo waliweza kuwaona wanyongaji na waliokuwa wakinyongwa

Anasema  kuwa ilifanya vile ili kujenga hofu miongoni mwa jamii za waafrika ili kuwa vunja moyo wa ushupavu na ujeuli hasa pale watakapokuwa wanapewa amri mbalimbali za wakoloni wa kijerumani.

Katika eneo ambalo mnara unatarajiwa kujengwa kuna nguzo kubwa mbili zilizosimikwa pande mbili ambazo kwa mujibu wa Mbano,nguzo hizo zilishikilia mnyororo uliofungwa vitanzi vinne na kwamba chini ya nguzo hizo kulikuwa na ubao uliowekwa juu ya nguzo fupi nne.

“Basi waliwafunga wafungwa wa nne toka kwenye mnyororo ule mkubwa na wakasimamishwa juu ya ule ubao uliotegeshwa wakawapachika zile kamba zilizoning’inia kila mmoja na kamba yake huku wakiwa wamefungwa kamba mikono yote miwili ili wasiweze kujimudu kujitikisa na nyuso zao zilikuwa zimefungwa vitambaa nyekundu ili wasiweze kuona” anasema Mbano.

Anasema kuwa walisitiliwa maumbile yao kwa vitambaa vidogo kwenye sehemu zao za siri kabla ya askari kufyatua ubao na ndipo miili ya Mashujaa hao ikabaki ikining’inia kwenye vitanzi mpaka  walipokata roho

Baada ya Mashujaa kukata roho katika mateso makali, wauaji hao waliondoa miili hiyo na kuweka kando kwani walikuwa wakiwanyonga  wanne kwa wakati mmoja ambapo kwa siku ya kwanza Februari 27 walinyongwa watu 40 na  machi 20 walinyongwa watu 26 na Aprili 12 . 1906 alinyongwa Jemedari Nduna Songea Mbano.

Anabainisha kuwa maiti za Mashujaa walionyongwa kwa siku moja zililazwa katika kaburi hilo kubwa kiubavu bila sanda na kufukiwa kidogo ili kutoa nafasi kwa maiti wengine wa siku nyingine kuzikwa na kwamba walioongezeka kunyongwa walilazwa juu ya wale wa kwanza na kufukiwa katika kaburi hilo moja kubwa na kuongeza kuwa kati ya Mashujaa hao kulikuwa na wa imani tofauti  kwani walikuwepo wapagani,wakristo na waislamu.

Anasema kuwa Aprili 12 .1906 Nduna Songea  Mbano alidai na yeye anyongwe kama ndugu zake na wajerumani walimnyonga na kumzika kwenye kaburi la pekee yake ambalo lipo kwenye eneo la Makumbusho ya Taifa ya  majimaji Songea katika eneo la  Mahenge,Manispaa ya Songea.

Anasema hiyo ilitokea kwa sababu Nduna Songea Mbano alikuwa ndiye jemedali mkuu wa jeshi la wangoni na alikuwa hodari asiyeogopa  lolote kwa hiyo wajerumani walitaka abakie ili wamtumie kwa malengo yao jambo ambalo hawakufanikiwa.

Mzee Mbano anasema kuwa Mashujaa walionyongwa  vitanzini walikuwa 67, waliokufa gerezani kabla ya kunyongwa walikuwa wawili na waliopigwa risasi ili kuonyesha nguvu ya risasi walikuwa watano na kufanya jumla ya mashujaa 74 waliouwawa kikatili.

Ingawa inakadiliwa kuwa watu 75,000 walipoteza maisha yao ukanda wa kusini mwa Tanznaia baada ya vita ambapo katika eneo la Ruvuma inakadiriwa kuwa zaidi ya watu 1000 walipoteza maisha yao.

Ni wazi kuwa vita vya Majimaji vilikuwa na madhara makubwa ya kiuchumi na kijamii kwa watu wa mikoa ya kusini mashariki mwa Tanzania bara kwani kulitokea vifo vilivyosababishwa na  mapigano,upungufu wa chakula, watu kushindwa kufanya kazi kutokana na kukimbia makazi yao, ulimwaji wa mashamba na maghala ya kuhifadhia chakula uliofanywa na wajerumani ili kudhoofisha uwezo wa kushambuliwa wajerumani nao walipata madhala  kwani wapiganaji wao waliuawa na wapiganaji wazalendo na walilazimika kuongeza wapiganaji kukabiliana na mashambulizi kabla ya ushindi.

Vita vya Majimaji ni kumbukumbu muhimu katika historia ya Tanzania na kwamba Mashujaa wa vita hivyo wanastahili kuheshimika kwa kuwa walitetea utu, heshima na haki za binadamu na kielelezo halisi cha watanzania kukataa kutawaliwa na wakoloni kwani machifu na wapiganaji wengine wa vita hivyo Nduna songea mbano na wenzake wanastahili kukumbukwa.

Pamoja na jamii nyingine zilizopambana na wakoloni wakiongozwa na  machifu kama vile Mkwawa wa wahehe, Mangi sina wa Moshi, Abushiri na Bwana heri wa Pangani na viongozi waliongoza harakati za kudai uhuru kutoka kwa  waingereza

Mashujaa wa harakati za kudai uhuru  ni wale wote walioshiriki bila kuyumbishwa na hila za wakoloni kuhamamisha wananchi kuondoa utawala wa kigeni mpaka Taifa letu lilipopata uhuru mwaka 1961 Tanzania bara,na mapinduzi ya Zanzibar yaliyoondoa utawala wa kisultani Tanzanaia visiwani  mwaka 1964.

Orodha ya Mashujaa wa vita vya Majimaji ni kubwa ambapo baadhi ya majina yao yamehifadhiwa katika orodha ya walionyongwa baada ya kukamatwa na kufungwa na wajerumani.

Miaka zaidi ya mia moja  baada ya vita vya Majimaji watanzania wamejifunza mengi na kujenga upendo miongoni mwao na mahusiano mazuri na mataifa mengine ingawa ni wazi kuwa machungu ya vita hivyo bado hayajasahaulika

Lakini utamaduni mpya umejengeka miongoni mwa watanzania wa kushirikiana na kuheshimiana bila kujali kabila,rangi na asili ya mtu anakotoka huu ni ukomavu mkubwa uliojengwa na Mashujaa wetu hivyo ujenzi wa mnara wa Mashujaa hao ni muhimu kwa kizazi kilichopo na kijacho kwani ni kielelezo muhimu cha kuwaenzi, kuwaheshimu na kuwathamini wazee hao

Mwandishi wa Makala haya
Anapatikana simu 0755-335051
Barua pepe;stephano12mango@yahoo.com.

KABURI LA NDUNA SONGEA MBANO

Mhifadhi Kiongozi wa Makumbusho ya Taifa ya Majimaji Songea Phillip Maligissu Akionyesha Kaburi alilozikwa Nduna Songea MbanoAmbalo Lipo kwenye Makumbusho ya Taifa ya Majimaji Songea

NDUNA SONGEA MBANO KIONGOZI SHUJAA WA WANGONI ANAYESTAHILI KUENZIWA DAIMA.




Na Stephano Mango, Songea.

HUWEZI kuilezea na kuikamilisha historia ya vita ya Majimaji na ukombozi wa nchi yetu bila kumtaja shujaa wa kabila la wangoni Nduna Songea Mbano ambaye jina lake lilipewa hadhi ya kuuita mji wa Songea kutoka kwenye jina la Ndonde mwaka 1906.

Kiongozi huyo alikuwa ni miongoni mwa wasaidizi ( Nduna) 12 wa Chifu wa kabila la wangoni (Nkosi) chifu Mputa bin Gwezerapasi Gama.

Ambapo wasaidizi wake wengine walikuwa ni Mgendera Mawaso Gama, Kohongo Magagura, Mputa Mkuzo Gama, Magodi Mbamba Mbano, Mtekateka Muyamuya Tawete, Fratela Fusi Gama.

Manduna wengiwe ni Maji ya kuhanga Komba, Zimanimoto Gama, Mpambalyoto Soko Msalawani, Mtepa Hawaya Gama na Nduna Mkomanile ambaye alikuwa ni mwanamke pekee kuwa nduna.

Nduna Songea Mbano alikuwa ni maarufu kuliko manduna wenzake na hata chifu Mputa Gama alikuwa anamtegemea sana katika kuwaongoza Manduna wenzake na wapiganaji wa vita ya Majimaji kiujumla.

Mhifadhi kiongozi wa Makumbusho ya Taifa Maji maji Songea Philipo Maligissu akizungumzia maisha ya Nduna Songea Mbano katika viwanja vya Makumbusho hayo,alisema kuwa Songea Mbano akiwa miongoni mwa manduna alitokea kuwa maarufu sana ukilinganisha na wenzake 11  ambapo sifa kubwa iliyo mpa umaarufu ili kuwa ni ueledi na ushadi wake wa kuandaa mikakati ya kivita, na maamuzi mazito yasiyoteteleka na kuyasimamia maamuzi hayo kikamilifu.

Kwa umakini mkubwa Nduna Songea Mbano aliweza kufanya kile alichokuwa akikiamini na uthibitisho wa jambo hilo ulianza kujitokeza julai 12, mwaka 1897 katika viwanja vya Bomani kwa mkuu wa Wilaya wa wajerumani luteni Engelhardt.

Maligissu anasema kuwa kwa rekodi zilizopo zinaonyesha kuwa tarehe hiyo Nduna Songea Mbano alionekana kuwa ni mtu wa kipekee katika idadi ya Manduna 11 ambao walikuwa wasaidizi wa chifu Mputa Gama kwa kitendo chake cha kubisha wazi wazi tamko la utawala mpya wa wajerumani la kutaka wangoni wakomeshe biashara ya utumwa.

Siku hiyo ilikuwa ni siku rasmi ambayo utawala wa kikoloni ulikuwa unaanzishwa katika mji wa Songea wakati huo ulikuwa unaitwa Ndonde na Mkoa wa Ruvuma kiujumla chini ya Luteni Engelhardt wa Jeshi la Kijerumani ambaye alikuwa ndiye Mkuu wa Jeshi kwa kanda ya Kusini.

Wajerumani walipofika kuanzisha makoloni yao katika maeneo ya ukanda wa kusini walikutana na msuguano mkubwa kutoka kwenye tawala za kiafrika hususani tawala za wangoni.

Maligissu anasema kuwa wangoni walikuwa na tabia ya kwenda mikoa ya Lindi na Mtwara kuvamia na kuchukua mateka na kuwaleta Songea kuwafanyisha shughuli mbalimbali katika maeneo yao ya utawala.

Tabia hiyo ya wangoni iliwachukiza sana wajerumani kwani wajerumani walikuwa wanaheshimu sana makubaliano yaliyofikiwa kutoka kwenye mkutano wa Berlin wa mwaka 1884 hadi 1885.

Katika mkutano huo moja ya makubaliano yaliyofikiwa ni pamoja na kila nchi yenye koloni barani Afrika ni lazima ikomeshe biashara ya utumwa na kwa kuwa wajerumani walikuwa wamejiimarisha sana katika mikoa ya Lindi na Mtwara.

Hivyo walipokuja Ruvuma wakatoa tamko kwa wangoni kuwa hairuhusiwi na haitaruhusiwa tena kwenda Lindi,Mtwara na maeneo mengine kuchukua mateka na kwamba mateka wote waliochukuliwa na wangoni waachiwe huru.

Baada ya wajerumani kutoa tamko hilo ndipo Nduna Songea Mbano alipojitokeza waziwazi na kusimama kujibu hoja iliyotolewa na wajerumani kuhusiana na tamko hilo.

Nduna Songea Mbano alisema kuwa utawala wa kabila la wangoni hauwezi kutekeleza tamko hilo na kwamba msimamo wao ni kutoutambua utawala mpya wa kijerumani na tamko lao.

Aliendelea kusema kuwa ujio wa utawala wa wajerumani na kutoa tamko hilo kwa wangoni  una lengo la kudhoofisha utawala wa Machifu na Manduna katika maeneo yao kwa kufuata kanuni zao za kimila na kitamaduni.

Kuanzia hapo wajerumani walimuona Nduna Songea Mbano kuwa ni mtu hatari sana katika utawala wao mpya na walimuweka alama maalumu na kuanza kumfuatilia nyendo zake.

Kwa sababu alionekana kuwa kiongozi shupavu na mwenye misimamo mikali na anayezingatia heshima na utu wa kabila lake bila kuyumbishwa.

Alionekana kuwa ni mtu wa pekee mwenye uwezo mkubwa wa kufanya kazi katika mazingira yoyote kwa kushirikiana na wananchi wake ambao walikuwa wana mheshimu sana na kumsikiliza.

Maligissu anaeleza kuwa Nduna Songea Mbano alikuwa na uwezo mkubwa wa kuwaunganisha wananchi wake na kuwa na umoja, upendo na mshikamano na kwamba alikuwa akiwaelekeza jambo wanalifanya kwa umakini na kwa ukamilifu.

Anaendelea kusema kuwa kuanzia hapo Nduna Songea Mbano aliendelea kujizolea umaarufu mkubwa na wajerumani baada ya kuona hivyo na kitendo cha nduna Songea kutamka kuwa yupo tayari kwa lolote lile na hawezi kukubali kuona tawala za kiafrka zinadharauliwa na wakoloni kwa namna yeyote ile.

Waliamua kuwaalika Machifu na Manduna wote Julai 13 mwaka 1897 Bomani kwa mkuu wa Wilaya wa kwanza katika nchi ya ungoni ambaye pia mkuu wa jeshi la wajerumani katika nchi ya ungoni Luteni Engelhardt na kuwaambia kuwa mtu yoyote katika eneo lake atakaye kaidi amri yeyote  kutoka kwa uongozi mpya wa wajerumani basi atapigwa risasi, kunyongwa hadi kufa au kufungwa maisha .

Siku hiyohiyo Machifu na Manduna walichukuliwa hadi juu ya mlima wa shabaha wa chandamari uliopo katikati ya mji wa Songea na kuwaonyesha nguvu ya risasi inavyoweza kufanya kazi katika mwili wa binadamu na kwamba silaha za kijadi na kimila za wangoni haziwezi kufua dafu mbele ya silaha hizo.

Licha ya wajerumani kutoa  mkwara na vitisho vingi Nduna Songea Mbano aliendelea kushikilia msimamo wake wa awali wa kuchukia utawala wa wajerumani na kuutetea utawala wa kiafrika mpaka vilipo kuja kutokea vita vya Majimaji.

Nduna Songea Mbano alitoa ushindani mkubwa sana katika vita hivyo na alionyesha ustadi mkubwa kwenye mapigano na katika sehemu zote ambazo wajerumani walipigana wameandika kuwa hawakupata ushindi mkubwa kama waliopata katika Mkoa wa Ruvuma zamani nchi ya ungoni.

Ambapo viongozi wao hawa kuwa wanafiki kwani walijitoa kikwe likweli kusaka ukombozi wa kweli na hadhi ya tamaduni zao mpaka dakika ya mwisho, ndio maana idadi ya watu walionyongwa katika historia ya nchi yetu walitoka katika himaya ya Nduna Songea Mbano na ushahidi upo wazi kuwa watu 67 walihukumiwa kunyongwa hadi kufa akiwemo Nduna Songea Mbano.

Katika kuonyesha kuwa Nduna Songea Mbano alikuwa na uwezo wa kufanya mambo kwa uweledi mkubwa bila kusaliti dhamira yake kuanzia mwaka 1897 alianza kuandaa jeshi lake la kupambana na utawala wa wajerumani.

Akaanza kuchukua watu wake na kuwapeleka juu ya mlima wa chandamari, kufanya nao mkutano na kutoa mafunzo ya kivita na kuwaelekeza kwa nini wanawachukia wajerumani.

Katika mlima huo ndipo alipoeleza kwa kina madhara ya kuukubali utawala wa wajerumani na kutoa ahadi kwa wananchi wake ya kuwaondoa wajerumani kwa lazima na kwamba alisema kuwa eneo hilo ni lao na wamekuwa wakiishi siku zote chini ya utawala wao sasa inakuwaje waletewe utawala mpya wakati hawahuitaji.

Chokochoko hizo zilizaa vita vya Majimaji na wakati mapigano yakiendelea wajerumani walianza kumtafuta Nduna Songea Mbano ili wamkamate na kufanya nae mazungumzo ya maridhiano.

Kumbe Songea Mbano alikuwa amejificha kwenye pango kubwa lililopo kwenye mlima wa chandamari na usiku hukutana na askari wake nje ya pango hilo na kuwapa mafunzo zaidi ya kivita.

Maligissu anaeleza kuwa Nduna Songea Mbano alikuwa anaishi na Ndugu zake katika eneo la Mateka lililopo katika eneo la Manispaa ya Songea na wakati wa vita ndipo Songea Mbano alikuwa anajifisha katika pango hilo ili wasimkamate mpaka atakapotimiza malengo yake.

Wajerumani walipoona wanaendelea kupata madhara makubwa kutokana na vita hivyo waliamua kuwakamata ndugu na familia yake, chifu Mputa Gama na Manduna wengine na kuwafunga gerezani kwa lengo la kumdhoofisha Nduna Songea Mbano.

Baada ya wajerumani kumdhoofisha Nduna Songea Mbano alipata taarifa zote na akaamua kutoka kwenye pango hilo na kwenda kwa wajerumani na kutaka watu wake waachiwe ili mapigano yaendelee.

Ndipo naye alipokamatwa na kuwekwa gerezani na kwamba utawala wa wajerumani waliamua kuwa hukumu wafugwa hao kunyogwa hadi kufa akiwemo chifu wa kabila la Wangoni.

Wafungwa hao waliamuliwa kuchimba shimo kubwa bila kujua kuwa shimo hilo ndilo litakalotumika kuwa kaburi lao na ilipofika siku ya kunyongwa walinyongwa kwa zamu siku mbili na maiti zao kwenda kuwekwa kwenye kaburi hilo hadi walipofikia 66 ndipo walizikwa kwa pamoja kwenye kaburi hilo.

Nduna Songea Mbano walimuacha ili aweze kuwasaidia kufikisha malengo yao kwa wananchi kwani waliamini kuwa yeye ni kiongozi jasiri na anayependwa na watu wake na kusikilizwa vizuri.

Toka siku hiyo walipomuacha bila kumnyonga Nduna Songea Mbano aliwasumbua sana wajerumani na kutaka naye anyongwe kama ndugu zake kwani haoni sababu ya yeye kuishi wakati ndugu zake wamekufa na kusema kama hawataki kumnyonga basi hataki kula wala kunywa  chochote mpaka afe.

Ndipo wajerumani walipoamua kumnyonga na kumzika katika kaburi la pekee yake wakiamini kuwa ni mtu wa pekee mwenye ushujaa na maamuzi mazito na misimamo isiyoyumba na walimuenzi kwa kubadilisha jina la mji wa Ndonde na kuubatiza jina la Songea ambapo mpaka sasa linatumika kuuita mji huo wenye hazina kubwa ya historia na utalii wa kitamaduni

Kila mmoja wetu hana budi kujiuliza ni mafundisho yepi anaweza kuyapata katika historia ya nchi yetu na mchango mkubwa alioutoa Nduna Songea Mbano na je kizazi kilichopo tunao ule moyo wa ushujaa , uzalendo heshima na usawa kama ilivyo kuwa kwa mababu zetu basi inatupasa tutimize wajibu wetu kikamilifu ili vizazi vijavyo viweze kunufaika na uwepo wetu duniani.


Mwandishi wa makala hii
Anapatikana kwa simu namba  - 0755 – 335051

STEPHANO MANGO

Mwandishi wa Habari wa Kujitegemea Songea  Stephano Mango akiwa anatafakari Jambo nje ya Hotel ya Ok 92 ilyopo Songea Mjini

WAANDISHI WA HABARI

Mwenye Miwani Ni Mwandishi wa Habari Mwandamizi wa IPP Media Gideoni Mwakanosya akiwa na Mwandishi wa Kujitegemea Stephano Mango Wakiwa Nje ya Chuo Cha EASY TECH. COMPUTER TRAINING CENTRE Kilichopo Songea Mjini.